RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 29


MTUNZI:ENEA FAIDY

.....MR Aloyce alizidi kumkazia macho mkewe akahisi ni mrembo zaidi ya Mama Eddy yule anayemfahamu yeye. Halafu alikuwa na madaha sana kuzidi vile alivyomzoea. Wasiwasi ukamtanda akilini make na kumfanya asimwamini sana mwanamke yule kuwa ndiye mkewe halisi.

"Mbona unaniangalia sana? Umemisi busu langu nini?" Aliuliza Mama Eddy.
"Hapana wala usijali"
"Ok kama wewe hukumiss basi Mimi nilimisi sana kiss lako mpenzi".

Alisema Mama Eddy huku akimsogelea Mr Aloyce kwa ukaribu zaidi na kumshikashika kidevu kwa mahaba. Mr Aloyce alionesha kutojali mguso ule aliopapaswa na mikono laini ya mkewe. Hakuelewa ni sababu zipi zilizomfanya asimjali mwanamke yule kwa kiasi kile ila moyo wake ulikuwa mzito sana.

"Baby mbona hivyo...? Embu usiwashe gari kwanza mpaka unibusu" alisema Mama Eddy kwa sauti iliyojaa mdeko wa kimahaba. Mr Aloyce hakutaka kukiri udhaifu, akaachia usukani na kusogeza mdomo wake karibu na mdomo wa mkewe kisha akambusu.

Busu lile lilimpa nafasi nzuri sana Mama Eddy ya kupenyezapenyeza mpaka kuingiza ulimi wake mdomoni kwa Mr Aloyce. Kisha wakabadilishana mate yao kwa mahaba. Lakini wakati tendon hilo likiendelea, Mwanamke yule alimwachia vitu Fulani Mr Aloyce bila yeye mwenyewe kujua. Na ilikuwa ni dawa Kali ya kumfanya Mr Aloyce amwamini mwanamke yule kuwa ndiye mkewe halisi wakati hakuwa yeye. Alikuwa ni mwanamke kutoka himaya ya akina Doreen na alitumwa nyumbani kwa Mr Aloyce ili afanye kazi muhimu sana aliyotumwa. 
Kwa vile alivyomfanyia Mr Aloyce, alifanikiwa kuziteka akili za Mwanaume yule. Baada tu ya busu lile la huba, Mr Aloyce alijkuta akimpenda sana mwanamke yule akijua ndie Mkewe halisi na kumbe haikuwa hivyo. Wasiwasi wake ulifutika kichwani mwake, pendo la dhati likatawala moyoni mwake.

"Tuondoke mume wangu" alisema mama Eddy kwa sauti ya upole iliyojaa huba huku akiwa ameachia tabasamu pana usoni mwake.

"Usijali mke wangu.. Nilikukumbuka sana... Nina imani hata mwanetu anakusubiri kwa hamu sana." Alisema Mr Aloyce huku akishikilia vizuri usukanu na kuondoa gari kwa kasi sana.
Mr Aloyce aliendesha gari kwa kasi ya ajabu na baada ya masaa machache tu waliwasili eneo la Ipogoro Iringa kisha wakaelekea nyumbani kwao. 

Walifika getini wakapiga honi geti lilifunguliwa. Mr Aloyce aliegesha gari pembeni kisha akashuka kwa furaha kubwa, na baada ya hapo akaelekea upande wa pili wa gari yake na kumfungulia mkewe huku tabasamu mwanana likiwa limechanua mdomoni mwake.

"Shuka malkia wangu... Tumeshafika kwetu.." Alisema Mr Aloyce huku mwanamke yule anayefanana kwa kila kitu na Mama Eddy akishuka kwa madaha kisha akamkumbatia Mr Aloyce na kumbusu. Wakati yote hayo yakiendelea Mlinzi alikuwa pembeni yao akishuhudia penzi la zamani lililochipua upya tena kwa kasi ya ajabu.

"Mh bosi naona mama Amerejea.." Alisema mlinzi kimzaha.
"Ndio.."alijibu Mr Aloyce kwa furaha.
"Baby nataka kuongea jambo na mlinzi wetu naomba utuache kidogo.." Alisema Mama Eddy.
"Ok ila kuwa makini tu nisije kupinduliwa na houseboy.." Alisema Mr Aloyce na kuondoka zake huku akimsisitiza mkewe asichelewe.

