Yanga karata muhimu leo

 Wachezaji wa Yanga wakishangilia bao katika moja ya mechi zao kwenye Uwanja wa Taifa Dar es Salaam. Yanga leo itakuwa Ghana katika mechi muhimu ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya Medeama ya huko. (Picha ya Maktaba).

KIKOSI cha Yanga leo kitakuwa na kibarua kigumu wakati kitakapokabiliana na wenyeji wao Medeama FC ya Ghana katika mchezo wa marudiano wa kombe la Shirikisho Afrika.
Mchezo huo utachezwa kwenye uwanja wa Sekondi Takoradi nje kidogo ya Jiji la Accra kuanzia saa 12:00 jioni kwa saa za Tanzania.

Katika mchezo wa kwanza uliofanyika Uwanja wa Taifa Dar es Salaam timu hizo zilitoshana nguvu kwa kutoka sare ya kufunga mabao 1-1, matokeo ambayo yalizidi kuiweka pabaya Yanga.

Yanga inahitaji ushindi katika mchezo wa leo ili ijinasue mkiani mwa kundi hilo na kufufua matumaini ya kucheza nusu fainali endapo watashinda mechi zao mbili zitakazosalia huku wakiwaombea mabaya wapinzani wao MO Bejai ya Algeria na Madeama zipate matokeo mabaya kwenye mechi zao zijazo.

Kocha Hans van Pluijm atamkosa beki Vicent Bossou kwenye kikosi chake kutokana na kuwa na kadi mbili za njano lakini nafasi yake huenda ikachukuliwa na nahodha Nadir Haroub ‘Cannavaro’ ambaye hiyo itakuwa mechi yake ya kwanza tangu kuanza kwa hatua hiyo ya makundi.

Pamoja na kuzidiwa na wapinzani wao Medeama katika mchezo wa kwanza, Pluijm ameondoka nchini akiwa na matumaini makubwa ya kupata ushindi katika mchezo huo wa leo huku akiwatumaini washambuliaji wake wawili Donald Ngoma na Obrey Chirwa ambao wameonekana tishio kwa wenyeji wao.

Pluijm alisema ameupa uzito mkubwa mchezo wa leo kwa sababu ndiyo uliobeba matumaini yao ya kufika kule ambapo walipakusudia wakati wanajiandaa na hatua hiyo ya makundi na hiyo inatokana na maandalizi ambayo wameyafanya kabla ya kuondoka nchini.

“Tutawakosa Bossou na Deusi Kaseke, lakini waliobaki wote wapo katika hali nzuri na ninafurahi kuona wachezaji wangu wote katika hali nzuri kuelekea mchezo huo naamini tutawashangaza wenyeji wetu Medeama kwa kuwafunga wakiwa nyumbani kwao,”alisema Pluijm.

Kocha huyo alisema kwa kuwa wanahitaji pointi tatu katika mchezo huo hawatocheza kwa kujihami bali watacheza kwa kushambulia zaidi huku akijaza viungo wengi katikati ili kusaidia ulinzi kwa sababu wapinzani wao wanatumia sana mashambulizi ya kustukiza.

Kwa upande wao Medeama ambao wanashika nafasi ya tatu kwenye kundi hilo wakiwa na pointi mbili, wametamba kuimaliza Yanga katika mchezo huo kwa sababu wanawajua vizuri wapinzani wao baada ya kuwaona katika mchezo wa kwanza ulioisha kwa sare ya 1-1.

Kocha Pride Yaw Owusu, alisema Yanga ni timu ngumu na nzuri lakini amewaanda vyema vijana wake kuhakikisha wanapambana kwa dakika zote 90, ili kupata ushindi ambao utawahakikishia kucheza hatua inayofuata ya nusu fainali.

“Najua kama Yanga wamekuja na nguvu kubwa ya kutafuta ushindi wakiwa ugenini lakini hata sisi tunahitaji pointi tatu ambazo zitatuweka kwenye nafasi nzuri ya kumaliza wa pili kwenye kundi letu ili tucheze nusu fainali hivyo hatutakubali kupoteza mchezo huo hata kidogo,” alisema.

Owusu alisema ataingia kwenye mchezo huo akitegemea huduma ya mshambuliaji wake Bismark Oppong, katika umaliziaji na kwa mbinu na mikakati waliyoipanga anaamini wanayo nafasi ya kushinda mchezo huo.
Kocha huyo alisema licha ya kikosi chake kuwa na uchovu kutokana na kukosa muda wa kupumzika, baada ya juzi kucheza mechi ngumu ya ligi ya Ghana dhidi ya Liberty Professionals na kuibuka na ushindi wa bao 1-0 wakiwa nyumbani Sekondi Tokaradi.

Medeama inayoshika nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi ya Ghana, kupitia kwa kocha wao wameapa kufanya maajabu kwenye michuano hiyo ikiwa ni mara yao ya kwanza kufika hatua hiyo ya makundi.
Yanga karata muhimu leo Yanga karata muhimu leo Reviewed by WANGOFIRA on 20:48:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.