Mtuhumiwa Auawa Ndani ya Kituo cha Polisi


MKAZI wa Kwere wilayani Babati Mkoa wa Manyara, Mohamedy Pagweje (29), amepigwa na kufa na mtu anayedaiwa kuwa hana akili timamu aliyewekwa naye katika chumba cha mahabusu katika Kituo cha Polisi cha Mkoa wa Manyara, kilichopo wilayani Babati.

Hata hivyo, ndugu wa Pagweje ambaye ni fundi ujenzi wa eneo hilo, wamekataa kuuchukua mwili kwa maziko wakitaka kujua ukweli wa kifo chake baada ya kupigwa akiwa mahabusu katika Kituo cha Polisi cha Babati.

Mama mzazi wa kijana huyo Hadija Pagweje, akizungumza na waandishi wa habari jana nje ya ofisi ya Mkuu wa Wilaya hiyo, Raymond Mushi, alisema alimkabidhi mtoto wake kituoni hapo saa 8:00 mchana juzi akiwa salama.

Alisema alimfikisha mwanawe kituoni hapo baada ya kijana huyo kulewa pombe na kutishia kujiua kutokana na kutolipwa fedha za ujenzi kutoka kwa askari aliyemjengea nyumba. Askari huyo ametajwa kwa jina moja la Justine.

“Nilimwacha hapa kituoni mahali pa usalama na kuwaomba askari wa zamu wanisaidie maana kijana wangu amekunywa pombe nyingi, anatishia kujiua kwa madai kuwa amekosa haki yake. Nilifanya hivyo nikijua kituo cha polisi kina usalama ili angalau pombe ziishe, jioni nimchukue,” alisema.

Alipokwenda kupeleka chakula polisi walimtaka arudi tena saa 12:00 jioni, aliporudi kituoni hapo alishangaa kuona baadhi ya watu wakimshangaa na kumjulisha kuwa kijana wake amepigana na mahabusu mwenzie na kuwa amepelekwa Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Babati ya Mrara kwa matibabu.

Alisema alipokwenda katika hospitali hiyo alikutana na askari ambaye alimfahamisha kuwa mtoto wake alikuwa amefariki dunia. Baba wa marehemu Amiri Shabani alisema alipata taarifa ya kifo cha kijana wake saa 1:00 usiku juzi baada ya kuelezwa kuwa mtoto wake alikufa akiwa anadai Sh 200,000 kutoka kwa askari huyo.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Manyara, Francis Massawe alikiri kutokea kwa tukio hilo, saa 8:00 mchana Agosti 8, mwaka huu ambapo alisema mama wa marehemu alimpeleka kituoni hapo kijana wake Pagweje, fundi ujenzi akidai kuwa alikuwa akimletea fujo na alifunguliwa mashtaka ya kutishia kuua.

Alipoingizwa mahabusu alipigana na mahabusu mwenzake Bura Malireh (19) mkulima na mkazi wa Gijedaboung Kata ya Mamire wilayani humo, ambaye ilidaiwa alikuwa mgonjwa wa akili.
Mtuhumiwa Auawa Ndani ya Kituo cha Polisi Mtuhumiwa Auawa Ndani ya Kituo cha Polisi Reviewed by WANGOFIRA on 08:08:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.