Rais Dkt. Magufuli aahidi neema kwa wafanyakazi

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli, leo tarehe Mosi Mei, 2017 amesema Serikali ya  Awamu ya tano imepanga kufanya  nyongeza ya kawaida ya kila mwaka katika mishahara yaani Annual increment, ambayo ilikuwa imesimama kwa muda mrefu ikiwa ni pamoja na promosheni.

Rais Magufuli ametoa ahadi hiyo katika Sherehe za siku ya Wafanyakazi duniani zilizofanyika katika Uwanja wa Chuo cha Ushirika Moshi mkoani Kilimanjaro.

Amesema uamuzi wa Serikali wa kuanza kutoa promosheni unatokana na kukamilika kwa zoezi la uhakiki wa Wafanyakazi hewa  zaidi ya wafanyakzi kumi 19,000 walibainika kuwa wafanyakazi  hewa.

''Yale mambo yote yaliyokuwa pending ikiwa ni pamoja na promosheni kwa sababu tulishindwa,  unaweza kupromoti mfanyakazi hewa hayupo,kwa sababu tungetoa promosheni wakati kuna wafanyakazi 19,000 hewa,maanake tungepromoti na 19,000 na siajabu na watu waliowaandika mule ndio wangeletwa katika mapendkezo ya promosheni'' amesema Rais Magufuli.

Aidha, Rais Magufuli amewaonya watumishi ambao wamekuwa wakidanganya umri wa kustaafu ili waendelee kufanya kazi kwa muda mrefu na kuwa siku zao sasa zimekwisha.

Katika hatua nyingine Rais Magufuli amepiga marufuku uhamisho wa Wafanyakazi bila kuwalipa stahili zao kutokana na kuwepo na tabia ya kuwahamisha wafanyakazi bila kuzingatia taratibu hasa za malipo ya uhamisho.

''Sasa niwaombe wafanyakazi yeyote akihamishwa hakuna kuhama mpaka umelipwa pesa ya uhamisho,kuanzia juu mpaka chini,yeyote atakaye kuhamisha mwambie nipe hela yangu ya uhamisho ninapoenda akishindwa usihame kaa hapohapo ufanye kazi'' Amesema Rais Magufuli.

Amesema viongozi wengine wamekuwa wakiwahamisha wafanyakazi  kwa maslahi binafsi au visasi kutokana na maendeleo wanayowapata wafanyakzi

Rais Mgufuli amewahakikishia wafanyakazi kuwa Serikali ya awamu ya Tano itaendelea kuwajali na kuwa  karibu nao katika kutimiza dhana ya utatu ya ushirikiano kati ya Serikali, Wafanyakazi na Waajiri kwa lengo la kuleta maendeleo.

Aidha, Rais Magufuli amewaeleza wafanyakazi mipango mbalimbali anayofanywa na Serikali katika kuwaletea maendeleo ikiwa ni pamoja na ununuzi wa ndege mpya ,ujenzi wa Reli ya kisasa, utoaji elimu bila malipo na uboreshaji wa miundombinu katika kuwaletea maendeleo wananchi.

Sherehe za Mei Mosi zilizofanyika katika mkoa wa Kilimanjaro pia zimehudhuriwa na Makamu wa Rais Mhe. Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Mhe. Kassim Majaliwa, Spika wa Bunge Mhe. Job Ndugai, Mawaziri, Manaibu Mawaziri, Wabunge na viongozi mbalimbali wa Chama na Serikali ambapo kauli mbiu inasema,'' Uchumi wa Viwanda uzingatie kulinda Haki, Maslahi na Heshima ya Mfanyakazi''.

Jaffar Haniu
Naibu Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, IKULU
Moshi, Kilimanjaro
1 Mei, 2017

Rais Dkt. Magufuli aahidi neema kwa wafanyakazi Rais Dkt. Magufuli aahidi neema kwa wafanyakazi Reviewed by WANGOFIRA on 20:12:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.