Wasomi Wamfagilia Sumaye..Wadai Atakuwa Msaada Mkubwa CHADEMA

Wasomi nchini wamesema iwapo Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye atakuwa mwenyekiti wa Chadema Kanda ya Pwani, atasaidia kukijenga chama hicho cha upinzani nchini, kuanzia ngazi ya chini.


Wakizungumza kwa nyakati tofauti walisema jana kuwa Sumaye ambaye juzi alirejesha fomu ya kuwania nafasi hiyo, katika ofisi za kanda hiyo Dar es Salaam, akitumia uzoefu alionao kiuongozi, atakuwa msaada kwa chama hicho.


Walisema uamuzi huo umeonyesha kuwa hakuhamia Chadema kwa masilahi binafsi. Profesa George Shumbusho wa Chuo Kikuu cha Mzumbe alisema: “Inaonekana (Sumaye) ana lengo la kusaidia upinzani ukue. Kwa mchango na uzoefu wake serikalini ataisaidia sana Chadema maana chama lazima kiwe na nguvu kuanzia ngazi ya chini.”


Sumaye ndiye Waziri Mkuu pekee katika historia ya Tanzania kushika wadhifa huo kwa miaka 10 baada ya kuwa msaidizi wa Rais mstaafu, Benjamin Mkapa kati ya mwaka 1995 hadi 2005.


Agosti mwaka jana, Sumaye aliyekuwa kete muhimu katika kampeni za aliyekuwa mgombea urais wa Chadema, Edward Lowassa kutokana kuikosoa Serikali na kuwataka Watanzania kutoichagua CCM, alitangaza kuachana na chama hicho tawala na kujiunga na upinzani.


Shumbusho alisema ameonyesha kuwa yeye siyo aina ya wastaafu wanaopenda sifa na hakwenda kusaka ulaji Chadema huku akibainisha nchi ikiwa na upinzani imara, chama kilichopo madarakani hugangamala.
Wasomi Wamfagilia Sumaye..Wadai Atakuwa Msaada Mkubwa CHADEMA  Wasomi Wamfagilia Sumaye..Wadai Atakuwa Msaada Mkubwa CHADEMA Reviewed by WANGOFIRA on 20:29:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.