Kodi kwa wateja wa benki yazuiwa
UPOTOSHAJI kuhusu makato ya Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) katika
miamala ya benki na simu za mikononi, uliochapishwa katika magazeti
baada ya kutangazwa na baadhi ya benki, umeilazimu Mamlaka ya Mapato
Tanzania (TRA) kuzuia benki hizo kutoza kodi kwa wateja wao.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Kamishna Mkuu
wa TRA, Alphayo Kidata, alihoji kwa nini mabenki yametoa matangazo ya
kuanza kutoza kodi hiyo, wakati hata kanuni za utekelezaji wa sheria
hiyo hazijatolewa.
Kidata alisema pamoja na kupitishwa kwa sheria hiyo bungeni, lakini
muongozo unaotokana na kanuni bado haujatolewa, ndio maana TRA
imeshindwa kuelewa kwanini taasisi hizo zimetoa taarifa zao kwa
wananchi.
Kutokana na hali hiyo ya kutoa matangazo ya kutekeleza sheria hiyo,
wakati kanuni za kutekeleza sheria yenyewe hazijatolewa, Kidata alisema
kumeonekana dalili za nia ovu.
“Tangu lini mmeona benki au taasisi ya fedha inaanza kutoa matangazo
ya utekelezaji wa sheria za serikali? Hii ni kwa sababu ya nia ovu.
“Kuna taarifa ambazo si za kweli zinazoenezwa kupitia mitandao ya
kijamii kuwa VAT itatozwa kwenye amana ya mwenye fedha kwenye benki. Hii
si kweli,” alisema Kidata.
Usahihi wa kodi
“Juzi Bunge la Tanzania lilipitisha marekebisho ya sheria hiyo ya
mwaka 2014 kuanzia Julai mosi mwaka huu kwenye huduma za kifedha kwa
kurekebisha kifungu cha 13 cha jedwali la msamaha wa kodi, lakini
taasisi hizo zimekuwa zikipotosha umma,” alisema.
Alisema kutokana na upotoshaji huo, TRA imeamua kueleza ukweli kuhusu
utekelezaji wa sheria hiyo, ili kuondoa utata na upotoshaji unaohusu
utekelezaji wa sheria hiyo.
Kidata alisema sheria hiyo inalenga kutoza VAT kwa kiwango cha
asilimia 18, kwenye ada ambazo benki zinatoza wateja wake katika huduma
mbalimbali zitolewazo na benki au taasisi za fedha.
“Ukweli ni kuwa kiasi cha VAT kitakachotozwa ni asilimia 18 ya kiasi
cha gharama ya huduma iliyotolewa na benki au taasisi yoyote ya fedha na
si kwa mteja,” alisema.
Akitolea mfano suala hilo, Kidata alisema kama ada ya huduma ya benki
ambayo mteja ametozwa ni Sh 1,000, VAT itakayotozwa kwenye kiasi hicho
ni Sh 152.50 tu na benki kubaki na Sh 847.50 na si kuwaongezea wananchi
mzigo.
“Kiwango hiki cha Sh 152.50 ndicho kitakachorejeshwa serikalini na
benki au taasisi ya fedha baada ya kupunguza VAT iliyolipwa kwenye
manunuzi ambayo yamefanywa kwa benki au taasisi ya fedha husika. Kwa
mujibu wa sheria hii, VAT haitatozwa kwenye riba inayotozwa na benki
kwenye mikopo,” alisema.
Alisema kuna maelezo yametolewa na moja ya benki hapa nchini kuwa
mtumiaji wa huduma za kifedha, atatakiwa kulipia kwa fedha taslimu kama
muamala husika haukupitia kwenye akaunti na kuongeza kuwa taarifa hiyo
siyo sahihi, kwa kuwa ukusanyaji wa VAT husika, utafanywa kwa njia ile
ile ambayo gharama za huduma za kifedha zinakusanywa sasa.
Kidata alisema TRA itatoa maelekezo ya namna utoaji wa risiti za
kielektroniki utakavyofanyika, ili kuwezesha mabenki au taasisi za
kifedha kutimiza matakwa ya kisheria ya VAT ya mwaka 2014 kama
ilivyorekebishwa mwaka 2016.
“Hivyo tunazitaka benki na taasisi za fedha zilizoamua kwa makusudi
kutoa taarifa zisizo sahihi kwa umma, kuacha mara moja vinginevyo hatua
kali za kisheria zitachukuliwa. “Kimsingi benki na taasisi za fedha
zinazohusika zinaagizwa kurekebisha mara moja taarifa
walizokwishazisambaza ili zibebe maudhui sahihi ya marekebisho ya sheria
hii,” alisema.
Barua BoT
Alisema katika hatua za awali, tayari wamewapa maelekezo Benki Kuu
(BoT) ambayo ni msimamizi wao mkuu, ihakikishe hicho kinachofanyika
kinasitishwa na hatua mbalimbali za kisheria zitachukuliwa.
“Mwanzo benki na taasisi hizo za fedha zilikuwa zikichukua tozo yote
wanayotoza, hivyo sasa tumewataka katika hiyo hiyo waliyokuwa
wakichukua, ndiyo watoe kodi na si kumuongezea mwananchi mzigo kwa
sababu kila kodi ina msingi wake na si kila kodi inapopanda, imlenge
mwananchi. Sisi tumelenga hiyo hiyo wanayotoza,” alisema.
Alitoa mwito kwa mtu yeyote mwenye uhakika kuwa ameongezewa makato na
benki au taasisi za fedha kwa madai ya utekelezaji wa sheria hiyo, atoe
taarifa ili hatua Alphayo Kidata zaidi za kisheria zichukuliwe.
Chanzo Habari Leo
Kodi kwa wateja wa benki yazuiwa
Reviewed by WANGOFIRA
on
21:37:00
Rating:
No comments: