BARUA YANGU KWA RAIS WA JAMHURI TUKUFU YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DR. JOHN POMBE MAGUFULI.

Image result for magufuli
Rais mtukufu wangu popote ulipo salaam,

Ni matumaini yangu kuwa haujambo na unaendelea na shughuli hadhimu ya kutuletea maendeleo wananchi wa Tanzania na Afrika kwa ujumla.

Nianze barua yangu kwa kukupongeza kwa jitihada zako zilizotukuka za kuleta maendeleo ndani ya taifa letu ambalo lilikuwa limefanywa shamba la la bibi. Ambalo kila mtu mwenye nguvu alikuwa na uwezo wa kufanya lolote aliloona linampendeza kufanya. Hata kama likiwa baya kiasi gani.
Nipongeze jitihada zako za utumbuaji majipu unaoendelea nao ili kutengeneza taifa lenye nidhamu na uzalendo wa kazi na utaifa. Na kujenga utaifa kwanza ubinafsi na starehe baadaye. Hili ndilo tulilolitaka watanzania.

Pamoja na yote hayo nikupongeze pia kwa juhudi zako za kuinua elimu ya mtanzania kupitia sera ya elimu bure ambapo imempa fursa mtoto wa yule maskini na mkulima kuisoma bila shida. Lakini pia ukahakikisha watoto hao hawapati shida ya kukaa kwenye mawe na sakafuni bali wanakaa kwenye madawati, tena yenye ubora wa hali ya juu. Kwa hapo Mtukufu rais nakupongeza sana.

Kwenye sekta ya afya pia ni wazi siku chache tu baada ya kuingia madarakani ulifanya mabadiliko makubwa kwa kuhakikisha hospitali zetu zinakuwa kwenye ubora. Na kununua vitanda ambapo haapo awali wagonjwa na mama zetu walioenda kujifungua walikuwa wanalala chini wengine wakilala zaidi ya watu watatu kwenye kitanda kimoja.

Mtukufu rais kwa heshima kubwa uliyonayo kwa watanzania tunakupenda sana, kwani tunaamini unaweza kutuvusha kambo hii ambayo ni ngumu inahitaji maombi na juhudi nyingi, ambazo kwa uwezo wa kibinadamu si rahisi kuifikia.

Image result for magufuli zanzibar

Natamani kuiona Tanzania ya viwanda uliyotuahidi ambayo naamini muda si mrefu vitaanza kujengwa, na kuifanya nchi yetu kuwa yenye uchumi wa kati . na kuwa nchi ya kuvutia wawekezaji wakubwa na wadogo kutoka ndani na nje ya nchi kuja kuwekeza nchini kwetu. Ili tuendelee kiuchumi na kuwa mfano wa kuigwa kwa mataifa makubwa na madogo dunia.

Kwani nauchukia umaskini na wewew pia ni imani yangu kuwa unauchukia umaskini na ndiyo maana kila kukicha kwenye hotuba yako unashangaa kuhusu rasilimali na madini yote tuliyonayo lakini bado ni maskini. Mimi sijui lakini naamini kama mkuu wan chi unaweza ukawa na majibu ya kwa nini bado tu maskini .

Kwa maana unauchukia umaskini ni imani yangu ya kuwa muda si mrefu tanzani nchi yetu itakuwa tajiri kufautana na mikakati yako thabiti ya kuinua uchumi na kujenga nidhamu ya kazi.
Sitosahau juhudi unazozifanya kupambana na rushwa na ufisadi, ili kujenga taifa la watu waadilifu na wenye utu kwanza, hapa umeanzisha mahakama ya mafisadi. Ambayo ikianza kazi itawafunga wale waliotuhujumu na kujineemesha, kwa rasilimali za watanzania maskini ambao babu zetu walipigana kuikomboa nchi hii kutoka mikononi mwa wakoloni.

Ambapo walilifanya kuwa  taifa huru chini ya Hayati baba wa Taifa mwalimu Nyerere Mungu amupumzishe mahala pema, maana daima tutamkumbuka kwa harakati zake na mapenzi yake kwa taifa letu la Tanzania. Ambapo jina lake kamwe halitasahaulika mioyoni mwa watanzani na duniani kiujumla.

