KAMPUNI YA TRUMARK YATOA ZAWADI YA EID EL-FITR KWA WATOTO YATIMA JIJINI DAR ES SALAAM
Keki maalumu ya hafla hiyo ikikatwa kwa pamoja. Kushoto ni Makamu Mkurugenzi wa Kituo hicho, Theobald Truphone na katikati ni Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Trumark, Agnes Mgongo. Wengine ni maofisa wa Kampuni ya Trumark.
Na Dotto Mwaibale
JAMII imetakiwa kujenga moyo wa kusaidia watu waliopo katika makundi yenye uhitaji ili nao wajisikie kama watu wengine waliopo katika familia.
Mwito huo umetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya Trumark inayojishughulisha na uwezeshaji jamii, Agnes Mgongo wakati kampuni hiyo ilipokuwa ikitoa zawadi ya Sikukuu ya Eid El-Fitr katika Kituo cha watoto Yatima cha Mtoto Wetu Tanzania kilichopo Kimara Suca jijini Dar es Salaam leo hii.
"Ni vizuri jamii ikajenga tabia ya kuwakumbuka watoto na watu wengine waliopo katika makundi maalumu kwa kuwafariji badala ya kuiachia serikali ambayo ina mambo mengi ya kufanya" alisema Mgongo.
Alisema kampuni yake iliguswa na changamoto walizonazo watoto waishio katika kituo hicho ikaona ni vizuri katika kipindi hiki cha sikukuu ya Eid El-Fitr wakajumuike nao kwa kula na kucheza pamoja na kuwapa zawadi mbalimbali.
Mgongo alitaja zawadi walizotoa kupitia wadau wengine marafiki wa taasisi hiyo kuwa ni nguo, vinywaji na chakula ambacho kilipikwa katika kituo hicho.
Akizungumzia changamoto wanazokumbana nazo watoto waliopo katika makundi yenye uhitaji, Wanswekula Zacharia alisema ni pamoja na vitabu, karo, sare za shule na mahitaji mengine.
Alisema pamoja na kuwepo kwa changamoto hizo mwanafunzi anapaswa kujua wajibu wake akiwa shuleni ni kusoma na si vinginevyo.
Alisema kupokea misaada ni jambo moja lakini hata mtu kufika tu kituoni hapo na kuwajulia hali bila ya kuwa na kitu chochote ni jambo la heri kwani wanachohitaji zaidi ni kujumuika na jamii na kupata faraja.
Mwanafunzi wa kidato cha sita, Shafii Hassan ambaye analelewa katika kituo hicho tangu akiwa mdogo anasema misaada wanayoipata imekuwa ikiwafanya wapate faraja ukizingatia ukubwa wa changamoto walizonazo.
Makamu Mkurugenzi wa Kituo hicho,Theobald Tryphone aliishukuru kampuni hiyo kwa msaada huo na kueleza changamoto kubwa walizonazo ni ada za wanafunzi, chakula, ulipaji wa umeme na kuwa Wakala wa Barabara Tanzania (Tanroad) wameweka alama za x katika majengo yao waondoke lakini suala hilo linashughulikiwa na Manispaa ya Ubungo kuona jinsi itakavyowasaidia kuwasaidia kupata eneo jingine kwa ajili ya
kujenga kituo hicho.
Mtoto analelewa katika kituo hicho, Godwin Steven alitoa shukurani kwa kampuni hiyo kwa niaba ya wenzake kwa msaada huo.
KAMPUNI YA TRUMARK YATOA ZAWADI YA EID EL-FITR KWA WATOTO YATIMA JIJINI DAR ES SALAAM
Reviewed by WANGOFIRA
on
21:50:00
Rating:
No comments: