PROF. NDALICHAKO ONDOA PAMBA MASIKIONI UWASIKIE WANAO WANAVYOTESEKA KWA KUKOSA MIKOPO ELIMU YA JUU

Related image

Tatizo la mikopo kwa wanafunzi wa elimu juu limekuwa likipigiwa kelele kila siku na wadau mbalimbali wa elimu, huku wanafunzi wa vyuo vikuu wakiwa wahanga wakubwa wa mikopo. Hata wale wanaonufaika na mkop huo ambao hutolewa na bodi ya mikopo ya elimu ya juu HESLB. Kwa uzoefu wangu mdogo wa kwenda kuangalia ofisi za bodi ya mikopo zilizopo Mwenge jijini Dar es salaam hakuna siku hata moja ambayo nimekuta sikukuta wanafunzi kutoka vyuo mbalimbali wakifuatilia mikopo yao.

Wengi wao ni watoto wa maskini na wakulima ambao wametoka mikoani na kuchaguliwa vyuo vilivyo Dar es salaam na maeneo ya jirani. Lakini pia wapo wale ambao huingia gharama za kuja Dar es salaam kufuatilia mikopo lakini kwa masikitiko huambulia kupoteza nauli na muda wao bure na kuamua kusitisha masomo ambayo ndiyo njia pekee ya kuishi ndoto zao.
Tangu serikali itoe majina ya wanufaika wa mkopo wa elimu ya juu ambayo mpaka sasa ni zaidi ya wanafunzi elfu ishrini na moja wa mwaka wa kwanza ambao wamepewa mkopo kati ya waombaji zaidi 58000 walikuwa wameomba mkopo. Huku lengo la serikali kwa mwaka huu likuwa kuwapa mkopo wanafunzi 25,500 tu kwa mwaka huu wa fedha. Kwa idadi hiyo ni sawa na asilimia kama 38 hivi za waombaji wote wa mwaka huu wa masomo 2016/17.

Nimekuwa nikipokea simu na jumbe nyingi kwenye simu yangu za wanafunzi, wazazi pamoja na walezi wa wanafunzi mbalimbali wakilia mizigo mizito na msongo wa mawazo walionao kwa kukosa mkopo wa elimu ya juu huku sifa zote wakiwa nazo. Lakini mkopo wamenyima hivyo kuwalazimu watoto wao kusiotisha masomo na kurudi nyumbani kulima na kuchunga ng’ombe maana ndizo kazi pekee ambazo zimewakuza na kuwasomesha.

Kwa taarifa zisizo rasmi zaidi ya wanafunzi 10,000 wa mwaka wa kwanza kwa mwaka huu pekee bado hawajaripoti kwenye vyuo walivyopangiwa. Idadi hii ni kubwa sana kwa taifa na ni aibu kwa taifa ambalo serikali inajigamba kuwa ni tajiri kwa kuwa na maliasili nyingi, madini ya kila aina, gesi na mbuga na hifadhi nyingi za wanyama wa kila aina. Lakini cha ajabu  imeshindwa kutoa elimu bure au kuchangia pesa ya kujikimu kwa kila mwanafunzi wa elimu ya juu.

Kwa muda sasa nimekuwa nikitiwa kichefuchefu na kauli za viongozi wa serikali hasa walionufaika kusomeshwa na serikali. Bila hata ya aibu husubutu kusema hadharani hata bila ya aibukuwa enzi wao wanasoma serikali ilikuwa ikiwahudumia kila kitu, kazii yao ilikuwa ni kusoma tu.

Na cha kushangaza hadi magari walikuwa wakipanda bure, kalamu, sabuni, chakula, malazi, posho, yaaani kila kitu kwao kilikuwa ni bure. Lakini leo baada ya kupata elimu wamesahau yote ambayo serikali iliwatendea badala yake wameondoa kila kitu na kuweka elimu ya kujitegemea ili wao na wanao waendelee kufaidi matunda ya nchi hii.

Inasikitisha sana pamoja na vilio vyote vya wanafunzi maskini na hoe hae ambao kwa sasa hawana mbele wala nyuma lakini kwa sasa wako vyuo vikuu wamebaki njia panda. Na hivyo kuamua kufanya ofisi za bodi ya mikopo kuwa shule yao ambapo kila kukicha wao huenda na kurudi lakini bado serikali imeziba masikio. Haisikii haioni na wala hata haijali maana watoto wao wanasoma vyuo vikuu vya nje na kama wapo vyuo vikuu vya ndani mkopo wamepewa kwa asilimia mia moja maana wao ni watoto wa mabosi.

