Bwawa Nyumba ya Mungu Lafungwa kwa Miezi 12


SERIKALI za mikoa ya Kilimanjaro na Manyara zimelifunga Bwawa la Nyumba ya Mungu kwa kipindi cha mwaka mmoja ili kuepusha kutoweka kwa viumbe hai wakiwamo samaki kutokana na kushamiri kwa uvuvi haramu.

Aidha, wakuu wa wilaya za Moshi, Mwanga na Simanjiro wametakiwa kusimamia maamuzi hayo na kuchukua hatua kali za kisheria kwa watakaokaidi agizo hilo.

Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Said Mecky Sadiki alisema hayo wakati wa hafla maalumu ya kuwaapisha wakuu wapya wa wilaya mkoani Kilimanjaro iliyofanyika mjini Moshi, juzi.

Alisema uamuzi huo ulifikiwa katika kikao cha ujirani mwema baina ya mikoa hiyo kupitia wilaya tatu zinazolizunguka bwawa hilo na kwamba utekelezaji wa agizo hilo umeanza rasmi Julai Mosi mwaka huu.

“Hali ya uvuvi haramu katika Bwawa la Nyumba ya Mungu ni mbaya sana, mazingira yameharibiwa, kuna athari nyingi zinajitokeza ikiwamo ya kupungua kwa maji katika bwawa hilo na hii huenda ikaathiri uzalishaji umeme na kutoweka kwa viumbe hai....kama serikali hatuwezi kuvumilia tena,” alisema Sadiki.

Pamoja na bwawa hilo, Sadiki alitaka wakuu wa wilaya kusimamia agizo la Kamati ya Ushauri ya Mkoa (RCC), kupiga marufuku misumeno ya mnyororo, kwani imebaini ni adui mkubwa wa misitu.

Katika hatua nyingine, Mkuu huyo wa Mkoa aliwakabidhi wakuu hao wa wilaya migogoro mikubwa mitano iliyopo katika hatua mbalimbali za utatuzi wake kupitia viongozi waliowatangulia na kutaka kufuata sheria katika kuishughulikia.

Miongoni mwa migogoro aliyoitaja ni unaohusisha jamii ya wafugaji wanaozunguka Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) na kampuni inayohudumia uwanja huo ya KADCO kuhusu umiliki wa eneo la ardhi.

Mgogoro mwingine ni wananchi wa wilaya ya Longido mkoani Arusha na mwekezaji wa eneo la utalii la Ndarakwai uliowahi kusababisha kuchomwa moto kwa eneo hilo.
Bwawa Nyumba ya Mungu Lafungwa kwa Miezi 12 Bwawa Nyumba ya Mungu Lafungwa kwa Miezi 12 Reviewed by WANGOFIRA on 21:45:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.