VIGOGO 12, NSSF WATUMBULIWA
Mwenyekiti wa Bodi ya wadhamini ya NSSF, Profesa Samwel Wangwe |
BODI ya Wadhamini ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF)
imeagiza kusimamishwa kwa wakurugenzi sita, mameneja watano na mhandisi
mmoja wa shirika hilo kupisha uchunguzi, kubaini wahusika katika tuhuma
za ubadhirifu, matumizi mabaya ya ofisi na kutofuata kanuni, sheria na
taratibu katika uwekezaji, usimamizi wa miradi, manunuzi ya ardhi na
ajira.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya NSSF, Profesa Samwel Wangwe,
alikiri katika mazungumzo na gazeti hili jana usiku kusimamishwa kwa
vigogo hao 11, kupisha uchunguzi wa tuhuma zilizoelekezwa kwao.
“Ni taarifa sahihi hizo. Kulikuwa na tuhuma katika ripoti ya ukaguzi,
kwa hiyo tumeamua wakae pembeni ili kupisha uchunguzi, hawajafukuzwa
kazi. Taarifa hiyo ya kusimamishwa ni sawa sawa,” alisema Profesa Wangwe
jana usiku.
Kwa mujibu wa taarifa kwa wafanyakazi, iliyotolewa na Ofisi ya
Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, iliwataja wakurugenzi sita waliosimamishwa kuwa
ni Yacob Kidula (Mkurugenzi wa Mipango, Uwekezaji na Miradi), Ludovick
Mrosso (Mkurugenzi wa Fedha) na Chiku Matessa (Mkurugenzi wa Rasilimali
Watu na Utawala).
Wengine ni Sadi Shemilwa (Mkurugenzi wa Udhibiti Hadhara na Majanga),
Pauline Mtunda (Mkurugenzi wa Ukaguzi wa Mahesabu ya Ndani) na
Crescentius Magori (Mkurugenzi wa Uendeshaji).
Aidha, taarifa hiyo iliwataja mameneja waliosimamishwa kuwa ni Amina
Abdallah (Meneja Utawala), Abdallah Mseli (Meneja wa Uwekezaji),
Mhandisi John Msemo (Meneja wa Miradi), Davis Kalanje (Mhasibu Mkuu),
Wakili Chedrik Komba (Meneja Kiongozi – Mkoa wa Temeke) na Mhandisi John
Ndazi (Meneja Mradi).
Taarifa hiyo kutoka Ofisi ya Mkurugenzi Mkuu wa NSSF, ilisema kwamba
uamuzi huo umefanywa na Bodi chini ya Profesa Wangwe iliyokutana Julai
15, mwaka huu kutokana na taarifa mbalimbali za wakaguzi wa hesabu na
shughuli za uendeshaji wa shirika hilo la umma.
“Bodi ya Wadhamini ya Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii chini ya
Uenyekiti wa Profesa Samwel Wangwe katika kikao chake cha 106
kilichofanyika tarehe 15 Julai, 2016 kimeagiza kusimamishwa kazi kwa
wakurugenzi sita (6), mameneja watano (5) na mhandisi mmoja ili kupisha
uchunguzi kubaini wahusika katika tuhuma za ubadhirifu, matumizi mabaya
ya ofisi na kutofuata kanuni, sheria na taratibu katika uwekezaji,
usimamizi wa miradi na manunuzi ya umma na ajira,” ilieleza taarifa
hiyo.
Hivi karibuni, NSSF ilitajwa katika vyombo vya habari kuhusu tuhuma
zikiwamo za ununuzi wa ardhi usiofuata taratibu za manunuzi ya umma,
kuwapo kwa ubadhirifu na ajira za upendeleo katika shirika hilo,
ukiwataja wahusika kuwa ni baadhi ya wakurugenzi wa shirika hilo.
CHANZO HABARI LEO
VIGOGO 12, NSSF WATUMBULIWA
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:35:00
Rating:
No comments: