YAKITOKEA YA MOI NI SHULE GANI ITABAKI SALAMA?
Na,
BARAKA NGOFIRA
0763580901,
0716216249
Siku za
nyuma ilikuwa rahisi sana kusikia wanafunzi wa shule fulani wamechoma shule au
mabweni. Muda mwingine walipokuwa wakigoma tu kitu cha kwanza ambacho walikuwa
wakikifanya ni uchomaji wa ofisi muhimu za shule ikiwemo stoo ya chakula,
mabweni yao na hata ofisi za walimu.
Lakini
kwa muda sasa matukio hayo yamekwisha na sasa hayasikiki tena na migomo
mashuleni pia ni kama imekwisha kabisa. Katika matukio hayo yote ya migomo na
uchomaji na uharibifu wa miundombinu ya shule kwa kiasi kikubwa hayakusababisha
vifo vya wanafunzi au walimu katika shule hizo. Japo hayo yamepita na sasa hali
ni shwari katika shule hizo lakini kuna umuhimu mkubwa wa viongozi waliopo
kuhakikisha kuwa hali hizo hazijirudii tena.
Katika
siku za hivi karibuni shule Moi sekondari iliyopo nchini Kenya iliungua na
kusababisha vifo vya wanafunzi 9, ambao waliteketezwa vibaya kwa moto na
kushindwa kufahamika hadi kwa vipimo vya DNA. Lakini pia wengi wao wakiwa
wamejeruhiwa vibaya kwa kuuguzwa na moto. Tukio hili la ajabu na la kinyama
kabisa kwa taarifa za awali linaonyeshwa kuwa lilifanywa na watoto wadogo tu
tena mabinti wa takribani miaka 15 hivi. Ambao walichukua uamuzi huo baada ya
kunyimwa ruhusa ya kwenda nyumbani kwa sababu walizojijua wao.
Ndipo
wakachukua uamuzi huo wa kuteketeza shule na kusababisha madhira makubwa kiasi
hicho. Nitumie fursa hii kuwapa pole wakenya wote kwa tukio hili lakini kwa
namna ya pekee wazazi na ndugu na jamaa wa wanafunzi waliopoteza maisha katika
tukio hilo. Lakini pia wale waliojeruhiwa Mwenyezi Mungu awajaalie ahueni ili
waweze kupona haraka warejee katika masomo yao.
Kwa
tukio hili lazima walimu na wamiliki wa shule wajitafakari waone je miundombinu
ya shule zao ni rafiki kwa wanafunzi hasa majanga ya moto yakitokea. Maana kuna
baadhi ya shule hasa katika mabweni wanafunzi wanapolala wanalazimika kuzima
taa na kufunga Milango kwa kufuri kwa kuogopa wezi au wanafunzi kutoroka.
Jambo
ambalo kwangu naliona ni mtazamo hasi kabisa, kwani kila ninapofikiria vifo
vilivyotokea katika shule ya MOI roho yangu inajawa na ganzi, na kubaki na
kujiuliza hadi hao wanafunzi 9 wanateketea kwa moto kiasi cha kushindwa
kufahamika, wenzao walikuwa wapi kuwaokoa. Huku nikiyafikiria hayo najiuliza
tena kwa nini kuna kiasi kikubwa cha wanafunzi katika bweni hilo walijeruhiwa?.
Jibu la
haraka haraka linaloniijia akilini mwangu ni kuwa huenda bweni hilo lilikuwa
limefungwa na hata njia mbadala za kujiokoa kama vile madirisha ya wazi au vioo
ambayo ni rahisi kuvunjika na kuokoa maisha ya watu hayakuwepo. Badala yake
madirisha yalikuwa ni ya nondo tena zile nzito zilizosokotwa kwa maua ndizo
zilikuwepo katika bweni hilo.
Lakini
pia vitanda vyao kwa kiasi kikubwa vilikuwa vya mbao, ambapo baada ya
mwanafunzi huyo kuwasha moto kwenye kitanda chake ilikuwa rahisi kusambaa na
kusababisha vifo na majeraha hayo ambayo hayatasahaurika.
Tuje
kwenye shule zetu je mabweni yake yana miundombinu gani? Je madirisha yake ni
ya namna gani? na vitanda je? Lakini mbali na hayo je ni shule ngapi ambazo
katika mabweni ya wanafunzi wanalala huku mabweni yao yakiwa yamefungwa na
funguo kulala nazo walezi wa wanafunzi hao au kiongozi wa bweni kwa kuhofia
wezi na wanafunzi kutoroka?
Lakini ni
shule ngapi ambazo kwa kuogopa gharama za umeme kuna ratiba kabisa za kuwasha
na kuzima taa za mabwenini? Tukiisha jiuliza hayo yote tujitafakari je
yakitokea kama yaliyotokea shule ya sekondari Moi ni shule gani itapona?
Ukiachilia
mbali hayo pia kuna baadhi ya shule kwa tama za fedha hasa za binafsi na
mashirika ya dini hubeba wanafunzi kupita kiasi. Na kuwalazimu wanafunzi kulala
zaidi ya mmoja na wengine kulala madarasani au chini katika korido za mabweni
hayo. Hivi kweli tutapona au ndiyo tutasubiri uchunguzi usiokuwa na mwisho na
hatimaye inabaki historia?
Mbali na
serikali kutaka kila shule au taasisi kuwa kuwa na vifaa vya kuzimia moto
maarufu kama fire extinguisher lakini kuna shule hazina kabisa hata moja. Na
kama zipo basi zimetunzwa katika ofisi ya mkuu wa shule au ofisi za walimu au
katika maabara kama ipo. Na shule nyingine zipo tu kama mapambo maana hakuna
hata mwanafunzi hata mmoja anayejua namna ya kuitumia endapo janga la moto
likitokea.
Ni rai
yangu kwa serikali na wadau wote wa elimu ikiwemo wamiliki wa shule kuhakikisha
kuwa shule wanazozijenga zinakuwa na miundombinu rafiki ambayo majanga ya moto
yatokeapo uokoaji unakuwa rahisi. Na hata kama yakitokea madhara basi yawe
kidogo tu. Kwa mfano shule ya sekondari Lyamungo iliyopo wilaya ya Hai mkoani
Kilimanjaro mbali na majaribio uliokuwa ukifanywa na wanafunzi wa shule hiyo
lakini hawakufanikiwa hata siku moja zaidi ilikuwa wanachoma vitu vyao wenyewe
na hivyo hasara ilikuwa kwa wahusika na si shule.
Pia ni
lazima kwa shule zote nchini kuwa na ving’amuzi moto au fire alarm ili hata
ikitoka itirafu ya umeme ambao unaweza kusababisha moto vile ving’ora vya
tahadhari vitasaidia kuwaamsha hata wale walioko usingizini. Na kwa kufanya
hivyo itasaidia kuokoa maisha ya wanafunzi katika shule zetu.
Na
mwisho kuwepo kwa fire extinguisher kwa aina zake zote zilizowekwa maeneo ya
wazi ikiambatana na mafunzo kwa
wanafunzi na walimu ili litokeapo tatizo la moto iwe rahisi kuzimwa na si
kubaki kushaangaa tu na kurekodi kwa simu. Pia ni lazima serikali kupitia
wizara ya elimu na mafunzo ya ufundi kushirikiana na wakala wa usalama wa
majengo kukagua upya shule zote ili kuona mapungufu yaliyopo na ili wamiliki wa
shule wafanya marekebisho ya haraka.
YAKITOKEA YA MOI NI SHULE GANI ITABAKI SALAMA?
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:58:00
Rating:
No comments: