RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 36 & 37
MTUNZI:ENEA FAIDY
...Mama
Eddy alitazama juu ili kuona kama kuna chochote lakini hakuona kitu.
Ilimbidi atumie nguvu zake za uchawi alizokuwa Nazo ili kujilinda kwani
aliziona dalili za kuvamiwa katika mazingira ya kutatanisha.
Mama
Eddy ambaye jina lake halisi alijulikana kama Maimuna hakuwa Mtu wa
kawaida Bali alitumwa na uongozi mkuu wa himaya aliyotokea Doreen ili
kumsaidia kupata vitu alivyovihitaji.
Alitumia
mbinu ya kujifanya mke wa Mr Aloyce ili kuweza kumteka vizuri na
kumfanya asihangaike sana kuhusu mwanae kwani kulikuwa na uwezekano
mkubwa sana wa kuharibu kazi. Maimuna alikuwa ni kijakazi mkongwe wa Bi
Tatile na alikuwa akiaminika sana katika himaya ya Wanatatile kwani ni
mtu pekee aliyewahi kufanikisha ajali kubwa ya mabasi mawili iliyoua
abiria wote kisha wakafanywa kitoweo katika sikukuu ya kumpongeza Bi
Tatile kama kiongozi bora wa wachawi wote Afrika Mashariki. Bi Maimuna
alikuwa akiaminika sana kwa kila kazi anayoagizwa kwani hakuwahi kufanya
makosa zaidi ya tukio moja tu la kuanguka kanisani akiwa katika
harakati za kuwanga mchana.
"Maimuna!
Maimuna! Hapa sio kwako na Leo ndio mwisho wa ubaya wako kwenye familia
hii" ilisikika sauti nyororo isiyo na mkwaruzo hata kidogo huku
ikijirudia rudia. Maimuna alibaki na mshangao wa ajabu sana, akataharuki
huku akihema kwa nguvu. Akaaangaza macho kila upande pasipo kumuona mtu
yeyote.
Akazidi
kuchanganyikiwa sana. Ghafla wazo likamjia akilini mwake, bila
kuchelewa akaamua kulifanyia kazi. Akanyoosha mkono wake wake wa kulia
kisha nguvu nyingi zikamjia kama radi mkononi mwake. Bi Maimuna akaachia
tabasamu mwanana akiamini hakuna kitakachomdhuru kwa wakati ule wala
wakati mwingine wowote. akatulia kimya akimsubiri adui yake, lakini
hakuona chochote zaidi ya ukimya mzito uliokuwa umetawala.
"Kumbe unaniogopa eeeh!" Alisema Maimuna.
"Ha
ha ha! Sikuogopi Maimuna... Nakuvutia pumzi tu maana sina papara" sauti
ile iliyojaa dharau ilisikika. Bi Maimuna hakutushika hata kidogo
kwani alikuwa anajiamini kupita kiasi. Ghafla sura yake ikabadilika
sana na kuwa sura ya kutisha sana.
Meno
yakawa marefu kama mnyama mkali, kucha zikawa ndefu na Kali kama za
chui anayemvamia swala, macho yake yakawa meusi huku mboni yake ikiwa
nyekundu kama moto. Lengo lake lilikuwa ni kuonesha nguvu zake mbele ya
adui yake ambaye hakujua ni nani. Ghafla kicheko kikali cha kutisha
kilichojaa dhauri na jeuri kikasikika na kumfanya Maimuna ajione mdogo
kama simimizi ilihali hamjui nana aliyemcheka.
Wakati huo huo Mlango ulifunguliwa na Mr Aloyce aliingia sebuleni pale.
"Mamaaaa"
Mr Aloyce alipiga ukunga wa nguvu baada ya kumkuta mkewe akiwa na
umbile la kutisha sana. Uvumilivu ulimshinda alijikuta anakimbia nje
kama chizi huku akihema kwa nguvu. Mlinzi alimshangaa Mr Aloyce bila
kuelewa kinachoendelea.
"Vipi
bosi?" Aliuliza mlinzi huku akicheka sana. Mr Aloyce alianguka chini
kama mzigo huku akihema kama Mtu aliyepanda mlima mrefu kwa kasi. Mlinzi
alimsogelea na kumuuliza kilichojiri.
"Kuna maajabu humo ndani"
"Maajabu gani?"
"Mke.. Mke wangu...Ame..."
"Amefanyaje
tena?" Aliuliza mlinzi kwa woga kwani alishapewa onto Kali na mwanamke
yule kuwa asimfatilie kwa lolote. Lakini kabla hajasema chochote kuna
kitu kiliwashtua Mr Aloyce na mlinzi wakabaki wameduwaa kwa mshangao.
******
Mama
Pamela hakuwa na la kufanya zaidi ya kulia tu. Muda wote ule hakujua
Doreen anaendeleaje ila kilichomshangaza ni kwanini Doreen hakwenda
sebuleni kujumuika nao? Alinyanyuka kitini na kwenda chumbani kwake.
Lakini ghafla mshangao wa ghafla ulimvaa mwanamama yule baada ya kukuta
hali ya chumba ni mbaya sana kila kitu kilikuwa shaghalabaghala tu,
ndipo machale yakamcheza, akasogelea droo anayohifadhia pesa.
"Mungu
wangu!" Alishtuka mama Pamela baada yakukuta droo IPO wazi lakini haina
pesa yoyote zaidi ya stakabadhi ambazo hakuwa na shida nazo wakati ule.
Macho yalimtoka kwa mshangao huku akitoatoa vitu ndani ya droo ile bila
kuona chochote. Akasimama wima akiwa ameshika mkono kiunoni kwa hasira
"Doreen!"
Aliita kwa jazba bila kujua Doreen alikwishaondoka muda mrefu uliopita.
Mama Pamela akakugua tena ili kujiridisha kama kweli pesa hazikuwamo
lakini bado hakukuta pesa ndani ya droo ile wala eneo lingine chumbani
mle.
Mama
Pamela alichanganyikiwa sana akatoka ndani ya chumba kile na kupiga
hatua za harakaharaka koridoni kuelekea chumbani kwa Doreen.
Alifika
mlangoni na kufungua mlango kwa jazba kubwa. Lakini cha ajabu chumba
kilikuwa kitupu na hakukuwa na mtu yeyote wala dalili za uwepo wa mtu.
Mama Pamela akahamaki, akamwita Doreen kwa sauti kali lakini hakuitikia.
"Mungu
wangu ina maana Doreen ametoroka na pesa au?" Alijiuliza Mama Pamela
akiwa ameishiwa nguvu kabisa. Hakutaka kuamini kama binti anayemuamini
kiasi kile angetenda tukio lililotokea.
Mama
Pamela alitoka nje ya nyumba yake ili kumtazama vizuri Doreen.
Alimtafuta pale uani na kila upande wa nyumba lakini Doreen hakuwepo.
Moyo wa mama Pamela ukatawaliwa na lawama nyingi sana. Akajilaumu ni
kwanini hakumsikiliza mumewe mpaka yote hayo yametokea.
Akakaa
chini kibarazani huku machozi yakimchuruzika. Kila akikumbuka maneno ya
mwanae roho ilimuuma zaidi, hakuwa na hamu hata ya kula. Alikuwa na
simanzi nzito iliyopelekea mafuriko ya machozi usoni mwake. Alilia mpaka
machozi yakamkauka akiwa pale pale kibarazani kwake. Hakutaka hata
kumwona binti yake kwani uchungu ungemzidia. Kwa jinsi alivyokuwa
akimpenda na kumjali Pamela hakuamini kirahisi kuwa Leo amekuwa adui
yake mkubwa na kumpa lawama za uchawi.
"Mungu tu Anajua" aliwaza Mama Pamela.
