Waziri Mkuu Majaliwa Akagua Kiwanda Cha Kutengeneza Vigae Cha Goodwill Ceramic Cha Mkuranga

WAZIRI MKUU Kassim Majaliwa amesema Serikali itahakikisha viwanda vinajengwa kwa wingi nchini kwani ndiyo msingi imara wa ukuaji wa uchumi na muarobaini wa tatizo la ajira hususan kwa vijana.

“Mbali na kukuza uchumi na kuongeza fursa za ajira nchini, viwanda hivi ndivyo vitakavyotufanya tununue bidhaa kwa bei nafuu tofauti na ilivyo sasa kwa kuwa vitu vingi vinaagizwa kutoka nje ya nchi,” alisema.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo jana (Jumatano Julai 13, 2016) wakati akikagua ujenzi wa kiwanda cha kutengeneza vigae (Tiles) cha Goodwill Tanzania Ceramic katika kijiji cha Mkiu wilayani Mkuranga, Pwani.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa kiwanda hicho Bw. Frank Yang alisema jumla ya ajira 4,500 zinatarajiwa kutolewa kiwandani hapo mara ujenzi utakapokamilika.

Akifafanua kuhusu ajira hizo Bw. Yang alisema ajira 1,500 zitakuwa rasmi na zisizo rasmi zitakuwa 3,000 huku wakazi wanaoishi katika maeneo yanayozunguka kiwanda hicho wanatarajiwa kupewa kipaumbele. Mkurugenzi huyo alisema ujenzi wa kiwanda hicho utagharimu dola milioni 100 na utafanyika kwa awamu mbili. Awamu ya kwanza inatarajiwa kukamilika Desemba mwaka huu.

“Ujenzi wa kiwanda hiki utainua ukuaji wa uchumi nchini Tanzania kwani utakapokamilika Serikali itakusanya sh. bilioni 30 kwa mwaka ikiwa ni mapato ya kodi,” alisema.

Naye Balozi wa China nchini Tanzania Dk.Lu Youqing aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa kuchagua sekta ya viwanda kuwa ndiyo kipaumbele chake katika kukuza uchumi. Alisema mbali ya ujenzi wa kiwanda cha vigae katika eneo hilo pia wawekezaji hao kutoka nchini China wanatarajia kujenga viwanda vya mbolea, karatasi na glasi (bilauli).

Katika hatua nyingine, Waziri Mkuu alipokea msaada wa madawati 500 yenye thamani ya sh milioni 40 ambayo yalitolewa na Balozi wa China nchini Dk. Lu kwa kushirikiano na Mkurugenzi Mtendaji wa Kiwanda cha Goodwill Tanzania Ceramic Bw. Yang.
Waziri Mkuu Majaliwa Akagua Kiwanda Cha Kutengeneza Vigae Cha Goodwill Ceramic Cha Mkuranga Waziri Mkuu Majaliwa Akagua Kiwanda Cha Kutengeneza Vigae Cha Goodwill Ceramic Cha Mkuranga Reviewed by WANGOFIRA on 20:17:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.