MIKAKATI YA AWAMU YA TANO KUBORESHA MASLAHI YA WAALIMU
NA, BARAKA NGOFIRA
Walimu ni miongoni mwa wafanyakazi wa
serikali ambao kwa muda mwingi wamekuwa wakiilalamikia serikali kuhusu
mazingira na hata maslahi yao. Kwani wengi wamekuwa wakiishi mazingira magumu
na hivyo kupelekea kupungua kwa ufanisi wa kazi zao.
Naandika makala haya nikijua fika maisha
halisi wanayoyaishi waalimu hususani wale waishio vijijini, wengi wao wakiishi
nyumba ambazo hazina hadhi nyingi zikiwa na mchwa ambao kwa namna moja ama
nyingine huwasaidia kutunza karatasi za wanafunzi au daftari pale
wanapozisahau.
Shule nyingi hazina nyumba za walimu
jambo linalopelekea walimu wengi kujibana kwenye nyumba ambazo zipo. Au wengine
kuishi kama wanafunzi wa bweni kwa kuishi kwenye chumba kimoja walimu wawili au
zaidi. Jambo linalopelekea kukosa faragha miongoni mwao kwani hayo ya maisha ya
kuishi hivyo yashapita, lakini kwa sababu ya kuipenda kazi yao hawana jinsi
kufanya hivyo ili waweze kupata tonge la ugali.
Naandika makala haya kwanza kuwapongeza
na kuwashukru walimu wa simiyu ambao wameishi jikoni kwa zaidi ya miaka miwili
sasa, lakini kamwe hawakuthubutu kuacha kazi , kuomba uhamisho au kutishia
kugoma kama wenzao katika maeneo mengine wafanyavyo. Kwangu mimi nawawaambia
hongereni sana kwa ujasiri mkubwa mliokuwa nao wa kuishi ndoto zetu za kuwa
walimu na si kama wengine ambao naweza kusema walishtuka wakajikuta wamekuwa
walimu. Ambao kimsingi ndo wale wanaokuwa mstari wa mbele kudai mishahara pale
inapochelewa hata kwa siku moja.
Wamekuwa mfano wa kuigwa na kielelezo chema
kwa wale wote walio kwenye fani ya ualimu na nyingine za serikali na binafsi kwa
kujua shida iliyonayo serikali yetu ambayo kwa awamu hii, Mungu akimjalia uzima Rais wetu Dr. Magufuli
naamini kuwa mtajengewa mazingira bora ya kazi. Kwani kinachonifurahisha ni
kwamba ameyaishi maisha ya ualimu kama kazi yake ya kwanza kuifanya miaka ile
ya 1980 kabla hajaenda bungeni.
Kinachonipa ujasiri tena wa kuandika
makala haya ni uchaguzi wa Prof. Ndalichako kuwa waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia
na Ufundi. Kwani naye anaijua vyema hali halisi ya walimu kwani na yeye amekuwa
mwalimu kwa hili sina shaka kabisa. Kuwa atajitahidi kwa kadri awezavyo
kulishawishi bunge kumpa bajeti kubwa kwa ajili ya kujenga mazingira yaliyo
rafiki kwa walimu.
Na si kwamba nawapigia debe walimu au
kwa sababu nimetokea katika familia ya kiualimu, la hasha! Penye ukweli lazima
tulonge pasipo hata kupepesa macho, ni lazima tuambizane ukweli wa mambo
yalivyo.
Japo tunategemeana lakini mwalimu bado
ataendelea kuwa mwalimu na mtu wa muhimu sana katika maisha ya mwanadamu
yeyote. Hata kama ukibisha ukweli utabaki pale pale mwalimu anatutoa kwenye
wimbi la ujinga na kutufanya tuwe welevu na baadaye wengine ugeuka na
kuwadharau hasa walimu wa shule za msingi ambao kimsingi ndiyo waliowafanya
wafike hapo walipo.
Jambo ambalo kiukweli ukikaa na
kulitafakari kwa kina tena mara mbilimbili utagundua thamani aliyonayo mwalimu
katika jamii zetu. Nakumbuka maadui watatu ambao Hayati Baba wa Taifa hili
Mwalimu J.K Nyerere alisema nchi hii inakabiliwa na maadui watatu ambao ni
Ujinga, Umaskini na Maradhi. Sasa kama utamdharau mwalimu nani atautoa ujinga
vichwani mwetu?
Mwingine anaweza sema nitaenda kujisomea
maktaba au kwenye mtandao kwa sababu ya kukua kwa teknolojia na kusahau enzi
zile alizokuwa anakimbia na vizibo vya soda akifundishwa kuhesabu, pia kipindi
kile anaandika chini akijifunza kuandika “a, e, i, o na u”.