Majira
ya saa kumi na moja jioni, Baba Pamela aliwasili jijini Mbeya na kufika
nyumbani kwake akiwa na mawazo tele juu ya familia yake. Alipofika
ndani tu alikutana na mkewe ambaye uso wake ulivimba sana kwa machozi ya
siku nzima. Baba Pamela hakushangaa sana kwani alihisi mkewe anamlilia
binti yao Pamela kumbe si hivyo tu, Bali alikuwa na jambo zito
lililomtatiza sana moyoni mwake.
****
Familia
ya akina Dorice ikiwa bado imekaa kikao babu yake Dorice aliyefahamika
kama Mganga Tawi La Mtawile alikuwa tayari ametoa wazo kuwa atafanya
jambo.
Familia
nzima ikaondoka kwenye nyumba ya mama Dorice na kwenda moja kwa moja
kwa Mganga Tawi la Mtawile ili kujua Dorice yupo wapi na katika hali
gani.
Na kwakuwa hapakuwa mbali sana, walitumia mwendo wa dakika tano tu mpaka kufika kwenye nyumba ta Tawi La Mtawile.
Mganga
yule maarufu mkoani singida, alikuwa ametenga eneo maalum nyumbani
kwake kwaajili ya shughuli za uganga. Alipanga vyema vibuyu na dawa zake
pembeni alizungushia kaniki nyeusi na nyekundu. Akavua viatu, kisha
akawaamrisha wote waliombatana nae wavue viatu ndipo wakae kwenye zulia
alilotandika chini. Wote wakafata kama walivyoamriwa.
Mganga
Tawi alianza kuimba nyimbo za kuita mizimu na kuongea maneno ambayo
wengine hawakuyaelewa . alitumia dakika kumi nzima kisha akachukua kioo
kikubwa, akanyunyiza dawa na kuipakaza vizuri kwa kutumia mkia kama wa
ng'ombe. Akaita jina la Dorice Mara tatu. Baada ya muda mfupi ardhi
ikatetemeka sana radi zikapiga mfulululizo na kuwafanya wote waogope. Na
kila mmoja alitamani kukimbia kwani palikuwa na utisho wa ajabu....
Riwaya:Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) -:Sehemu ya 37
....ukimya
mzito ulitawala huku ndugu zake Dorice wakijiuliza ni mini kitatokea.
Ghafla moshi mweusi ulioambatana na radi ukatokea mbele yao karibu na
mti mdogo uliokuwa karibu na kile kijumba cha uganga cha Tawi La
Mtawile. Wote wakakaza macho kwa woga huku wakitazama kwa makini moshi
ule ulitokana na nini ilhali hakuna moto wowote katika eneo lile.
Kwa
namna ya ajabu na ya kustaabisha sana ambayo hakuna aliyeitarajia.
Doreen alitokea mbele yao akiwa na muonekano tofauti na waliomzoea.
Alikuwa ni mrembo kupita kiasi huku marashi makali yenye harufu nzuri
yakizidi kuziumiza pua zao kwa fujo, mikufu ya dhahabu ilining'nia
shingoni mwake ikienda sambamba na hereni ilizokuwa amezivaa pamoja na
Pete kwenye vidole vyake. Kila mmoja alionesha mshangao wa ajabu kwani
hawakuelewa ni kwanini Dorice yupo vile. Walitulia kimya huku woga
ukiwazidia kwani walijua ni mzimu wa Dorice.
"Dorice
umekuwa jini?" Aliuliza Tawi la Mtawile kwa sauti Kali. Dorice
akajiweka sawa na kuachia tabasamu mwanana huku akipiga hatua chache
kuwasogelea ndugu zake ingawa hakuwa nao karibu sana.
"Kwanza
kabisa nimefurahi kuwaona ndugu zangu... Mama nilionana nae tangu akiwa
kwenye basi.." Alisema Dorice kwa sauti tulivu sana. Maneno yake
yalimshtua sana Mama Dorice na kumfanya akumbuke matukio yote
yaliyomtokea alipokuwa kwenye basi na kabla ya kuingia kwenye basi.
