Waliofukuzwa Chuo Kikuu cha St. Joseph Wafungua Kesi Mahakamani


MAHAKAMA Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imetoa kibali cha kufungua kesi ya uwakilishi, kwa wanafunzi wanne, waliofukuzwa katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Joseph kwa madai ya kutokuwa na sifa za kudahiliwa kwenye vyuo vikuu.

Jaji Eliezer Feleshi alitoa kibali hicho baada ya wanafunzi hao kuwasilisha maombi ya kibali cha kuwakilisha wenzao mahakamani pamoja na kusitisha masomo wakati kesi ya msingi ikiendelea kusikilizwa.

Wanafunzi hao, walisimamishwa masomo baada ya kutolewa amri ya Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Joyce Ndalichako kwamba kutokana na tatizo la ufundishaji wa Stashahada ya Elimu (Sayansi, Hisabati na Teknolojia) wanafunzi wote wanatakiwa kurejea nyumbani.

Akiwasilisha maombi ya wanafunzi hao, Wakili Emmanuel Muga aliomba wanafunzi 316 waliofukuzwa chuo, wapewe kibali cha kufungua kesi ya uwakilishi pia Mahakama itoe amri ya kusitisha masomo wakati wa usikilizwaji wa kesi.

Akitoa uamuzi, Jaji Feleshi alisema Mahakama imekubali ombi hilo, isipokuwa la kusimamishwa masomo wanafunzi wote na kufafanua kuwa “masomo yataendelea kusimama kwa wanafunzi 316 waliosimamishwa”.

Aidha alisema wanafunzi hao wanatakiwa kuwa na wawakilishi wanne tu, badala ya 316, kwa sababu idadi yao ni kubwa. Baada ya uamuzi huo, Wakili Muga aliwataja wanafunzi wanne watakaowawakilisha wenzao mahakamani hapo kuwa ni Innocent Peter, Ramadhan Kipenya, Oswald Mwinuka na Faith Kyando.

Jaji Feleshi alisema Mahakama imetoa kibali na itapanga tarehe ya kusikilizwa kwa kesi baada ya walalamikaji hao kufungua kesi yao. 

Katika madai yao, wanafunzi hao wanadai fidia ya miaka mitatu waliyokaa chuoni hapo dhidi ya Tume ya Vyuo Vikuu (TCU) iliyowakilishwa na Wakili Rose Lwita na Judith Misokia na Chuo cha Mtakatifu Joseph, kikiwakilishwa na wakili Jeromah Msemwa.
Waliofukuzwa Chuo Kikuu cha St. Joseph Wafungua Kesi Mahakamani Waliofukuzwa Chuo Kikuu cha St. Joseph Wafungua Kesi Mahakamani Reviewed by WANGOFIRA on 20:42:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.