Waziri Mkuu Kassim Majaliwa awataka watanzania kudumisha amani


WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amewaomba viongozi wa dini zote kutumia nyumba za ibada kuwahamasisha waumini wao umuhimu wa kulinda na kudumisha amani na utulivu uliopo nchini.

Amesema Serikali itahakikisha amani na utulivu vinaendelea kudumishwa nchini ili Watanzania wawe na uhakika wa kuendelea kufanya kazi zao za kuwaingizia kipato na kuwaletea tija.

Waziri Mkuu ametoa wito huo jana (Jumatatu, Septemba 12, 2016) wakati akizungumza na waumini wa dini ya kiislam mara baada ya kumaliza kuswali sala ya Eid El Haji kwenye viwanja vya Mwembe Yanga, Temeke Dar es Salaam.

“Serikali itaendelea kuimarisha ulinzi katika maeneo yote nchini. Wito wangu kwa viongozi wa dini msisitize waumini juu ya utunzaji wa amani pamoja na kukemea vitendo viovu ili Taifa lizidi kusonga mbele,” amesema.

Wakati huo huo Waziri Mkuu amewasisitiza wananchi kuendelea kuwaombea mahujaji waliopo mjini Makka na Madina nchini Saudi Arabia wakiendelea na ibada ya hijja warudi salama.

Pia Waziri Mkuu ametumia fursa hiyo kuwaomba wananchi kuwasaidia kwa hali na mali watu waliokumbwa na tetemeko la ardhi mkoani Kagera ambako jumla ya watu 16 walifariki na wengine 253 kujeruhiwa.

Pia maelfu ya wananchi kukosa makazi baada ya nyumba 840 kuanguka na nyingine 1264 zikipata nyufa yakiwemo majengo 44 ya taasisi mbalimbali za umma

Awali akisoma hutuba ya Eid viwanjani hapo Sheikh Nurdin Kishki alisema dini ya Uislamu ni dini ya amani hivyo amewaomba waislamu kujiepusha na vitendo vya uvunjifu wa amani yakiwemo mauaji ya watu wasiokuwa na hatia.

Sheikh Kishki amesema ni muhimu watu kulinda amani kwani ikitoweka ni vigumu kuirudisha, alitolea mfano wanachi wa nchi za Libya na Misri ambazo hadi sasa zimeshindwa kuirudisha.

Amesema mtu yeyote anayejihusisha na vitendo vya uwamwagaji wa damu, kudhulumu mali za watu pamoja na kuwavunjia heshima wenzake atakuwa ameangamia, hivyo amewataka Watanzania hususan wakazi wa Temeke kujiepusha navyo.

“Temeke sasa inaongoza kwa matukio ya mauaji, wanaua hadi walinzi. Askari wameuawa bila hatia, jambo hili linasikitisha sana. Watu waliokuwa wanafanya kazi ya kulinda raia na mali zao wanauawa bila ya hatia! Ameongea kwa masikitiko na kuwaomba Watanzania wajiepuszhe na vitendo hivyo.

Katika hatua nyingine Sheikh Kishki ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuonyesha dhamira ya dhati ya kuwatumikia wananchi na kuwaletea maendeleo hivyo amewaomba wananchi wawe mstari wa mbele kutoa ushirikiano ili taifa liweze kusomba mbele.

“Ndugu zangu tumepewa heshima kubwa leo kuswali Eid na Mheshimiwa Waziri Mkuu tena amekuja hapa kwenye viwanja hivi vya Mwembe Yanga, hii inaonyesha ukaribu wa viongozi wetu wakuu kwa wananchi wao hususan wa hali ya chini,” amesema.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa awataka watanzania kudumisha amani Waziri Mkuu Kassim Majaliwa awataka watanzania kudumisha amani Reviewed by WANGOFIRA on 20:52:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.