"Ni wewe?? Kwanini umekuwa jini?" Alisema Mama Dorice kwa sauti iliyojaa woga sana.
"Mimi sio jini ila ninataka kulipa kisasi na kuwakomboa watu wasio na hatia.." Alisema Dorice.
Baada
ya Dorice kusema vile Wote wakatazamana kwa mshangao sana, mama Dorice
alitaman mwanae Arudi katika hali ya kawaida ili aendelee kuishi nae
lakini Dorice asingekubali hata kidogo kupoteza malengo yake
aliyopangilia kuyafanya kwa wakati ule.
"Mama
ninakupenda sana! Nina imani nitarudi nyimbani baada ya kumaliza kazi
yangu... Asanteni kwa kuniita... Kwaherini!" Aliema Dorice kwa huzuni
kubwa huku neno kwaheri likijirudia Mara kadhaa mpaka Alipopotea na
kutoonekana tena machoni mwao. Huzuni ikamtanda mama Dorice akamtazama
Mganga Tawi la Mtawile na kwa bahati wakagongana macho kwa mganga pia
alikuwa akimtazama mama Dorice.
"Baba Naomba mwanangu arudi.." Alisema Mama Dorice huku chozi likimlengalenga machoni.
"Mmh!
Hilo haliwezekani mwanangu... Dorice hakuwa duniani Bali aliolewa na
jini na amepewa nguvu za kijini ambazo ni tishio sana... Ni kubwa kuliko
kawaida na nadhani kuna jambo muhimu amekuja kulifanya maana lasivyo
asingerudishwa duniani... Tawii..Tawi La Mtawileeee..!"
Alisema mganga yule kwa sauti Kali ya kiganga.
"Inamaana atakuwa jini?"
"Inawezekana akawa MTU wa ujinini siku zote"
"Eeh Mungu wangu" alisema Mama Dorice.
Mganga
hakuwa na la kufanya juu ya Dorice. Wanaukoo wote walistaajabu lakini
hawakuwa na la kufanya zaidi ya kupigwa na butwaa. Mama Dorice alikuwa
haamini kilichomtokea mwanawe lakini hakuwa na jinsi na maneno ya mganga
yalizidi kumpa mawazo mengi.
Haukupita muda sana wote walitawanyika na kwenda majumbani mwao huku suala la Dorice likiwa gumzo akilini mwao.
****
"Mama Pamela unakumbuka nilikuambia nini kuhusu mgeni wako?" Aliuliza Baba Pamela.
"Nakumbuka
mume wangu" alijibu mama Pamela huku akilia. Na alijua fika kwa jinsi
Baba Pamela alivyompenda mwanae basi lazima atafanya kitu kulingana na
tuhuma zile alizoshtakiwa na mwanae.
"Umeona maisha mlioishi tangu amekuja?"
"Ndio.. "
"Vizuri...hebu muite hapa.."
"Hayupo...
Nimemtafuta sijamwona..." Alisema Mama Pamela huku aibu na hofu
vikizidi kumvamia kwa kasi sana kwani usemi usemao Asiye Sikia La Mkuu
huvunjika guu ulitimia kwake kwa wakati ule ingawa hakuwa na imani kama
Aliyemtoa titi binti yake alikuwa Doreen.
"Hayupo? Ameenda wapi?"
"Sijui...sijuii ameto...ametoroka... Na pesa amechukua!"
"Umeona sasa mke wangu? Umeona faida za ubishi e??"
"Nisamehe mume wangu..."
"Nilishakusamehe
ila nilikuacha ujifunze.. Ila roho inaniuma sana kwa binti yangu.."
Alisema Baba Pamela kwa huzuni. Maneno yake yaliibua tumaini jipya kwa
mama Pamela na yakawa faraja tosha kwake. Lakini Pamela akawa kikwazo
sana kwake kwani bado alikazania msimamo wake kuwa mama yake ndiye
aliyemroga na kuchukua titi lake.
