BUNGE LA TANZANIA LAKATAA MAJINA YA WAGOMBEA WA CHADEMA NA CUF KUGOMBEA UBUNGE AFRIKA MASHARIKI


Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limekataa majina ya wagombea wa CHADEMA na CUF kwenda kugombea nafasi ya Ubunge wa Afrika Mashariki (EALA) baada ya kukutwa na mapungufu katika fomu zao.

Hatua hiyo imekuja baada ya wagombea hao kuonekana na mapungufu mbalimbali yaliyobainika kwenye nyaraka zao a uteuzi yakiwa yamekiuka masharti ya Ibara ya 50 ya Mkataba wa Kuanzishwa kwa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Ibara ya 67 ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Kifungu cha 4(4) cha Sheria ya Uchaguzi wa wajumbe wa Bunge la Afrika Mashariki ya Mwaka 2011 iliyotungwa na Bunge la Afrika Mashariki.

Aidha taarifa hiyo imesema CHADEMA uteuzi wao haukuzingatia jinsia, lakini pia hawajaambatanisha fomu za maombi ya wagombea, orodha ya waombaji pamoja na fomu ya matokeo ya kura.

Huku CUF wakiwa wametuma fomu za uteuzi wa wagombea zikiwa zimewasilishwa na mamlaka mbili tofauti, wagombea wawili hawana uthibitisho wa uraia wao, fomu za uthibitisho wa hiari ya kugombea haikuwepo kwa wagombea wote, orodha ya waombaji haipo kwa mgombea mmoja, fomu ya matokeo ya kura kwa wagombea haikuwepo pamoja na fomu ya mahudhurio kwa mgombea mmoja kutotimia.

Kutokana na mapungufu hayo msimamizi wa Uchaguzi Dr. Thomas D. Kashililah amesema ameshindwa kufanya uteuzi huo huku akiwataka kurekebisha mapungufu yaliyobainishwa kabla ya saa 7 mchana, Aprili 4 ofisini kwake mjini Dodoma.

Kwa upande mwingine amewashukuru wadau wote hususani vyama vyote vya siasa nchini kwa ushirikiano mzuri waliyompa katika zoezi zima la mchakato wa uteuzi wagombea pamoja na vyombo vya habari kwa ujumla.
BUNGE LA TANZANIA LAKATAA MAJINA YA WAGOMBEA WA CHADEMA NA CUF KUGOMBEA UBUNGE AFRIKA MASHARIKI BUNGE LA TANZANIA LAKATAA MAJINA YA WAGOMBEA WA CHADEMA NA CUF KUGOMBEA UBUNGE AFRIKA MASHARIKI Reviewed by WANGOFIRA on 20:32:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.