Agness Leonard mwanafunzi aliyechaguliwa kujiunga na shahada ya kwanza ya ualimu Chuo Kikuu cha Dar es salaam na kupewa namba ya usajili ya 2016-04-00782. Ni miongoni mwa maelfu ya  wanafunzi waliokosa mkopo kwa mwaka huu huku akiwa anatokea familia maskini. Ambao wanandoto ya kupata elimu ya chuo kikuu lakini kwa sababu ya kukosa mkopo huku wakiwa na ufaulu mzuri ameamua kusitisha masomo yake huku hata nauli ya kurudi nyumbani kwao Tabora hakiwa hana.

Amesoma kwa shida sana na kwa bidii huku akiamini kuwa akifaulu na kujiunga na elimu ya chuo kikuu walau uchungu wa maisha utapungua. Lakini zilikuwa ni ndoto za mchana kwake ambazo kwa sasa hana tena matumaini na kubaki kufutwa machozi na rafiki zake.

Maisha ya kushindia mkate wa shilingi mia tano kila siku yamemshinda maana kwa sasa hata hiyo 500 ya kununulia mkate hana. Haya ndiyo maisha ya watoto wengi wa maskini na makabwela wanaosoma vyuo vikuu.

Inatia hasira sana kuona serikali inaweka vipaumbele vya mikopo kwa wanafunzi wa masomo ya sayansi na mengine yakiachwa bila kipaumbele huku wanaosoma masomo ya biashara na sanaa wakiachwa. Na cha kushangaza zaidi wanaosoma masomo ya sayansi wenyewe mara baada ya kumaliza vyuo hawathaminiwi na serikali yao.

Ndiyo ni jambo zuri kuwekeza kwenye masomo ya sayansi lakini mbona hata wanasayansi waliosomeshwa na serikali tena kwa gharama kubwa faida yao haionekani. Nasema haionekani kwa sababu hatuna unachokitengeneza cha kwetu, viberiti, chumvi, kalamu, pamba za kutolea uchafu maskioni na hata njiti za kutolea mabaki ya chakula tunaagiza nje?

Japo sera na mikakati ipo ya kuboresha viwanda vya ndani ili nasi tuwe na vya kujivunia, ni bora serikali ikaweka mipango mikakati ya mikopo kwa wanafunzi wote wa elimu ya juu pasipo kuwa na ubaguzi.

Rais Magufuli alisisitiza kuwa mikopo ya elimu ya juu itakuwa kipaumbele ikiwa atachaguliwa. Lakini leo imekuwa danganya toto kwa wanafunzi wa vyuo vikuu na kuongeza uchungu zaidi kwao kwa kuwacheleweshea mkopo ambapo hadi waandamane na kupiga kelele kwenye vyombo vya habari ndipo wapewe.

Cha kushangaza zaidi ni baadhi ya watu ambao hata hawakuwahi kusoma au kunufaika na fedha za mkopo wa elimu ya juu majina yao kuonekana kwenye orodha ya wadaiwa sugu. Jambo ambalo linatia shaka kwa utendaji na usahihi wa taarifa na utunzwaji wa kumbukumbuku za wanafuika wa mikopo kwa elimu ya juu.

Chonde chonde waziri wa elimu wasaidie watoto wa maskini wapate mkopo wasome elimu ya juu kama wewe na wenzako mlivyonufaika na elimu ya bure mliyopewa na serikali kwa kipindi chenu. Ni haki yao kupata mkopo maana ni kodi za wazazi wao na babu zao waliowawekea ninyi mazingira mazuri ya kusoma na kushikia nyazifa mlizonazo.

Lakini kama mmeamua kuendelea kuweka pamba maskioni ili watoto wenu waendelee kusoma ili waje kuongoza taifa ili haina shida lakini tambueni kuwa ipo siku Mungu atajibu maombi yao. Maana machozi yao hayapotei bure.


Makala hii imeandikwa na mwanafunzi wa mwaka wa tatu wa shahada ya kwanza ya mawasiliano kwa Umma katika Chuo Kikuu cha Dar es salaam. Anapatikana kwa mawasiliano ya barua pepe ya barakangofira@gmail.com au 0763580901.
PROF. NDALICHAKO ONDOA PAMBA MASIKIONI UWASIKIE WANAO WANAVYOTESEKA KWA KUKOSA MIKOPO ELIMU YA JUU PROF. NDALICHAKO ONDOA PAMBA MASIKIONI UWASIKIE WANAO WANAVYOTESEKA KWA KUKOSA MIKOPO ELIMU YA JUU Reviewed by WANGOFIRA on 01:29:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.