Pia kwa wale waliokuwa na akili nzito ya
kushika wanasahau jinsi ambaavyo walitandikwa japo kidogo na kuambiwa hii ni “a
au ni u” au kuhesabu namba 1 mpaka 10. Ambaye pasipo shaka yeyote vilimpa shida
sana kukariri lakini leo utashangaa anakuambia mwalimu hana faida kwangu kisa
tu yeye si mwalimu.
Ebu tugeuze mielekeo ya mawazo yetu ili
tuiunge mkono serikali yetu ya awamu ya tano ambayo ninaamini ina dhamiri ya
dhati kabisa ya kuondoa ujinga kwa watanzania wote. Na kamwe ujinga hauwezi
kuondoka pasipo walimu kutengenezewa mazingira mazuri ya kufanyia kazi, ikiwemo
mishahara mizuri, kujengewa nyumba ambazo watishi na kufurahia kazi yao.
Narudia kuwapongeza sana walimu wawili
wa Simiyu waliovumila kuishi jikoni kwa muda wa miaka miwili na zaidi pia wale
ambao wanavumila kuishi na michwa ndani ya nyumba zao ambayo inawasaidia
kutunza karatasi na madaftari ya wanafunzi pale wanaposahau au kudondoka chini,
bila kuwasahau wale wanaoishi nyumba zilizo sawa na mapango ambazo ukiziangalia
kwa nje hauwezi kuamini kuna binadamu anayeishi ndani ya jengo hilo.
Huu ndio uvumilivu na uthamani wa kazi
ninaouandikia makala haya waswahili husema “Heshima kazi” au “Acha kazi uone
uthamani wake”. Haya ndiyo maisha halisi ya walimu ambao wamemfundisha kila mtu
ambaye kwa namna moja ama nyingine anaajiona aana umuhimu mkubwa kwenye jamii
kuliko mwalimu wake.
Hivyo basi ni ombi langu kwa wadau wa
Elimu nchini Tanzania waunganishe nguvu na watanzania wote kuhamasishana
kujenga nyumba za walimu ili walimu wanapoajiriwa waweze kuishi maisha yenye
uafadhali. Ambayo itawasaidia kuwajengea moyo wa wao kujituma na kufanya kazi
kwa ufanisi zaidi kwa kujengewa mazingira rafiki. Kwani hata wataalamu wa
masuala ya kitaaluma wanashauri kuwa ili ufanisi wa kazi uwe wa weredi zaidi,
mazingira bora ya kufanyia kazi ni muhimu zaidi ili kuongeza mazao na mapato ya
kazi wanazozifanya.
Pia nina imani kubwa na serikali ya
awamu ya tano chini ya waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi Prof.
Ndalichako ambaye kitaaruma ni mwalimu. Kuwa maisha bora ya walimu yataboreshwa
ili waweze kuongeza ufanisi wa kazi zao za kuondoa ujinga kwa watoto na wadogo
zetu ambao kesho na kesho kutwa watakuwa viongozi wakubwa kwenye nchi yetu na
duniani kwa ujumla.
Kwa sababu pia dhamira ya serikali ya
awamu ya tano ni kujenga Tanzania yenye wataalamu waliobobea kutokana na Elimu
inayopatikana kutoka kwenye Shule na Vyuo vya hapa nchini. Ni imani yangu kuwa
waziri mwenye dhamana atapambana vilivyo ili kuhakikisha kuwa tunajenga
Tanzania ya watu wenye Fikra chanya na watu wanaofikri mara mbilimbili ili
kuvuta mataifa mengine ya duniani yaweze kuleta watu wao kuja kusoma hapa
nchini. Kama sisi tupelekavyo wataalamu nje ya nchi kwenda kusoma na kupata
ujuzi mbalimbali na kuja kuutumia hapa nchini.
Hivyo ni ombi langu kwa waanaanchi na
wadau wa elimu kuunga mkono serikali kwa kujitolea kwa mioyo ya dhati, kama
tulivyoshiriki kwenye ujengaji wa shule na maabara za shule za sekondari.
Tufanye hivyo kwa kushirikiana kujenga nyumba za walimu ili wajapo kuripoti
kwenye vituo vyao vya kazi wafanye kazi na si kila siku kulalamika. Kwani muda
wa malalamiko umeshapita na Sasa ni Kazi Tu. Ili wale wasioweza kazi wakae
pembeni na wa kazi waendelee tuijenge Tanzania iliyo imara na kuwa mfano wa
kuigwa.
Makala haya yameandaliwa na mwanafunzi
wa Mawasiliano kwa Umma katika Shule Kuu ya Uhandishi wa Habari na Mawasiliano
kwa Umma ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Anapatikana kwa mawasiliano ya
0763580901, 0716216249 au barua pepe ya barakangofira@gmail.com
MIKAKATI YA AWAMU YA TANO KUBORESHA MASLAHI YA WAALIMU
Reviewed by WANGOFIRA
on
11:18:00
Rating:
No comments: