Alichokisema Rais Magufuli Baada ya Kuchaguliwa Kuwa Mwenyekiti wa CCM

MWENYEKITI wa tano wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais John Magufuli, amewaomba wanachama wa chama hicho kumuombea kwa Mungu ili apate uvumilivu wa mtangulizi wake, Mwenyekiti mstaafu, Jakaya Kikwete.

“Mzee Kikwete wewe una moyo wa uvumilivu. Sina hakika kama mimi ninao uvumilivu kama wako...umetupa fundisho kubwa sana,” alisema Magufuli wakati akizungumza kwa mara ya kwanza baada ya kuchaguliwa kwa kura asilimia 100 kuwa Mwenyekiti wa chama hicho.

Katika kuonesha tofauti yake na Kikwete katika uvumilivu, Magufuli alikumbusha changamoto aliyokutana nayo Kikwete, wakati alipoingia katika kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya CCM mwaka jana, kupeleka mapendekezo ya majina ya wagombea watano wa urais waliokuwa wamepitishwa na kikao cha Kamati Kuu, ili wapigiwe kura.

Ndani ya kikao hicho wakati Kikwete, wajumbe wa Kamati Kuu na wa Baraza la Wazee la Ushauri wakiingia, baadhi ya wajumbe wa kikao hicho walikiuka utaratibu wa siku zote wa chama hicho, kwa kuimba kuwa na imani na mmoja wa wagombea wa urais, Edward Lowassa, ambaye jina lake lilikatwa katika kikao cha Kamati Kuu.

Kupotezwa  
“Siku ile umeingia ukumbini, watu wakawa wanaimba kuwa wana imani na mtu mwingine, siku hiyo hiyo robo au nusu yao wangepotea...sifahamu, umetoa fundisho kwa sisi vijana kwamba saa nyingine uvumilivu ni kitu muhimu,” alisema akimaanisha kama hali hiyo ingemkuta yeye ndiye Mwenyekiti, hayo ndiyo yangetokea.

Kutokana na uvumilivu aliouonesha Kikwete katika mkutano huo, Magufuli aliwataka wanachama hao wa CCM kumuombea kwa Mungu, ili apate angalau nusu ya uvumilivu wa Kikwete, ili katika uongozi wake mambo yaende salama.

Kuzushiwa JK
Alimsifu Kikwete kwa kutumia hekima ya uvumilivu, kwa kuwa kiongozi huyo mstaafu, amesemwa mambo mengi, akazushiwa na hata kutukanwa kutokana na hatua, uamuzi na vitendo vyake Magufuli.

“Umesemwa mengi, umetukanwa mengi na umezushiwa mengi kwa ajili yangu, lakini kwa upendo wako na kwa kumtegemea Mungu, ukakaa kimya...sina cha kukulipa, bali nitafanyia kazi Watanzania na hasa wana CCM kwa nguvu zote,” alisema Dk Magufuli.

Alitoa mfano wa Kikwete kuzushiwa alikuwa akikataa kumkabidhi Dk Magufuli uenyekiti wa CCM kwa kufuata desturi ya chama hicho, akasema Mwenyekiti huyo mstaafu amemshawishi mara nne, lakini yeye ndiye aliyekuwa akikataa.

“Nakumbuka umeniambia mara nne, ya kwanza ulikuja kuniambia nikakukatalia bosi wangu, ulinipigia simu na mimi nikawa naanzisha mjadala mwingine. Nakupa pole na unisamehe sana kwa kuwa kukukatalia kulisababisha utukanwe,” alisema Rais Magufuli.

Serikali Dodoma
Kabla ya kumaliza hotuba yake, Magufuli alitangaza ahadi kwa wanachama hao, kuwa amebakiza miezi minne na miaka minne kabla ya kumaliza kipindi chake cha miaka mitano na kusema kabla ya kumaliza kipindi hicho, atakuwa amehamishia serikali yote Dodoma.

Magufuli alisema kwa sasa miundombinu ya Dodoma inawezesha serikali kuhamia huko, kwa kuwa barabara za kutoka Makao Makuu hayo ya serikali kwenda sehemu mbalimbali nchini, zinapitika kwa lami.

Mbali na barabara, alisema pia huduma kwa ajili ya maisha ya watu nazo zinapatikana kwa kuwa mkoa huo una uzoefu wa kuhudumia wabunge, wajumbe wa Mkutano Mkuu wa CCM na mikutano mingine, huku mkoa huo ukiwa na Chuo Kikuu cha Dodoma, ambacho ndio kikubwa kuliko vyote nchini.

Alisema, akihamia yeye katika Ikulu ya Chamwino ambayo alisema ina kila huduma anayohitaji, anatarajia Makamu wa Rais, Waziri Mkuu, mawaziri na serikali nzima itamfuata.

Babu wa demokrasia
Magufuli alisema CCM ndio chama kilicholea demokrasia hapa nchini na kinaendelea kutoa ulezi huo na kufafanua kuwa chama hicho ndio babu na bibi wa demokrasia; baba na mama wa demokrasia na kaka na dada wa demokrasia kwa vyama vyote nchini.

Alisema kwa kuwa Serikali anayoiongoza inatekeleza Ilani ya chama hicho, hivyo chama hicho ndio mabosi wa mabosi wote serikalini na kuonya kuwa ambaye hataki hilo, ataondolewa.

Kupendekezwa kwake
Awali wajumbe wa Mkutano huo Mkuu Maalumu wa CCM wapatao 2,398 walimpigia kura ya kumchagua Magufuli kuwa Mwenyekiti mpya wa chama hicho.

Mwenyekiti aliyemaliza muda wake, Kikwete ndiye aliyesoma pendekezo la NEC kwa wajumbe wa mkutano huo kuhusu mgombea wa nafasi hiyo.

“Madhumuni ya mkutano huu ni kuchagua mwenyekiti mpya. Sisi katika Halmashauri Kuu tunampendekeza kwenu Mheshimiwa Dakta John Pombe Joseph Magufuli ashike nafasi hiyo,” alisema Kikwete saa 7:10 na kauli yake hiyo kupokelewa kwa shangwe, vifijo na vigelegele.

Akimwelezea Magufuli, Kikwete alisema ana imani isiyo na hata chembe ya shaka kuwa atafanya kazi hiyo vizuri, kwa sababu ya imani na mapenzi yake makubwa kwa chama hicho na Watanzania.

Alisema Magufuli ametumikia Taifa na wananchi kwa miaka mingi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa, katika wadhifa mbalimbali aliokuwa nao. Alisema Magufuli amekuwa mbunge na waziri kwa miaka 20, ambapo miaka 10 wakati wa serikali ya Rais Benjamin Mkapa na mingine 10 wakati wa serikali yake.

Alisema pia Magufuli amekuwa mjumbe wa kamati ya siasa ya wilaya na mkoa, mjumbe wa mkutano mkuu wa wilaya na mkoa na mjumbe wa mkutano mkuu wa taifa kwa miaka 20, hivyo anakijua mno chama.

Kikwete alisema Magufuli ameongoza nchi kwa uaminifu na uadilifu mkubwa katika kipindi kifupi cha miezi 8 tangu alipochaguliwa, hivyo sasa anafaa kuvaa kofia zote mbili.

“Kichwa chake sasa kinatosha avae kofia zote mbili - ya urais na uenyekiti wa chama. Nawaomba wajumbe wote tumuunge mkono. 

“Tumpe kura zote za ‘Ndiyo’ na isipotee hata moja,” alisema Kikwete ambaye ameng’atuka baada ya kuongoza Chama tangu Juni 2006. 

“Mimi naondoka na bila shaka yoyote namwachia Chama Cha Mapinduzi Rais Dakta John Pombe Joseph Magufuli. Nakiacha Chama Cha Mapinduzi katika mikono salama na nina hakika kitapata maendeleo makubwa ya haraka,” alisema.

Kura zatangazwa
Kazi ya kupiga kura na kuzihesabu ilipokuwa ikiendelea, viongozi wakuu wa CCM na wastaafu baada ya baadhi yao kupiga kura, waliondoka kwa ajili ya mapumziko.

Baada ya mapumziko, walirejea ambapo baada ya salamu za wageni na baadhi ya wanasiasa waliorejea CCM baada ya kukimbilia upinzani kumalizika, Kikwete alisoma matokeo.

Akitangaza matokeo hayo, Kikwete alisema kura zilizopigwa zilikuwa 2,398, zilizoharibika sifuri na hivyo kura halali zikawa 2,398. 

Kikwete aliendelea kuwa matokeo yameonesha kuwa, kura za Hapana ni sifuri na kura za ndio ni 2,398, na hivyo Magufuli amepitishwa na wajumbe wa CCM kwa nidhamu ya juu ya kumpa asilimia 100 ya kura.

Makamu wenyeviti
Awali, Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana alisema mkutano mkuu huo usio wa kawaida, unafanyika kwa mujibu wa Kifungu cha 7 (103) (4) cha Katiba ya CCM na ajenda yake ni kumchagua mwenyekiti mpya, kufuatia uamuzi wa Kikwete kung’atuka, akitekeleza utamaduni wa chama kuachiana madaraka, ili kumpisha Rais John Magufuli.

Aidha, alisema kwa mujibu wa Kifungu 7 (105) (5) (a) cha Katiba hiyo, unapofika wakati wa uchaguzi kazi mojawapo ya mkutano mkuu ni kuchagua makamu wenyeviti. 

Lakini, alisisitiza makamu wote wawili wa sasa, muda wao haujamalizika kikatiba na utamalizika mwezi Novemba 2017 “Makamu wote wawili hawajamaliza muda wao. Muda wao utamalizika Novemba 2017, hivyo hakuna sababu ya kuwachagua tena. Hapa leo tunachagua mwenyekiti peke yake,” alitangaza Kinana.

Makamu Mwenyekiti wa CCM kwa upande wa Bara ni Phillip Mangula na upande wa Zanzibar ni Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein.

Viongozi wengine waliohudhuria mkutano huo ni pamoja na marais wastaafu, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa, Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan, Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, Rais wa Zanzibar Dk Shein , mawaziri wakuu wastaafu Mizengo Pinda, Cleopa Msuya, Dk Salim Ahmed Salim, Jaji Joseph Warioba, John Malecela, Makamu wa Rais mstaafu Mohamed Gharib Bilal na makatibu wakuu wastaafu wa CCM, Yusuf Makamba na Wilson Mukama.
Alichokisema Rais Magufuli Baada ya Kuchaguliwa Kuwa Mwenyekiti wa CCM Alichokisema Rais Magufuli Baada ya Kuchaguliwa Kuwa Mwenyekiti wa CCM Reviewed by WANGOFIRA on 20:32:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.