RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya Ishirini

MTUNZI: ENEA FAIDY

.....EDDY aliumia sana kwa taarifa zile za kifo cha mama yake. Hakutaka kuamini kama kweli mama yake hatakuwa pamoja nao tena. Machozi yalimbubujika kwa kasi huku akimwita mama take kana kwamba alikuwa karibu yake.

Mr.Alloyce alishindwa kuvumilia, alijikuta akiungana na mwanaye kulia. Walilia sana mpaka machozi yaliwakauka, Mr Alloyce alichukua leso yake na kujifuta machozi yake kisha akachukua simu ili awajulishe ndugu na marafiki kuhusu kifo cha mkewe.

Moyo wake ulisita sita sana kwani aliwaza ni jinsi gani ndugu wangeupokea msiba ule wa ghafla bila hata maiti.
"Eddy watanielewaje shemeji zangu? Umesababisha yote haya mwanangu, lakini siwezi kukulaumu!" Alisema Mr Alloyce huku machozi yakimlengalenga.
"Nisamehe dady kwa kuwa chanzo cha matatizo yote!" Alisema Eddy na kuendelea kulia.

Lakini hawakuwa na jinsi ya kufanya kwani tayari maji yalikwisha mwagika na ilikuwa vigumu sana kuzoleka. Ilibidi wakubaliane na kilichotokea ingawa kishingo upande sana.

Mr Alloyce alitafuta namba kwenye simu yake, MTU wa kwanza kumpata alikuwa shemeji yake aishiye jijini Dar ( Dada wa mama Eddy). Simu iliita kisha ikapokelewa, kwa kutetemeka na woga Mr Alloyce akaanzisha mazungumzo.

"Halloo Shem"
"Niambie Shem wake mie.. Kwema huko?" Alisema shemeji take Alloyce kwa uchangamfu sana kama ilivyokuwa kawaida yake. Hakuijua msiba mzito uliokuwa moyoni mwa Mr.Alloyce.
"Huku sio kwema Shem..!" Aliens Mr Alloyce.
"Sio kwema kuna nini?" Alishtuka.
"Sio kwema naomba kesho mfike nyumbani kwangu tafadhali.."
"Kuna nini shemeji? Naomba niambie tu.. Nini kimetokea?"
"Utajua kila kitu kesho..!"
"Hapana..niambie Leo.. Au MPE mama Eddy simu niongee nae..!" Maneno hayo yalimkata maini Baba Eddy hakuelewa ajibu nini akabaki kimya kwa sekunde chache akitafakari cha kujibu lakini ghafla akasikia sauti Kali ya Eddy ikimwita."Daaaaaaaaady!" 

Mr Alloyce alishtuka sana kwani Eddy alikuwa ametoka sebuleni pale dakika chache zilizopita wakati yeye akiongea na simu. Hofu ikamkamata ghafla na kumfanya Mr Alloyce atupe simu sofani na kuelekea sauti ya Eddy inakotokea. Eddy aliita tena "Daaaaaaaady!" Mara hii sauti ile iliambatana na mwangwi mkali uliozidi kumtisha Mr Alloyce.

Alitoka sebuleni na kwenda koridoni lakini hakumuona Eddy. Akasikia sauti ikitokea chooni, alikimbia haraka na kwenda chooni lakini hakumuona, ghafla sauti ya Eddy ikasikika tena ikitokea chumbani kwa Eddy ilibidi amfuate haraka lakini cha kusikitisha Mr Alloyce hakumkuta Eddy ila alikuta damu nyingi zikiwa sakafuni. Alishtuka sana.

*****
Doreen aliamua kuondoka katika shule ya mabango kwani mambo yake yalikwishaanza kuharibika hivyo aliona heri aondoke zake kabla mambo makubwa hayajampata. Na yote hiyo ilitokana na maombi makali aliyokuwa akiyafanya Nadia Joseph ili kuinusuru shule yake kwa majanga yanayoikumba kila kukicha. Aliamua kujitesa kwa kufunga kila siku ili mradi tu shule yao ikomboke na irudi katika mstari ulionyooka.

