Pengo awaasa mapadri
ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp
Kardinali Pengo, amewataka mapadre wa Kanisa Katoliki kutambua kuwa
kazi waliyonayo ni kubariki na si kulaani.
Pengo alitoa mwito huo jana kwenye misa ya upadirisho kwa mashemasi
watatu iliyofanyika katika Kanisa la Mtakatifu Petro lililopo Oysterbay,
jijini Dar es Salaam.
Misa hiyo ilihudhuriwa na Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, masista na mapadre mbalimbali pamoja na waumini.
Mashemasi hao waliopewa daraja la upadri ni James Ngonyani, William
Sindano na Francisco José ambao wote walipangiwa vituo vya kazi katika
jimbo la Dar es Salaam huku Pengo akiwataka wawe tayari kufanya kazi
watakapohitajika katika majimbo mengine.
Upadrisho huo umefanya jimbo kuu la Dar es Salaam kuwa na jumla ya
mapadri 74 ikiondolewa wa mashirika mbalimbali. Alisema kamwe lisitokee
neno la laana kutoka katika midomo ya mapadre bali litoke neno la baraka
kwao kwenda kwa waumini.
Aliwataka wawe watu wa kutoa faraja kwa waumini kama ambavyo maagizo ya Mungu yanavyoelekeza.
Awali Askofu Pengo aliwakumbusha pia mapadre kuwa parokia zote ziko
katika Jimbo Kuu la Dar es Saam chini ya Askofu Mkuu na kwamba hakuna
parokia ambayo ni ya shirika.
Askofu Pengo alitangaza pia parokia mpya tano ambazo ni Parokia ya
Wazo, Mikoroshoni, Tabata Kisiwani, Magole na ya Mbagala Kuu ambazo
zimefanya parokia za jimbo hilo kuwa 100.
Pengo awaasa mapadri
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:14:00
Rating:
No comments: