Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Azindua Ripoti Ya Hali Ya Hewa Barani Africa

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewataka viongozi wa Afrika wajiulize wanaweza kuchangia kitu gani katika kuboresha maisha ya mamilioni ya wakazi wa bara hilo.

Ametoa kauli hiyo Alhamisi, Agosti 31, 2016 usiku  wakati akizungumza na wawakilishi wa taasisi za kimataifa waliohudhuria uzinduzi wa taarifa ya Taasisi ya Kuboresha Mazingira ya Uwekezaji barani Afrika (ICF) uliofanyika kwenye hoteli ya Serena jijini Dar es Salaam.

Waziri Mkuu ambaye alikuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo alisema taasisi hiyo imesaidia kukuza uwekezaji kupitia miradi katika nchi mbalimbali za Afrika kwa kuimarisha mifumo ya ukusanyaji kodi, usajili wa biashara za wajasiriamali na upatikanaji wa leseni za biashara.

“Kutokana na kazi inayofanywa na taasisi hii, hali ya uwekezaji katika nchi nyingi imeimarika na bara la Afrika limekuwa mbia kwa wawekezaji kutokana na ushirikiano baina ya Serikali za nchi husika na sekta binafsi. Uchumi wa nyingi za Afrika umeimarika kuliko hapo awali,” alisema.

Akitoa mfano, Waziri Mkuu alisema zaidi ya wajasiriamali 500 kutoka Tanzania walipatiwa mafunzo kwa ushirikiano baina ya ICF, Serikali na ESAURP ili kuwajengea uwezo waweze kufanya biashara zao kwa tija zaidi. “Mafunzo hayo yaliwalenga wajasiriamali wadogo na wa kati ambao wanajihusisha na uvuvi, biashara za rejereja na jumla kutoka mikoa ya Mwanza na Dar es Salaam”.

“Kupitia mafunzo hayo, wajasiriamali hao waliweza kusajili biashara, kurasimisha biashara zao, kuongeza mitaji na kujua namna ya kutunza taarifa za biashara zao,” alisema.

Mapema, Mwenyekiti Mwenza wa taasisi hiyo ambaye pia ni Rais Mstaafu wa awamu ya tatu, Mhe. Benjamin Mkapa alisema kuna haja ya wananchi kubadili mitazamo yao juu ya sekta binafsi kwani nayo ni muhimu katika ujenzi wa uchumi kwa nchi yoyote ile.

“Watu wengi wanahisi kwamba wawekezaji ni wabaya. Hii si kweli. Tunapaswa kujenga mazingira ya kuwakubali kwa sababu wanakuja na mitaji yao na wao wanawakilisha michango kutoka kwa mamilioni ya wafanyakazi kutoka kwenye nchi zao. Hatupaswi kuwaona kwamba ni maadui,” alisema.

Alitumia fursa hiyo kumshukuru Rais Mstaafu wa Serikali ya awamu ya nne, Mhe. Jakaya Kikwete kwa uamuzi wake wa kukubali kuiruhusu taasisi hiyo ya ICF iweke makao yake makuu hapa nchini wakati ilikuwa imeshakataliwa kufanya hivyo katika nchi nyingi ambako ilipeleka maombi yake.

Aliwataka viongozi mbalimbali watumie uzoefu uliowekezwa na taasisi hiyo kwenye uboreshaji wa mifumo ya mahakama na ukusanyaji kodi, utoaji wa leseni, urasmishaji wa biashara za wajasiriamali wadogo.

“Tunayo maeneo mengi ambayo tumefanya vizuri iwe ni katika TEHAMA, miundombinu, mahakama au mambo ya forodha. Uamuzi ni wenu juu ya jambo lipi muanze nalo katika kuboresha huduma ili kuharakisha maendeleo ya bara hili,” alisema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,

ALHAMISI, SEPTEMBA MOSI, 2016


Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Azindua Ripoti Ya Hali Ya Hewa Barani Africa Waziri Mkuu Kassim Majaliwa Azindua Ripoti Ya Hali Ya Hewa Barani Africa Reviewed by WANGOFIRA on 21:20:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.