UBAGUZI KWENYE UTOAJI WA MIKOPO ELIMU YA JUU CHANZO CHA KUUA VIPAJI VYA VIJANA WA KITANZANIA


Na, BARAKA NGOFIRA                                                                                                               
0763580901, 0716216249
Kwanza kabisa nianze kuwashukru wadau wote wa elimu kwa kuonesha juhudi zao kubwa za kuhakikisha wanapigana vilivyo kuhakikisha wanafunzi wote wa vyuo vikuu wanapata mikopo bila kuzingatia fani na masomo wanayoyasoma.
Shukrani zangu za dhati ziwaendee wazazi na wadhamini mbalimbali walioamua kuwasomesha wanafunzi ambao hawakupata mkopo kwa sababu ya vitivo na masomo  wasomayo siyo kipaumbele  “priority” au havina kipaumbele katika kupewa mkopo wa vyuo vikuu.
Sitakuwa na maana ya kuandika makala haya pasipo washukru watanzania wote bila kuzingatia itikadi za vyama vyao kwa kuungana na Rais John Pombe Magufuli katika harakati zake za kutumbua majipu ambayo yalikuwa yamegeuza nchi yetu shamba la bibi kwa kujichotea mali za watanzania bila hata woga ambayo baadhi yao kwa sasa yameanza kutumbuliwa na wengine wameanza kukamuliwa vilivyo ili watapike mali walizotuibia wakidhani hawaonekani.
Inasikitisha sana lakini hamna namna nyingine zaidi ya kutumbuliwa, kwangu nimpongeze Rais Magufuli na timu yake yote ya utendaji  tu nyuma yako hatutakuangusha daima  katika juhudi za kutumbua majipu ambayo yalitutesa na kusababisha watoto wengi wa watanzania kushindwa kusoma elimu ya juu kwa kukosa mikopo. Na wengine kusoma fani ambazo hazikuwa ndoto zao ambapo kwa sasa wamehitimu masomo yao lakini hawajui wapi waende,  kwani hata masomo yaliyoyasoma mioyo yao haipendi bali walisoma kwa sababu tu wapate mkopo na wao kuingia kwenye orodha ya wasomi wenye shahada.
Siwalaumu bodi ya mikopo ya elimu ya juu (HESLB) kwani wao ni watekelezaji tu na ndiyo maana muda mwingi baadhi ya watendaji wao hutujibu vibaya kwani wao hupokea maagizo kutoka kwa wakubwa wao. Lawama na malalamiko haya yanawapasa yawaendee wizara zote katika nchi yetu kwa wao kutopaza kelele na kurizika na kazi walizonazo maofisini kwao, kwani wanadhani wataishi milele kwenye ofisi hizo ambazo wengine wamezigeuza kuwa sehemu na vijiwe vyao vya upigaji na kusahau kuwa walisomeshwa kwa kodi za watanzania ambao leo hii wajukuu wao wanabaguliwa kuwa wao wanasoma vitivo ambavyo si kipaumbele “non priority”.
Wamesahau kuwa  kuna maisha baada ya wao kustaafu au kufariki  pia hawajiulizi kuwa wakiondoka  maofisini wakina nani wataiingia na watakuwa na uwezo ganiwa kufanya kazi walizozifanya kwa weledi mkubwa kwani walizipenda  au ndo kusema kuwa walishapiga vilivyo na ndo maana wengine ukienda maofisini kwao wanakuangalia kana kwamba shida yako ishafanyiwa kazi kumbe ndo kwanza umeingia kuongea naye kuhusu tatizo linalo hitaji msaada wake, au  ndo kusema wakiondoka maofisini wanawarithisha watoto wao waliowasomesha elimu ya kimagharibi, wakafundishwa kuiba na kufuzu katika fani hizo ili waje waibe  kwao na kufaidisha wazungu mali ambazo waasisi walisema zitunzwe ili watoto wa kitanzania waje wafaidi?