Mtukufu rais pamoja na juhudi zako hizo lakini leo imenibidi nikuandikie barua hii.  Ambayo ni kutoka chini ya uvungu wa moyo wangu, kukushauri juu ya masuala machache ambayo ninaamini yanaweza kutuvusha ikiwa utayatilia maanani na kuyafanyia kazi japo kwa kidogo.

Kusema kweli rais wangu imenibidi kukuandikia barua hii ambayo naamini hata kama hautoisoma kwa kuipuuza au kuitilia maanani naamini wasaidizi wako, au watakayoisoma watakufikishia ujumbe. Japo wengine waweza kuogopa kwa kukufikishia kwa kuogopa kutumbulia. Lakini binafsi imenibidi nikuandikie barua hii kama mwananchi wako na mzalendo wa nchi yangu ya Tanzania ambapo popote nikienda najivunia utanzania wangu.

Tangu uingie madarakani novemba 5, 2015 nimekuwa nikifuatilia hotuba zako ambazo binafsi nimekuwa nikizifurahia sana. Kwani zinalenga kujenga taifa lenye mshikamano na umoja.

Nikianza na ile ya ufunguzi wa bunge ambayo ilipongezwa sana na watanzania kwani nilitoa mwanga wa uongozi wako kwa kipindi cha miaka mitano ya kwanza. Lakini hotuba nyingine pia ambazo umekuwa ukizitoa sehemu mbalimbali. Zikionyesha kutoka moyoni na hata sura yako ikionyesha dhaili kuwa unachukia maskini na watu wengine wa tabaka la chini kunyanyaswa na wenye navyo.

Hapa naizungumzia hotuba yako uliyoitoa hivi karibuni ulipokuwa jijini mwanza kwa kuwatetea wachuuzi na wafanya biashara ndogo ndogo nchini wanaosumbuliwa na baadhi ya viongoz.  Na kuwafanya watanzania hawa wa hali ya chini kuishi maisha kama wakimbizi katika nchi yao ambayo imejawa na amani tele.

Waswahili wana msemo usemao mkubwa hakosei, lakini pia wengine wakasema mkubwa jaa. Lakini mimi nipingane kidogo na usemi huu ambao kwa uelewa wangu mdogo naona umepitwa na wakati. Maana binadamu tumeumbiwa kukosea na ndiyo maana waswahili wakasema kutenda kosa si kosa bali kurudia kosa.

Wakiwa na maana unaweza kutenda kosa mara moja lakini baada ya kuelewa utekosea unaweza kusahisha makosa au kasoro zilizojitokeza hapo awali ili kuepuka nkurudia kosa. Ambalo litajenga taswira mbaya ya kibuli, chuki, wivu,majivuno na dharau miongoni mwa watu.

Nasema hivyo mkuu wangu na mtukufu rais kutokana na kauli zako ambazo naweza sema huwa zina ukakasi japo wewe unaziona zipo sahihi. Na nyingine ambazo huwa unazitoa japo kwa matani lakini ukumbuke kuwa tunatofautiana mapokeo wengine wakiamini rais amesema hivyo tunabidi tutekeleze.

Nikiachana na hilo nije kwenye kauli zako ulizo zitoa hivi karibuni ulipokuwa kwenye ziara yako ya kuwashukru watanzania waishio katika visiwa vya Pemba na Unguja. Ambayo watu wengi nikiwemo na mimi mwenyewe kuwa ilikuwa imejaa kebehi, uhasama, ubabe, vitisho, vijembe na mambo mengine kadha wa kadha ambayo kiukweli hayakupaswa kuzungumza na mtu mwenye hadhi ya kwako.
Image result for magufuli zanzibar

Utakumbuka kuwa mgogoro wa Zanzibar ni wa muda mrefu ambao kama mkuu wan chi ulipaswa kwenda kuwaunganisha wazanzibar ambao wengi wao wamejawa na hasira kutokana na yale ambayo wanaamini hawatendewi sawa na serikali yao.

Image result for magufuli zanzibar
Kauli mbalimbali ulizozitoa Zanzibar kiukweli umetonesha donda ambalo lilikuwa limeanza kupona miongoni mwa wazanzibar. Lakini kwa kauli zako kiukweli zinaweza kuleta mpasuko mkubwa na kurudisha hali ya uhasama mkubwa visiwani humo kutokana na kauli zako ulizo zitoa.

Utakumbuka kuwa kurudiwa kwa uchaguzi wa Zanzibar kulitafsiriwa na mataifa makubwa na wadau mbalimbali wa maendeleo kama ni uonevu. Na upendeleo ambao ilikuwa ni dhahili faulu ya kutengenezewa upenyo wa ushindi kwa chama tawala ili kiongoze tena kwa mara nyingine. Lakini ukweli halisi unajulikana miongoni mwa tume ya uchaguzi ya Zanzibar.

Utakumbuka kuwa tume ilikuwa huru lakini kitendo cha kauli yako ya kumtaka Dr. Shein kumpa tuzo Jecha Salim Jecha kumezihilisha wazi kuwa ulikuwa mpango wa serikali kuvuruga uchaguzi ili chama tawala kiendeleze ubabe wake visiwani humo.

Kwa kweli haikuwa kauli ya kuitoa kama Rais wan chi tena kwenye hadhara ya watu wote wale ambapo, watu walikusanyika kuja kusikiliza nini rais wao atawaambia na kuwashukru kwa kumpa sifa ya kuwa Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Pia kauli yako ya kumtaka Dr. Shein Kutomsainia pesa ya matibabu mpinzani wake Maalim Seif kwa kisa cha kutokumpa mkono, kiukweli imeonyesha wazi kuwa haumpendi na unafurahia migogoro inayoendelea.

Nilitegemea kama mkuu wa nchi kuwaweka pamoja watu hawa kwa kuwa uchaguzi umekwisha, waweze kushirikiana pamoja ili kujenga Tanzania yenye amani na upendo baina ya watanzania. Lakini mkuu wangu ulienda kutonesha donda ndugu ambalo limeuguzwa kwa muda mrefu tena kwa kulipiga na nyundo nzito.

Itakumbukwa kuwa marudio ya uchaguzi wa Zanzibar yaliifanya serikali ya Tanzania kusitishiwa fedha zilizokuwa zinatolewa na mfuko wa changamoto za maendeleo kutoka Marekani  MCC na nchi nyingine wahisani walisitisha misaada yao kwa kile walichokiona ni kubanwa kwa demokrasia visiwani Zanzibar.

Ni rai yangu kwa viongozi na timu ya washauri wako wakaona umuhimu wa kukuandalia hotuba ambayo utaisoma mbele ya kusanyiko lolote ambalo utaenda. Ili kuepusha kutiririka kwa maneno ambayo yanaweza kupandikiza chuki na uhasama baina ya wananchi wan chi hii na viongozi wao au baina ya chama tawala na vyama pinzani.

Japo itakuwa vigumu kwako kusoma neno kwa neno lakini itasaidia kuondoa maneno amabyo yanakera baadhi ya watanzania na mataifa mengine yanayokutazama kwa mkuwa mfano bora. Maana kwa muda mchache ambao umekaa kwenye kiti hiki mataifa makubwa yamekusifu na baadhi ya viongozi wa kimataifa umekuwa mfano wao wa kuigwa kama kiongozi.

Ni wako katika ujenzi wa taifa hili, Baraka Ngofira,  mwananchi mzalendo wa Tanzania.


Mungu ibariki Tanzania, Mungu Mbariki rais wetu mtukufu John Pombe Magufuli na watanzania wote ili Amani na Upendo vikatawale daima.
BARUA YANGU KWA RAIS WA JAMHURI TUKUFU YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DR. JOHN POMBE MAGUFULI. BARUA YANGU KWA RAIS WA JAMHURI TUKUFU YA MUUNGANO WA TANZANIA, MHESHIMIWA DR. JOHN POMBE MAGUFULI. Reviewed by WANGOFIRA on 04:26:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.