Profesa Lipumba Asema Hana mpango wa kuhama CUF wala kuanzisha chama Kingine

Aliyekuwa mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amesema hana mpango wa kuhamia chama chochote.

Aidha amesema hana mpango wa kuanzisha chama chake kwa kuwa yeye bado ni Mwenyekiti halali wa CUF kwa mujibu wa Katiba ya chama hicho.

Akiongea katika kipindi cha Powerbreakfast cha Clouds FM Alhamisi hii, Profesa Lipumba amesema Katibu Mkuu wa CUF anataka kukiua chama cha CUF Tanzania bara.

“Mimi nipo CUF bado, na ni Mwenyekiti halali kwa mujibu wa Katiba na sina mpango wa kuhamia chama kingine,”

“Katibu Mkuu wetu anataka chama hiki upande wa bara kife kabisa na ibaki CHADEMA pekee yake ndio maana anafukuza wabunge.,”

Pia Lipumba amesema Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif alikosea kumnyima mkono Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein kwa kuwa unapoenda kwenye msiba jambo la msiba lilipaswa kutawala.

“Hata mimi nilipokutana na Maalim baada ya kunikatalia kurudi kwenye uenyekiti tulisalimiana.” Alisema Lipumba.

Katika hatua nyingine Lipumba alizungumzia sababu ya kutomkubali Mh. Edward Lowassa kuingia UKAWA.

“Sababu za msingi za kutomkubali Mh. Edward Lowassa kuingia UKAWA, ni kwamba ukiwa katika siasa unahitaji uongozwe na misingi na ‘principals’ na hoja kwamba mnagombea kitu gani, na sisi tulianzisha UKAWA kwa kusema kwamba tutafute nchi, serikali na dola inayowajibika ambayo inatengeneza mambo vizuri, inatumia rasilimali vizuri itapambana na ufisadi na itajenga demokrasia ya kweli katika nchi yetu, ukiwa na misingi hiyo kwamba utataka kiongozi ambaye anaunga mkono misingi hiyo na tulikuwa wote kwenye bunge la katiba na Mh. Edward Lowassa alikuwepo kwenye bunge hilo hakuwa mmoja ya wabunge aliyeunga mkono rasimu ya Katiba,” alisema Lipumba.

Alioongeza, “Kwahiyo ilikuwa ni kinyume kabisa na ile misingi iliyotuunganisha kwamba utataka kiongozi ambaye anaunga mkono misingi hiyo na ukumbuke Mh. Edward Lowassa alikuwepo katika bunge la katiba ya rasimu ya Jaji Warioba na hakuunga mkono rasimu hiyo kwahiyo ilikuwa ni kinyume kabisa na ile misingi iliyotuunganisha na kuanzisha UKAWA kuja kumchukua Edward Lowassa ndiye awe mgombea urais wa watu wanaounga mkono rasimu ya Jaji Warioba,”
Profesa Lipumba Asema Hana mpango wa kuhama CUF wala kuanzisha chama Kingine Profesa Lipumba Asema Hana mpango wa kuhama CUF wala kuanzisha chama Kingine Reviewed by WANGOFIRA on 15:41:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.