 Ebu jiulize maswali yafuatayo kisha ujijibu mwenyewe, siku ikitokea vyombo vya habari vyote vinapiga miziki na magazeti yote kuandika udaku itakuwaje? Na ukiwauliza wahusika wakakuambia wamekosa wataalam wenye ujuzi wa kuendesha vyombo vya habari na wanahabari wa kufanya habari za kiuchunguzi “investigative journalists” unajisikiaje? Na hapo ukamwona mwanao au mtu fulani aliyekuwa na ndoto za kuwa kama Salim Kikeke ameshindwa kusoma elimu ya juu kisa fani yake si kipaumbele  “non priority”?
Jiulize wakina Ibrahim Lipumba wa kesho ni wapi kama fani ya uchumi nayo ni “non priority” au nchi yetu haihitaji wachumi baada ya akina Prof. Lipumba siku zao zikiwa zimepita? Mimi sijui au ndo kusema watoto wa wakubwa waliosoma na kubobea katika masuala ya uchumi ndo watakuja wachukue nafasi zao? Kwani wao walisoma nje na kufundishwa kutuibia sie watanzania wanyonge ambao wengi wa wazazi wetu ni masikini na hawawezi kutusomesha fani tulizo zitamani kuzisoma na kuishi ndoto zetu?
Hizo ni baadhi ya fani tu ambazo ni muhimu sana kwa taifa letu lakini wahusika wameona hawahitaji watu wengine kwani waliopo wanatosha na watadumu milele. Inasikitisha na kuhuzunisha sana kuona watoto wengi wa masikini kusoma fani ambazo ukiwauliza kuwa wanazipenda wanatakujibu nilisoma hii fani ili nipewe mkopo.
Na ndio maana sishangai kabisa kuona walimu kufanya mapenzi na wanafunzi wao kwa ufinyu wa akili wakidhani wanaawakomoa huku wao wenyewe wakijiweka kwenye mazingira magumu ya kazi zao, lakini si kwamba walipenda kuwa walimu bali walisoma ualimu ili tu wapewe mkopo na wao waesabiwe kuwa ni miongoni mwa wasomi wenye shahada ya elimu ya juu.
Pia sishangai kuona idadi ya walimu wengi kuhitimu kila mwaka na kupangiwa mashule ya kwenda kufundisha lakini kadri wanavyozidi kuajiliwa ndivyo idadi ya wanafunzi wanaofeli inazidi kuongezeka kila mwaka ukilinganishwa na miaka ambayo kulikuwa na walimu wachache waliokuwa na wito kutoka mioyoni mwao kuwa waalimu.
Huo ni baadhi ya mfano ulio hai kabisa na kila mtu anajiuliza pasipo kupata majibu lakini kwa wahusika watakuambia tumesoma ualimu ili tupate mikopo na ajira kwa uharaka na uhakika wa ajira.  Ndivyo hali ilivyo kwani ni “priority”. Huwa inaumiza sana pale unapoona mwanafunzi, rafiki yako au mtu unayekaa naye chumba kimoja anaongea kuhusu masuala ya mikopo na pengine kukuuliza tunaenda kusaini lini “boom” huku wewe unaye ulizwa hauna, au anakuambia twende kuangalia majina ya “boom” yamebandikwa cafeteria au Darajani kwa wale wa chuo kikuu cha Dar es salaam huku wewe unayeambiwa hauna.
 Huwa ni simanzi kubwa na huzuni kubwa kwa wanafunzi ambao hawana mkopo kubaki kulia na mioyo yao na kubaki kuomba wenzao wenye mikopo wabakize chakula ili na wao wapate walau makombo tu wanayoyabakiza,  lakini muda mwingine ni vigumu kwa msomaji wangu kuamini niyaandikayo lakini ndivyo hali ilivyo na kama unabisha omba mwanao au kama wewe ni mwanafunzi wa sekondari ukose mkopo na wazazi wako wawe wale wenzangu na mimi utaamini niyaandikayo leo.
Nilisikitishwa sana siku moja nilipopigiwa simu na mdau mmoja wa habari kutoka kigoma na kuniaambia kuwa anapenda sana kuwa mwanahabari lakini alikosa mkopo kutoka elimu ya juu wa kumwezesha kusoma elimu ya juu na hivyo ikamlazimu kusitisha ndoto zake alizokuwa nazo awali na ndipo alikaa nyumbani na mwaka uliofuata akaamua kwenda kusoma ualimu kwa sababu tu ya uhakika wa kupata mkopo na uhakika wa ajira.
Chonde chonde kwa wahusika tukumbuke tuyafanyayo leo ndiyo matokeo ya kesho, na kama leo tunapuuzia mambo ya muhimu kwa kutoona vipaumbele vyake, tukumbuke taifa la kesho halina wataalamu wa kutosha katiak fani za habari, uchumi, mazingira, utalii, sanaa, wataalam wa lugha na wengineo wengi na hivyo tujue tunajenga taifa lenye waalimu wengi wanaofundisha kwa kutopenda hiyo fani na hivyo kujaza waalimu wanaofundisha waalimu ambao kwa kesho shule nazo zitakuwa haziwahitaji tena.
Na msije mkashangaa vyombo vya habari vikabaki kupiga mzuki na kukosa vipindi vya uelimishaji na kujenga taifa la watu wenye fikra chanya juu ya taifa lao, na magazeti mengi kugeuka ya kidaku kwa kukosa watu wenye kufikiria mbali juu ya kuibua matatizo yaliyopo ndani ya jamii zetu na kusababisha muhimili wa nne ya taifa kuvunjika kwa  sababu wataalam wengi waliokuwa na uwezo wa kufanya kazi hizo vipaji vyao vilizikwa vikiwa hai kwa kukosa mkopo na kukumbilia fani zenye “priority” au zenye vipaumbele wa kupata mkopo na uhakika wa ajira mapema.
Lakini mwisho nitaendelea kuwashukru sana wazazi na wadhamini walioamua kuwasomesha wanafunzi fani zilizo ndoto zao bila kujalisha wamepata au wamekosa mkopo, kwenu ujira wenu utalipwa na mwenyezi Mungu siku ile tutakapokuwa tunaulizwa uliitumiaje talanta na kipaji ulichopewa na mwenyezi Mungu. Hivyo ni muhimu kwa wanafunzi wanaofadhiliwa na wazazi au wafadhili wengine wana haja ya kujua kuwa wamejinyima ili wao wasome ili waweze kuziishi ndoto zao.
Na si kama wale waliofaidi nchi hii na kuifanya shamba la bibi ambalo kila mwenye dhamana alifanya alivyotaka na kuamua kuweka masharti magumu yanayowalazimisha watoto wa watanzania oye aye na wa  yule mkulima wa mihogo na mtama ambaye kwake mchicha pori na mboga za majani ambazo hazijui mafuta wala nyanya na kitunguu ndicho chakula chake cha kila wasiishi ndoto zao kwani hawana uwezo wa kuwasomesha watoto wao elimu ya chuo kikuu. Na kusahau kuwa muda utafika wa wao kutapika vile walivyovila kwa uroho wao na tamaa zao madaraka. Hongera sana Magufuli rais wa Tanzania na Kassim Majariwa mkumbukapo kuagiza pesa za kujenga barabara tukumbukeni nasi pia wanafunzi tunaosoma fani waziitazo ni “Non priority” tuliokosa mkopo mwaka wa masomo 2014/2015 maji yametufika shingoni hatujapewa mkopo wakuu, ndani yauongozi wenu tunaamini sauti zetu zitasikika na kilio chetu kitajibiwa muda si mrefuili nasi tuziishi ndoto zetu.

Makala haya yameandikwa na mwanafunzi wa mwaka wa pili anayesoma fani ya mawasiliano kwa umma, katika chuo kikuu cha Dar es salaam ambaye pia ni miongoni mwa wanafunzi ambao hawajawahi kupata mkopo kutoka bodi ya mikopo ya elimu ya juu kwa miaka yote miwili ya kuomba kwake. Anapatikana kwa mawasiliano ya 0763580901, 0716216249 au email ya barakangofira@gmail.com.
UBAGUZI KWENYE UTOAJI WA MIKOPO ELIMU YA JUU CHANZO CHA KUUA VIPAJI VYA VIJANA WA KITANZANIA UBAGUZI KWENYE UTOAJI WA MIKOPO ELIMU YA JUU CHANZO CHA KUUA VIPAJI VYA VIJANA WA KITANZANIA Reviewed by WANGOFIRA on 00:15:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.