ACT-Wazalendo Wambipu Magufuli......Watangaza kufanya kongamano la kidemokrasia Septemba, 24

Chama cha ACT – Wazalendo kimetangaza azma yake ya kufanya mkutano mkuu wa kidemokrasia Jumamosi ijayo licha ya kuwapo kwa amri ya Polisi iliyokataza kufanyika kwa mikutano yote ya kisiasa nchini. 

Jeshi la Polisi lilipiga marufuku maandamano na mikutano yote ya hadhara tangu Juni 7 hadi pale hali ya usalama itakapotengemaa. 

Jeshi hilo lilisema limefikia hatua hiyo baada ya kupokea taarifa kutoka kwa vyama vya siasa vikitaka kufanya mikutano na maandamano kwa lengo la kuwahamasisha wananchi kutotii sheria za nchi.

Lakini jana, Katibu wa Itikadi, Mawasiliano na Uenezi wa ACT – Wazalendo, Ado Shaibu alisema wamepanga kufanya mkutano huo kwa sababu Katiba inawaruhusu.

“ACT kimekusudia kuitisha mkutano mkuu wa kidemokrasia, hii ni haki yetu kikatiba na hata kwa dunia nzima si ajabu kwa kuwa vyama vya siasa hufanya hivyo. Kongamano hili litawaleta pamoja wanachama, wadau na wafadhili wa ACT ambao watajadili hali ya maendeleo ya nchi,” alisema na kuongeza.

“Hatutaji mahali na ukumbi tutakaoufanyia kwa sasa, wakati ukifika tutawajulisha.Na hatutaomba kibali kwa kuwa katiba haisemi vyama vya siasa viombe  kibali vinapotaka kufanya mikutano ya ndani.

Shaibu alisema kuwa endapo serikali itazuia kufanyika kongamano hilo watachukua hatua za kisheria kupinga maamuzi hayo kwa madai kuwa katiba ya nchi na ya vyama vya siasa inarushusu kufanyika.

“Serikali ilituzia kufanya mikutano na vikao vya ndani, tulikaa kimya awali tukiamini kuwa tutaishawishi kwa hoja na itajirekebisa lakini haikufanya hivyo.Tunaamini serikali itarudi nyuma na kuamini haina mamlaka ya kuzuia mikutano na vikao vya ndani kwa sababu kuizuia inamaana unafuta shughuli za siasa na sisi tutakuwa wa mwisho kukubali vyama kufutwa ,” alisema.

Alisema ACT haitokuwa nyuma kuiunga mkono serikali inapofanya vyema na kwamba endapo chama hicho kitakosoa utendaji kazi wake, serikali isikichukie kwa kuwa kinatekeleza wajibu wajibu wake.

Kwa upande mwingine, Shaibu alisema Kamati Kuu ya Uongozi wa Chama cha ACT imefanya baadhi ya marekebisho ya muundo wa uendeshaji kwa kuteua baadhi ya makatibu wa kamati za chama hicho.

“Kikao cha tatu cha kamati kuu kilichoketi Septemba 5,2016 kilifanya teuzi mbalimbali za makatibu, sambamba na kugawa baadhi ya kamati ikiwemo iliyokuwa kamati ya Ulinzi, Usalama na Uadilifu ambapo kwa sasa imegawanyika na kuwa kamati ya Usalama na Ulinzi na mpya ni Kamati ya Uadilifu, ” alisema.

Aliwataja makatibu wapya wa kamati walioteuliwa akiwemo aliyewahi kuwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Vijana Chama cha Wananchi CUF (JUVICUF) Mohamed Babu ambaye kwa sasa ni Katibu wa Kamati ya Ulinzi na Usalama, Ally Kifu ameteuliwa kuwa Katibu wa kamati ya Fedha na Miradi ya Kujitegemea. Katibu mwingine aliyeteuliwa ni Sabrah Mohamed ambaye ameshikilia Kitengo cha Kushughulikia Maendeleo ya Zanzibar.
ACT-Wazalendo Wambipu Magufuli......Watangaza kufanya kongamano la kidemokrasia Septemba, 24 ACT-Wazalendo Wambipu Magufuli......Watangaza kufanya kongamano la kidemokrasia Septemba, 24 Reviewed by WANGOFIRA on 21:08:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.