‘Mkutano Mkuu wa CCM siyo wa kupokezana vijiti’
Msemaji wa Chama Ole Sendeka |
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimesema kwamba Mkutano Mkuu Maalumu wa
chama hicho, utakaofanyika mwishoni mwa wiki hii si wa kupokezana
vijiti, kwa sababu nafasi za Mwenyekiti na Makamu Mwenyekiti unapofika
wakati wa uchaguzi haziombwi, bali yanapendekezwa majina ya watu
wanaofaa kushika nyadhifa huo.
Aidha, kimesema maandalizi ya mkutano huo utakaofanyika Jumamosi wiki
hii, yamekamilika na unatarajiwa kushirikisha wajumbe 2,456 na mpaka
sasa wamekodi hoteli 306 ambazo zitawalaza zaidi ya watu 3,331 mjini
Dodoma.
Katika mkutano wake na waandishi wa habari jana, Msemaji wa CCM,
Christopher ole Sendeka alisema Mkutano Mkuu Maalumu wa Taifa utamchagua
Mwenyekiti wa CCM Taifa baada ya Mwenyekiti wa sasa, Jakaya Kikwete
kung’atuka na kutoa nafasi hiyo kwa Rais John Magufuli kugombea.
Alisema Rais Magufuli atakuwa Mwenyekiti wa CCM wa tano baada ya Baba
wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na
Kikwete.
“Kwa mujibu wa Katiba ya CCM, nafasi ya Mwenyekiti wa CCM na Makamu
Mwenyekiti wawili unapofikia wakati wa uchaguzi nafasi hizi haziombwi
isipokuwa Kamati Kuu inafikiria na kupendekeza majina na kuyawasilisha
kwa Halmashauri Kuu ya Taifa ambayo humteua,” alisema Sendeka.
Alisema kisha Mkutano Mkuu wa Taifa unamchagua kwa kumpigia kura.
Alisema wanaopendekezwa hawajazi fomu za kugombea nafasi hizo na katika
mchakato huo kinachofanyika si kupokezana kijiti, kama wengi
wanavyopenda kuita, bali ni uchaguzi wa kumpata mwenyekiti wa CCM.
Alisema katika uchaguzi huo itapigwa kura ya ‘ndio’ au ‘hapana’ ili
kupata mwenyekiti na lazima apate nusu ya kura na akipata chini ya nusu
mapendekezo yataanza upya.
“Tuna imani wajumbe wote watampa mwenyekiti mpya kura zote za ‘ndio’
ili achukue nafasi ya kuongoza kitaifa,” alisema na kuongeza kuwa
akipatikana mwenyekiti ataunda ‘jeshi’ lake, kwani hiyo ni desturi ya
chama na walio katika Sektetarieti, watapisha ili mwenyekiti mpya aunde
jeshi lake.
Rais Magufuli anatarajiwa kufanya mabadiliko makubwa ya uongozi ndani
ya CCM baada ya kukabidhiwa uenyekiti wa Taifa, kwa kupanga upya safu
yake ya viongozi, ambao anaamini anaweza kufanya kazi nao kwa ajili ya
kuleta mabadiliko ndani ya Chama.
Viongozi watakaojiuzulu ili kupisha Dk Magufuli kupanga safu hiyo ni
Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, manaibu katibu mkuu wawili na
watendaji wengine.
Wajumbe wa Sekretarieti ya Halmashauri Kuu ya Taifa ni pamoja na
Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu Bara, Naibu Katibu Mkuu Zanzibar, Katibu
wa Oganaizesheni, Katibu wa Siasa na Uhusiano ya Kimataifa, Katibu wa
Uchumi na Fedha na wa Itikadi na Uenezi.
“Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana atakabidhi barua yake kwa
mwenyekiti wa chama kupisha Rais Magufuli aweze kuunda safu yake ya watu
atakaofanya nao kazi,” alieleza Sendeka na kuongeza kuwa anaamini
Magufuli ataunda safu nzuri itakayoleta mabadiliko.
“Chama madhubuti huzaa serikali madhubuti na chama legelege huzaa
serikali legelege,” aliongeza na kubainisha kuwa maandalizi kwa ajili ya
mkutano huo, yamekamilika na tayari fedha zimetumwa mikoani ili
kuwezesha wajumbe wote kufika; na magari yatakodishwa kuwaleta mjini
hapa.
Alisema jumla ya wajumbe 2,456 watahudhuria mkutano huo, lakini pia
wanajitahidi kuweka hesabu vizuri kwa kuondoa wajumbe wenye kofia mbili.
Alisema wamekodi hoteli 306. Akizungumzia hali ya usalama alisema
wamejipanga kuhakikisha mkutano huo unafanyika kwa amani.
“Dodoma ni shwari na salama watu wasiwe na hofu na tuna imani mkutano
utamalizika vizuri,” alifafanua na kuongeza kuwa wajumbe wa NEC
watawasili Alhamisi tayari kwa kikao cha Ijumaa na wajumbe wengine
watawasili Ijumaa.
HABARI LEO
‘Mkutano Mkuu wa CCM siyo wa kupokezana vijiti’
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:41:00
Rating:
No comments: