WATANZANIA MILIONI 16 WANAFANYA SHUGHULI ZAO KWENYE MITANDAO YA INTANETI


Tafiti zinaonyesha kuwa karibu nusu ya wakazi wa dunia wanatumia mitandao, wakati nchini Watanzania milioni 16 wanafanya shughuli zao kwenye mitandao mbalimbali ya intaneti.

Mkurugenzi wa Idara ya Habari Maelezo, Dk Hassan Abbas, ameyasema hayo wakati anazindua tovuti mpya 37 za mikoa mitano na Halmashauri 37 nchini zitakazokuwa zikitumiwa na maofisa habari na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (Tehama) katika hafla iliyofanyika jijini hapa.

Amesema kutokana na hali hiyo, watu wengi kwa sasa wanatumia muda wao mwingi wakisoma nyaraka, matukio na vitu mbalimbali kuliko hata kusoma magazeti.

Amewataka maofisa habari hao kuzitumia tovuti hizo vizuri kwa madai kuwa ni nyenzo muhimu itakayowawezesha kutekeleza majukumu yao kwa wakati na zaidi kutoa taarifa sahihi za maendeleo kwa wananchi na kwa wakati.

"Tumieni tovuti hizi katika kutoa taarifa muhimu kwa ajili ya wananchi wetu na msisubiri wananchi waandamane kudai taarifa za bajeti na mapato na matumizi kwenye maeneo yao," amesema Dk Abbas.

Amewataka kutumia vyema mafunzo waliyopata katika kutekeleza wajibu wao kwa kuwatumikia wananchi kwa kufanya kazi kwa ubunifu, weledi na kwa wakati.

Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano kutoka Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Rebeka Kwandu, amesema kuzinduliwa kwa tovuti hizo zitatoa fursa kwa maofisa habari kuwa na uwajibikaji kwa kutoa taarifa sahihi kwa wananchi na kwa wakati.

"Kwa uzinduzi wa tovuti hizi matarajio yetu ni kuona manung’uniko mengi waliyo nayo wananchi yanapungua na wanapata taarifa sahihi za maendeleo na za serikali kwa wakati kwenye maeneo yao", amesema Kwandu.

Kwandu alisema Tamisemi itashirikiana kwa karibu na Idara ya Habari Maelezo kuhakikisha kuwa tovuti hizo zinafanya kazi muda wote tangu kuzinduliwa kwake.

Alisema Tamisemi kwa kushirikiana na Wakala wa Serikali Mtandao (eGA), Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora pamoja na Shirika la Maendeleo la Marekani (USAID) waliunda mfumo ambao utafanya kazi ya kuhuisha mfumo kwa kushirikisha taarifa ambazo zitajenga ufanisi, uwazi na uaminifu kwa umma.

"Kwa msaada wa Tamisemi, Utumishi, eGA na USAID, tovuti za mikoa mingine na halmashauri zilizobaki kwa Tanzania Bara zitazinduliwa Machi mwaka huu, zikiwa chini ya muonekano mpya wa tovuti za serikali na kuhakikisha halmashauri zina mifumo bora ya kushirikisha wananchi na kuboresha utendaji kazi", alisema Kwandu.

Amesema utoaji wa mafunzo hayo ya tovuti yamefadhiliwa na Mradi wa Uimarishaji wa Mifumo ya Sekta za Umma (PS3) ambao ni wa miaka mitano ulioundwa kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania.

Mkuu wa Mifumo ya Mawasiliano wa PS3, Desdery Wengaa, amesema PS3 inafanya kazi katika sekta mbalimbali ili kuimarisha mifumo ya mawasiliano, utawala bora, fedha na rasilimali watu katika ngazi ya kitaifa na Serikali za Mitaa.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Magu, Said Fundikira aliishukuru PS3 kwa kutoa mafunzo hayo ya wiki moja kwa maofisa habari ambayo alisema yatawawezesha kutoa taarifa sahihi kwa umma na kwa wakati.

IMEANDIKWA NA NASHON KENNEDY-habarileo MWANZA
WATANZANIA MILIONI 16 WANAFANYA SHUGHULI ZAO KWENYE MITANDAO YA INTANETI WATANZANIA MILIONI 16 WANAFANYA SHUGHULI ZAO KWENYE MITANDAO YA INTANETI Reviewed by WANGOFIRA on 05:18:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.