"Pamela
mwanangu... Mama yako hawezi kufanya hivyo isipokuwa mwanazaya yule
asiye na haya... Nilimwona tangu alipifika hapa ya kwamba ni mchawi ila
mke wangu hakuelewa... Alimwamini sana binti yule mwenye sura ya kondoo
kumbe chui"alisema Baba Pamela kwa sauti iliyojaa busara ya hali ya juu.
"Unamtetea mama.."
"Simtetei
ila utaujua ukweli tu... Naamini Mungu wa Mbinguni atafanya muujiza
wake hapa na lazima aliyekutenda hivi adhalilishwe.. In Jesus Name"
alisema Baba Pamela mwanaume aliyekuwa anamcha Mungu kupita kiasi,
alikuwa ni mwaminifu sana katika masuala ya Mungu kupita kiasi.
*****
Mr
Aloyce na Mlinzi walistaajabu sana baada ta kumuona Mama Eddy (maimuna)
akitoka nje mbio akiwa hajavaa nguo yoyote huku akihema kwa nguvu na
kupiga mayowe hovyo.
"Nimekosaaa!
Nimekosaaa" alilalama Mama Eddy huku akianguka chini na kujigaragaza
kama mtu anayecharazwa viboko na nyaya za umeme.
Mr
Aloyce na mlinzi walibaki wakiwa wamepigwa butwaa. Kila mmoja
alishindwa la kufanya zaidi ya kumtazama tu mwanamke yule aliyeendelea
kupiga kelele sana.
"Sirudiiii!sirudiiii nasema..." Alizidi kupiga kelele.
"Bosi kwani mama ana nini?" Aliuliza mlinzi.
"Unaniuliza nini na wewe si unamuona?" Alijibu Mr Aloyce.
Mama
Eddy alihangaika kwa muda mrefu pale nje. Mr Aloyce aliingia ndani na
kuchukua upande wa khanga ili akamsitiri mkewe lakini kila alipotaka
kumfunika mkewe alikimbia kama chizi pale nje hakutaka hata kujifunika
kwani alikuwa akiadhibiwa kupita kiasi bila kumuona MTU aliyemwadhibu.
Mr Aloyce ilibidi atulie tuli na kumuacha mkewe aendelee kutaabika kwani
yeye hakuwa na la kufanya.
Baada
ya muda mrefu kupita. Mama Eddy akaanza kutulia kidogo huku akihema kwa
nguvu lakini aliongea maneno ambayo hakuna aliyemwelewa.
"Mke wangu kulikoni?" Alisema Mr Aloyce kwa huruma.
"Nisamehe"
"Nikusamehe nini?"
"Nisamehe Mr Aloyce"
Mama
Eddy aliendelea kuomba msamaga bila kutaja kosa lake alilolifanya. Na
akiwa amekaa pale chini ghafla akaendelea kuisikia sauti iliyokuwa
inamwongelesha tangu alipokuwa ndani.
"Na hapo bado... Mpaka mlipie mateso mliyowatesa watu wasio na hatia" "sirudii tafadhali" alisema mama Eddy huku akipiga magoti.
Mlinzi Na Mr Aloyce walishindwa kumuelewa Mama Eddy kwani walihisi anazungumza peke yake .
"Hurudii nini?" Aliuliza Mr Aloyce.
"Naomba nikwambie ukweli baba Eddy...mimi....!" Alisema Mama Eddy.
Wakati huo mlinzi yule alikuwa akiwaza vitisho alivyotishwa na mwanamke yule pindi alipofika nyumbani pale.
'Mh kumbeee ni mchawii' aliwaza mlinzi.
"Ukweli upi" aliuliza Mr Aloyce kwa mshangao kwani katu hakujua kama kuna kitu kinaendelea nyuma ya pazia...
Itaendelea...
RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya 36 & 37
Reviewed by WANGOFIRA
on
21:32:00
Rating:
No comments: