Sita wauawa katika shambulio dhidi ya mabasi Kenya
Watu sita wameuawa nchini Kenya baada ya washambuliaji wanaoshukiwa kuwa
wa kundi la itikadi kali la Al-Shabaab kuyafyatulia risasi mabasi
mawili kaskazini mashariki mwa nchi hiyo karibu na mpaka na Somalia.
Inspekta Jenerali mkuu wa Polisi IGP Joseph Boinnet, amesema maafisa wa
jeshi hilo walioko kwenye eneo la tukio walikuta watu sita wakiwa
wamepigwa risasi na kuuawa, na kuongeza kuwa msako dhidi ya magaidi hao
ulikuwa unaendelea.
Boinnet alisema watu wengine wawili wamejeruhiwa, lakini mratibu wa
usalama wa kanda ya Kaskazini-Mashariki Mohammed Saleh alisema watu
wengi walijeruhiwa. Haikubainika bado iwapo wahanga wa shambulio hilo
walikuwa raia au maafisa wa polisi waliokuwa wanatoa ulinzi katika
mabasi hayo.
Shambulio hilo la Ijumaa asubuhi limetokea karibu na El Wak katika
kaunti ya Mandera, eneo maskini la vijiji katika nchi hiyo ambako
mashambulizi ya maafa sawa na hilo katika siku za nyuma yamedaiwa na
kundi la Al-Shabaab lenye mafungamano na mtandao wa Al-Qaeda.
Kamishna wa kaunti ya Mandera Fredrick Shisia ameliambia shirika la habari la Reuters, kuwa shambulio hilo lilitokea majira ya saa tatu na nusu asubuhi ya Ijumaa, wakati mabasi hayo yakisafiri kwenda mjini Mandera kutoka mji mkuu Nairobi.
CHANZO: DW
Sita wauawa katika shambulio dhidi ya mabasi Kenya
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:37:00
Rating:
No comments: