MWANAMKE USIPOTHAMINI MTOTO, HAKUNA ATAKEYEMTHAMINI

.
na Baraka ngofira


Image result for picha za ukatili kwa watoto 
( picha za watoto waliofanyiwa vitendo vya  kikatili. picha kwa Hisani ya IIP MEDIA)
Mwanamke ni mama wa familia, na kiimani amebeba uponyoji wa mwanaume kwa kuwa  ametokana na ubavu wa mwanaume. Hivyo mwanaume amebeba vidonda kwa ajili ya mwanamke na kwa sababu hiyo basi  wawili huishi pamoja kwa kushirikiana katika kutekeleza majukumu mbalimbal
i.
Ukiachilia mbali nafasi mbalimbali ambazo baadhi ya waandishi wa kazi za kifasihi kumwandika na kumchora mwanamke katika mitazamo hasi, lakini bado mwanamke atabaki kuwa, ni  jasiri kwani naamini kuwa kama ingekuwa mimba ina zamu ya kulea na kuibeba, sina shaka kuwa wanaume wengi wasingekubali kukaa nayo hata kwa siku moja. Na hivyo ingemlazimu mama kuibeba tena mpaka atakapojifungua. Na hapo kidogo ndipo mwanamme angejifunza thamani ya kubeba mimba na kuilea kwa muda wote wa miezi tisa mpaka kuijifungua na kuendeleza malezi ya mtoto wake.
Pia, ni mchapakazi, mchumi, mwalimu yaani waswahili wanasema katika kila sekta yuko vizuri. Na kama hauamini angalia wanawake wengi wakienda kufanya manunuzi sokoni, wanavyopiga bajeti ili pesa aliyopewa hata kama ni kidogo itoshe kununua mahitaji na ikiwezekana ibaki walau salio kidogo la kuanzia kesho au akanunue vocha.
Huyu ndiye mwanamke ambaye baadhi ya wanaume umdharau bila kugeuka nyuma na kuangalia upande wa pili wa sarafu, kwa haya anapaswa pongezi kubwa kwani si jambo la kawaida kwa shughuli anazozifanya.
Ukienda kijijini utamkuta mwanamke kabeba mtoto mgongoni, ndoo ya maji kichwani, bado kuni juu ya ndoo ya maji, jembe mkononi na mengine kibao. Huku mme wake akitembea tena kwa ujasiri kabisa na jembe lake moja bila hata wasiwasi wowote. Na mara tu wafikapo nyumbani bado mwanamke huyu huyu anashughulika na kuwasha moto wa kuni au mkaa ili aandae chakula cha familia huku baba akiwa amestarehe kabisa. Na pengine akimfokea mwanamama huyu kwa nini chakula hakiivi haraka.
Lakini pamoja na kuwa na sifa zote hizo baadhi yao siku hizi wamegeuka na kuwa zaidi ya simba au chui kwa vitendo ambavyo vimekuwa vikilipotiwa na vyombo vya habari na matukio mengine kusambazwa kwenye mitandao ya kijamii.
Siku hizi imekuwa ni kawaida sana kusikia mtoto kawekwa kwenye jokofu na wengine kubanikwa kwenye “oven” na baadhi ya wadada wa kazi, mara utasikia mtoto kachomwa na pasi ya umeme eti kisa kaiba shilingi mia tano. Hii inasikitisha sana kwa watu ambao jamii inawaamini lakini kwa sasa imani imeanza kupungua kwa wadada hawa wa kazi.
Ukiachilia mbali wadada wa kazi wapo baadhi ya wakina mama ambao naweza kusema hawaujui uchungu na pia naweza kusema kwao watoto ni kama waliwaokota tu na hawakuingia kwenye chumba cha kujifungulia maarufu kama leba. Kwani karibu kila mwezi utasikia mtoto katupwa mtaroni au karibu na jaa la taka. Na hapa ndipo najawa na wasiwasi kama huyu mtu aliyefanya kitendo hiki ana akili timamu au kidogo waswahili usema zimempita kushoto.
Hii inasikitisha sana na huleta hisia kali mkiongoni mwa wanajamii na baadhi ya mashirika ya kutetea haki za kibinadamu na watoto kuhusu ukatili huu wanaofanyiwa.  Labda kidogo niwakumbushe video ambayo ilikuwa maarufu sana mwishoni mwa mwaka 2014, ambayo ilikuwa ikimwonyesha mfanyakazi wa ndani  huko nchini Uganda alivyokuwa akimpiga mtoto ambacho kwangu naweza sema ni kipigo kitakatifu. Ilikuwa ni video ya kusikitisha na baada ya maamuzi ya mahakama ya kumfunga miaka mitatu jela lakini bado wanaharakati wa haki xza watoto bado hawajaridhika na adhabu hiyo.
Na hapo ndipo usemi usemao uchungu wa mwana haujuaye mama lakini cha ajabu baadhi ya mama hawaujui kiukweli uchungu  na thamani ya mtoto au watoto wao. Chonde chonde dada zangu mtatia aibu na heshima na thamani yenu inashuka kwani hakuna mwanaume yeyote anayependa kuwa na mwanamke katili, kwani wengi wao wafanyao vitendo hivi ni wale hata bado kwenye ndoa hawajaingia.
Namalizia kwa msemo mmoja wa Kiswahili usemao “ Usipoziba Ufa utajenga ukuta” na “ Mchelea mwana hulia mwenyewe” kwa maana uchungu wa mwana aujuaye mama hivyo Napata ujasiri wa kusema kama mama asipothamini uchungu wake kwa mwanaye hakuna atakaye weza kuthamini na kamwe baba hatojali mtoto kama mama ukishindwa kumtunza mwanao.




MWANAMKE USIPOTHAMINI MTOTO, HAKUNA ATAKEYEMTHAMINI MWANAMKE USIPOTHAMINI MTOTO, HAKUNA ATAKEYEMTHAMINI Reviewed by WANGOFIRA on 23:19:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.