Baada ya Mr Aloyce kuondoka pale, Mwanamke yule alimsogelea mlinzi na kumtazama kwa ghadhabu Kali. Hali hiyo ilimtisha sana mlinzi na kumfanya ajiulize maswali mengi ambayo alishindwa kujijibu mwenyewe.
****
 
Mama Pamela aliishiwa nguvu kabisa. Alijiuliza sana ni kwanini mwanaye amelala chooni kule ilhali ana kitanda kizuri cha kumfaa? Maswali yake hayakuwa na majibu akajikuta anaishia kupiga makofi kwa mshangao.

"Pamela!" Alimwamsha mwanae ambaye bado alionekana ana usingizi mzito sana. Alimtikisa tikisa mpaka alipofanikiwa kumwamsha kabisa. Pamela aliinuka, lakini alibaki mdomo wazi baada kuona mazingira aliyopo si ya kitandani kwake.

"Mama nipo wapi hapa? Mbona kama chooni?" Aliuliza Pamela kwa mshangao.
"Nikuulize wewe mwanangu.. Umefikafikafikaje mpaka ukalala chooni?" Aliuliza Mama Pamela.
"Mbona sielewi mama" alisema Pamela.
"Haya chukua hilo shuka lako twende chumbani.. Hayo mengine tutajua huko huko.." 

Walitoka chooni mle na kuelekea chumbani kwa mama Pamela. Pamela alitoa nguo aliyokuwa amevaa kwaajili ya kulalia kisha akavaa nyingine kwani ile tayari ilishapata unyevunyevu wa chooni.
"Lakini mama mbona Doreen hatujaenda kumwangalia si atahisi tunamtenga.." Alisema Pamela.
"Ila kweli"

"Tumfate basi.." Alisema Pamela kisha wakainuka na kwenda chumbani kwa Doreen. Kulikuwa na Giza totoro ambalo bila msaada wa tochi basi wasingeona chochote. Walimulika kitandani kwa Doreen na kumwona Doreen akiwa amelala fofofo. Walimsogelea kwa ukaribu na kumwamsha lakini Doreen hakuitikia. Pamela na mama yake walitazamana mshangao.

"Mbona haamki?" Walinong'ona taratibu.
"Isije ikawa ndo amek.. Amepata matatizo mengine" alisema Pamela.
"Doreen! Doreen" Mama Pamela aliita kwa sauti kubwa lakini Doreen bado hakuamka.

"Tumuache basi tutamkuta kesho yawezekana mwenzetu hajakumbwa na mauzauza" alisema Pamela kisha wakarudi chumbani kwa Mama Pamela kupumzika kidogo maana Pamela asingeweza kulala peke yake kutokans na woga aliokuwa nao kwa usiku ule.
***** 
"Umeshika nini hicho Mansoor" aliuliza Dorice kwa woga .
"Nimeshika Pete" alijibu Mansoor. Jibu hilo lilimshangaza Dorice kwani alichokiona mkononi kwa Mansoor haikuwa Pete Bali alikuwa nyoka mkubwa aliyejiviringisha kama Duara kiganjani kwa Mansoor. 

"Pete gani hiyo?" Dorice alizidi kuogopa.
"Ni pete ya kukupa wewe ili uwe na nguvu ya kurudi duniani na kufanya lolote utakalo..."
"Mbona namuona Nyoka?"
"Fumba macho kisha ufumbue nikikuruhusu" alisema Mansoor kisha Dorice alifanya kama alivyoambiwa.
Mansoor alisogeza mkono wa Dorice kisha akchuku kidole Chanda na kumwambia Dorice afumbue macho yake.
Dorice alifumbua macho yake na kutazama kidole chake. Alishtuka kuona pete inayong'aa sana kidoleni mwake.

"Umenivisha SAA ngapi?"
"Nimekuvisha ulipofumba macho"
"Mbona sikuhisi chochote? Na je yule nyoka yuko wapi?"
"Sikushika nyoka.. Nilishika pete" alisema Mansoor.

Ghafla Dorice alijiona wa tofauti sana. Kichwa kikaanza kumgonga kwa kasi sana, akaanza kulalamika. Na kadri alivyolalamika ndivyo kadri maumivu yalivyomzidia.

Machozi yalianza kuchuruzika lakini cha ajabu, matone ya machozi yake hayakuwa ya kawaida kwani kila tone alilodondosha lilikuwa damu. Dorice alijishangaa sana lakini Mansoor akaangua kicheko kikali kilichomshangaza Dorice.

ITAENDELEA......
RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 29  RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 29 Reviewed by WANGOFIRA on 22:35:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.