Hakika Sikio la Mungu si zito ili lisisikie, Mungu alisikia maombi ya Nadia ndio maana alianza kuharibu mambo ya Doreen taratibu.Doreen alimchukia sana Nadia, akaahidi kumfanyia kitu kibaya sana ili alipize kisasi

"Ipo siku yake... Nitamwadhibu huyu mshe** kwa alichonifanyia... Nimeondoka kwasababu yake... Ila hata ipite miaka kumi ntampata tu!" Alijisemea Doreen na kusonya. Wakati huo akiwa njiani kuelekea nyumbani kwa mwalimu Jason kwani alipajua vizuri sana.

Alitembea kwa haraka kwa mwendo wa nusu SAA nzima hatimaye akawasili ndani ya nyumba ya Mwalimu Jason ili akatazame kinachoendelea.

Aliongia mdani na kukutana na ukimya mzito. Kwa ujasiri na kujiamini sana Doreen aliingia chumbani kwa Mwalimu Jason na kukuta harufu Kali ya damu na mwili wa mwalimu Jason.

Kwa wakati huo Judith alikuwa tayari amechapa lapa ili kuiepuka kesi ya mauaji ambayo ingemkabili. Na kama angekuwepo ndani mle basi ingekuwa nyama ya Doreen kwani angetumia vizuri nafasi ile kupata titi la Judith.

Doreen aliutazama mwili wa Jason kisha akaachia sonyo Kali. Akakisogelea kitanda na kutafuta karatasi lake, akalikuta chini ya mto. Akachukua na kulitia kwenye mkoba wake kisha akaondoka zake.

Akashika njia kuelekea kituo cha mabasi cha mkoani Iringa ili atafute gari liendalo mkoani Mbeya aende huko.Alipokuwa njiani alitazama pesa aliyokuwa nayo alishtuka kidogo kwani ilikuwa ni shilingi elfu moja tu ambayo haitoshi kwa lolote. Akawaza kwa sekunde kadhaa jinsi ya kufanya akapata jibu kisha akaendelea na safari yake.Alipofika mbele kidogo aliona duka kubwa limeandikwa Sanga Mini Market akaingia mle.

"Karibu! " sauti ya mwanaume mwenye duka ilimkaribisha.
"Asante! Nataka pop corn moja!"
"OK.. Ya 500 au 1000?."
"Nipe ya 500.." Alisema Doreen na alijua kabisa ana shilingi elfu moja. Lakini kuna kitu alitaka kufanya, alitaka kuiba pesa kwa kutumia ile shilingi elfu moja yake.

Mzee yule alitoa popcorn na kumkabidhi Doreen.Doreen alichukua shilingi elfu moja kwenye mkoba wake na kumpa Muuza duka. Muuza duka alipokea akataka kumrudishia chenji lakini ghafla akasita.

"We mtoto unanichezea? Hebu rudisha hizo popcorn... Shika hela yako.. Mpuuzi mkubwa wewe unataka kuniletea wanga wako hapa?" Alifoka muuza duka yule kwa jazba kwani alipoipokea hela ile akaugundua mchezo mzima wa Doreen aliotaka kuifanya. Doreen alishtuka, akaona aibu.

"Kwani vipi baba?" Alisema Doreen kwa upole kwani uligundua Mzee yule in kiboko zaidi yake.
"Wewe mtoto ntakuumbua hapa? Toka zako...." Mzee yule aliitupa chini hela Doreen na kumnyang'anya kwa nguvu ile popcorn.

"Unafikiri tunauza kizembe? Wachezee huko huko hii namba tasa sio shufwa..!" Alisema Mzee yule Doreen akiwa anaondoka.Doreen aliona aibu sana lakini hakukata tamaa kwani alijua tu atapata mtu ambaye hana zindiko lolote.

Uzuri wake uliwachanganya wengi sana kwani kila alipopita alikuwa akitazamwa kama nyota ya alfajiri huku wengine wakimpigia miruzi na wengine wakijaribu kumwita majina wanayoyajua wenyewe ili tu wabahatishe jina lake. Ni kweli Doreen alikuwa mzuri kupindukia, aling'aa kama m balamwezi ila tabia zake za ndani zilitisha zilokuwa mbaya kama Israel mtoa roho.

Alitembea taratibu na kuingia kwenye mgahawa mmoja wa vyakula. Aliketi kisha akaagiza chipsi kavu za shilingi mia saba.

"Sahani moja elfu moja?"
"Samahani Dada nina mia saba tu nisaidie.. Nimetoka mbali na nina njaa sana..!" Alisema Doreen kwa upole sana ambapo aliweza kumshawishi kirahisi muuzaji, akamkubalia kwa kumuonea huruma. 

Watu walikuwa wengi mhahawani mle, Doreen alijiinamia chini tu akisubiri aletewe chipsi zake. Kwa muoneakano wa haraka ilikuwa vigumu sana kubaini tabia za Doreen kwani alionekana mpole na mkarimu sana.

Chipsi sake zikaletwa, ilibidi atoe hela na arudishiwe chenji yake. Chenji ambayo ilikuwa tofauti na kiwango kinachostahili.
*****
Ulimi wa Mwalimu John ulikuwa mzito kutamka neno lolote. Kila akijaribu kusema chochote maneno yalikuwa hayaeleweki ndipo mkewe akabaini kuwa tayari mumewe amekuwa bubu. Roho ilimuuma sana kwani mumewe asingeweza kufanya kazi tena. Wataishi vipi mjini bila kazi? Aliwaza mkewe.

Lakini licha ya kuumia moyo ila alimshukuru Mungu kwa uhai alioachiwa mumewe. Siku zikaendelea kusonga.Ilikuwa saa mbili usiku nyumbani kwa mwalimu John.Ukimya ulitawala sebuleni pale kwani ndugu wote walikuwa wameenda majumbani mwao hivyo walibaki wawili tu, ghafla mlango uligongwa. 

"Karibu! " alikaribisha Leyla mke wa mwalimu John. Bila kutegemea aliingia Judith, kwani alikuwa akipafahamu vizuri nyumbani kwa mwalimu John. Na hii ilitokana na ukaribu waliokuwa nao mwalimu John na Jason, hivyo mwalimu Jason alimtambulisha Judith kama mkewe mtarajiwa.

"Karibu.." Alimkaribisha Leyla.
"Asante.. Za hapa!"
"Nzuri kiasi.. Umefika lini?"
"Tangu juzi.." Alisema Judith lakini alionekana mwenye hofu na mawazo mengi.
"Karibu.. Ulikuwa kwa Jason?"

Swali like liliibua kumbukumbu ya tukio aliloshuhudia kwa mpenzi wake. Machozi yalimshuka kwa kasi, lakini alishangaa sana kwanini tangu amefika Mwalimu John hajasema lolote.

"Hamjasikia chochote kuhusu Jason?"
"Ndio.. Kwani kuna nini?" Alishtuka sana Leyla.
"Ni stori ndefu sana ila mwalimu Jason alijiua!"
"Ati nini?"
"Ndio.. Inaniuma sana... Alitaka kuniua Mimi lakini akabadili msimamo na kusema bora ajiue yeye.." Aliendelea Julia Judith
"Kwanini?"
"Alisema ana sharti la.." Kabla Judith hajaendelea....
 
itaendelea..... 
 
 KWANINI DOREEN ANAKUWA KATILI KIASI KILE? ATAFANIKIWA KUPATA TITI? NA NINI HATMA YAKE USIACHE KUFUATILIA.
RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya Ishirini RIWAYA: Mwanafunzi Mchawi - (A Wizard Student) - Sehemu ya Ishirini Reviewed by WANGOFIRA on 08:31:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.