Sheria inamtoa hatiani kwa kosa la jinai mtoto wa kiume aliye chini ya miaka 12

KWA kipindi kirefu kati ya miaka ya 1996 hadi mwanzoni mwa mwaka 1998, Tanzania kama nchi ilishuhudia kuongezeka kwa kiasi kikubwa makosa ya jinai yanayohusiana na ngono.


Kwa wengi waliokuwa wakifuatilia vyombo vya habari walikuwa mashahidi wa kile wanasheria wa makosa ya jinai wanachokiita crime rate, kukua kwa kiasi cha kutisha.

Hata hivyo, mwaka 1998 Bunge la Jamhuri la Muungano wa Tanzania lilitunga sheria inayoitwa Sheria Maalumu ya Makosa ya Kujamiiana au kwa lugha ya kigeni ‘Sexual Offences Special Provisions Act’ au kwa kifupi SOSPA.


Sheria hii ilitiwa saini na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wa wakati huo, Benjamin Mkapa Julai mwaka 1998.

Kwa kiasi kikubwa sheria hii ilikuwa kama shubiri wa tatizo la makosa ya kujamiiana kama ubakaji au kufanya ngono kinyume cha maumbile katika jamii yetu.

Leo tutaiangalia sheria hii, yaliyomo, adhabu zake na mabadiliko katika sheria hii.

Kwa kiasi kikubwa, sheria hii imekuja kufanya mabadiliko katika sheria kadhaa za makosa ya jinai kama vile Kanuni ya Adhabu (sura ya 16 ya sheria za Tanzania) Sheria ya Ushahidi na Sheria ya Mwenendo wa Makosa ya Jinai.

Hivyo sehemu ya kwanza ya sheria hii imefanya mabadiliko katika sheria ya kanuni za adhabu.

Ndani ya sheria hii mvulana ametambuliwa kama mwanamme aliye chini ya miaka 18.

Hii ina maana kwa mtoto wa kiume kutambulika kama mtoto, umri wake ni lazima uwe chini ya miaka 18, wakati kwa msichana, yeye ametambulishwa kama mwanamke aliye chini ya miaka 18 pia.

Chini ya kifungu cha 4 cha sheria hii, kanuni ya adhabu imefanyiwa marekebisho na kwa sasa kwa mtoto ambaye ‘hajakomaa’ (immature) umri wake ni ule ulio chini ya miaka 10.

Kisheria, mtoto huyo hawezi kuwa na mashitaka wala hatia ya makosa ya jinai hata hivyo, marekebisho yaliyofanyika kwenye kifungu kidogo cha 2 cha kifungu cha 15 cha kanuni za adhabu, kinaelekeza kwamba mtoto aliye chini ya miaka 12 hawezi kuwa na hatia ya kosa la jinai isipokuwa kama wakati anatenda au anaacha kutenda tendo (ambalo ni jinai), itathibitishwa kwamba alikuwa na uwezo wa kujua kwamba hatakiwi kutenda au kutokutenda kosa hilo.

Pia kifungu hiko kinamtoa hatiani kwa kosa lolote la jinai mtoto wa kiume aliye chini ya miaka 12 kwa dhana kwamba hawezi kufanya tendo la ngono, kubaka.

Tofauti na wengi wanavyodhani kwamba kubaka ni tendo la kumlazimisha mwanamke kufanya mapenzi, sheria hii imetoa maana pana ya neno kubaka.

Chini ya kifungu cha 5 cha sheria hii, ambacho kimetengeneza kifungu cha 130 cha Kanuni za Adhabu inasomeka kwamba kubaka ni kitendo cha mtu mwanamme kufanya tendo la ndoa na mwanamke bila idhini au kitendo cha kufanya tendo la ndoa na mwanamke ambaye si mke wake au mke wake lakini waliye tengana naye na bila idhini yake; au kwa idhini yake ambayo imepatikana kwa kutumia nguvu, vitisho.

Au kwa kuweka maisha yake katika hofu ya kifo, kuumia, akiwa katika kifungo au kwa idhini yake lakini idhini hiyo ikiwa imepatikana akiwa katika akili iliyochanganyikiwa kama amelewa kwa dawa aliyopewa na mwanamme huyo, isipokuwa endapo itathibitika kwamba kulikuwa na makubaliano awali, mwanamme atahesabika kuwa amebaka kama atafanya tendo la ndoa na msichana aliye chini ya miaka 18 hata kama msichana huyo atakuwa amekubali kufanya tendo la ndoa kwa ridhaa yake.

Pengine kwa kutambua kwamba kuna aina nyingine za ubakaji, sheria hii chini ya kifungu cha 5 kifungu kidogo cha 3 imetoa maana nyingine zaidi ya kubaka kwa kujumuisha maana hiyo kwa kitendo cha mtu mwenye mamlaka katika ofisi anapofanya tendo la ndoa na mtu wa chini yake kimamlaka au pale ofisa mahabusu zilizoanzishwa kisheria atakapofanya ngono na mahabusu mwanamke.

Maana nyingine ya kubaka ni pale maofisa wa afya au hospitali watakapotumia mwanya wa nafasi zao kufanya tendo la ndoa na mgonjwa msichana au mwanamke; au kwa waganga wa tiba za jadi atakaye tumia mwanya wa nafasi yake kufanya tendo la ndoa na wagonjwa wake wa kike, mtumishi wa dini ambaye kwa kutambua ushawishi wake juu ya waumini wake afanye nao ngono nao (waumini wanawake).

Kosa la shambulio la aibu litahesabika tu pale ambapo mtu akiwa na nia ya kusababisha aibu ya kingono kwa mtu yeyote.

Neno lolote, sauti yoyote, ishara yoyote au kuonekana kwa picha yoyote ikimaanisha sauti mdhaliliko wa kijinsia, atakuwa na hatia ya kufanya shambulio la aibu na kwa adhabu atahukumiwa kwanda jela kwa kipindi kisichozidi miaka mitano (5) au faini isiyozidi sh 300,000 au vyote, jela na faini kwa pamoja.

Lakini kama shambulio hili la aibu linahusisha msichana aliye chini ya miaka 18, mtuhumiwa hawezi kujitetea kwamba msichana huyo aliridhia shambulio hilo.

Katika mitaa yetu, baadhi ya mambo yanakemewa vikali na sheria na bado yanapata nafasi, ikiwamo watu kutumia lugha za kudhalilisha kimapenzi watu wengine.

Tunapaswa tujue kwamba haya ni makosa ya jinai na ni lazima hatua za kisheria zichukuliwe ili kuyakabili kama si kuyatokomeza kabisa.

Biashara ya ukahaba

Kosa jingine ambalo sheria hii imelielezea ni lile kosa la kufanya ukahaba.

Hili nalo ni kosa la jinai chini ya kifungu cha 12 cha Sheria ya Makosa ya Kujamiiana, ambacho ni marekebisho ya kifungu cha 139 cha Kanuni za Adhabu.

Kuna sababu au visingizio mbalimbali ambavyo watu wengi hasa mijini wanavitaja kama ndiyo sababu zinazosababisha jinai hii kutendeka, lakini ukweli ni kwamba biashara ya ukahaba imeshamiri sana.

Pamoja na sababu au visingizio vinavyotolewa na watu mbalimbali juu ya kufanya biashara hii, lakini katika upande wa sheria, hili ni kosa la jinai na adhabu yake imeanishwa katika kifungu cha 139 ni kifungo kisichopungua miaka 10 jela na faini isiyopungua sh 100,000 na isiyozidi sh 300,000 au vyote faini na kifungo kwa pamoja.

Usafirishaji wa binadamu

Pamoja na makosa yaliyotajwa hapo juu, kuna kosa lililoorodheshwa kama kosa la kusafirisha binadamu.

Hili limetambuliwa chini ya kifungu cha 139A kama kilivyorekebishwa na kifungu cha 14 cha sheria hii.

Ndani ya kifungu hiki , mtu yeyote atakaethibitika kwamba anatangaza, anasaidia au anapigia upatu kununua au kuuza au kubadilishana mtu yeyote kwa ajili ya kupata pesa au malipo mengine, iwe ndani au kwa nia ya kusafirisha mtu huyo nje ya Jamhuri ya Muungano, bila idhini ya wazazi au waangalizi wake; au akipata idhini ya mwanamke mjamzito kwa ajili ya pesa na kumuasili mtoto wa mwanamke huyo ambaye hajazaliwa.

Au anawasaidia wanawake hao kupata ujauzito kwa nia ya kuzaa au kama anahusika na usajili wa vizazi, akijua na bado akaruhusu kutoa taarifa zisizo sahihi juu ya uzazi wa wowote au akisajili taarifa zisizo sahihi, pia atakuwa na hatia ya kutenda kosa la kusafirisha watu na adhabu yake ni kifungo si chini ya miaka 20 na kisichozidi miaka 30 na fidia isiyopungua sh 300,000 au vyote, jela na faini kwa pamoja.

Kiasi hiki hata hivyo, kitaamuliwa na mahakama.
Sheria inamtoa hatiani kwa kosa la jinai mtoto wa kiume aliye chini ya miaka 12 Sheria inamtoa hatiani kwa kosa la jinai mtoto wa kiume aliye chini ya miaka 12 Reviewed by WANGOFIRA on 09:23:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.