Kiswahili kinazidi kupasua anga


Image result for KISWAHILI 

TANZANIA inatarajiwa kuanza kutumia Kiswahili katika mikutano yote ya kimataifa itakayowakilishwa na viongozi wake baada ya serikali kukamilisha kutuma wataalamu watakaotafsiri lugha hiyo kwa watumiaji wa lugha nyingine duniani.

Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameyasema hayo bungeni mjini Dodoma katika kipindi cha maswali ya papo kwa hapo kwa Waziri Mkuu. Kauli ya Majaliwa ni jibu kwa swali la Mbunge wa Viti Maalumu, Zainabu Vulu (CCM) aliyehoji namna serikali inavyoenzi lugha ya Kiswahili aliyoitumia Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere kuunganisha taifa. Majaliwa anasema, vyuo vikuu duniani kote vimeanza kufundisha Kiswahili hivyo kuongeza mahitaji ya walimu wa kufundisha lugha hiyo kutoka Tanzania.

Anasema, vyuo vikuu nchini vinafundisha walimu wa lugha hiyo kukidhi mahitaji kwenye soko la kimataifa, lakini pia serikali inajiandaa kupeleka nje wataalamu wa kutafsiri Kiswahili. Chama cha Wafanyakazi wa Taasisi za Elimu ya Juu Tanzania (THTU), Tawi la Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kimempongeza Waziri Mkuu kwa tamko hilo la Juni 16 mwaka huu. Kinaishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa juhudi za kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili kwa kuwa ni tunu ya taifa.

Kinasema, tamko la kutumia Kiswahili kuwa lugha kuu ya mawasiliano katika ofisi za serikali na vikao vya ndani n a v y a kimataifa ni jambo jema. T H T U inaipongeza serikali kwa kuboresha utumishi wa umma, kudhibiti watumishi hewa serikalini na kusitisha ajira kwa muda ili kuboresha mchakato wa ajira nchini. Kinasema, juhudi za serikali zitawezesha kufahamu idadi ya watumishi hivyo kuwa rahisi kuboresha maslahi na wakati huohuo ikiongeza ajira kwa kukuza Kiswahili kuongeza pato la taifa.
 
Mwenyekiti THTU Mlimani, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Salifius Mligo anasema wameona lugha ya Kiswahili inavyozidi kukua kwa kasi barani Afrika, Afrika Mashariki na nje ya Bara la Afrika. Anatoa mfano wa Bunge la Afrika kuwa linatumia lugha ya Kiswahili. Anasema lugha hiyo inafundishwa katika vyuo na shule za serikali na watu binafsi katika nchi kadhaa ikiwemo Ghana, Libya, Zimbabwe, Namibia, Misri, Aljeria, Afrika Kusini, Kenya, Uganda, Burundi na Rwanda. Bara la Asia ni China, Japan, Korea Kusini na India.

Ulaya ni Ujerumani, Italia, Uholanzi, Uingereza, Sweden, Ufaransa na Austria. Kwa Amerika ya Kaskazini ni Marekani na Canada. Amerika ya Kusini ni Mexico na Jamaika, na Australia ni katika miji ya Melbourne, Sydney na Adelaide. Mligo anasema, lugha ya Kiswahili inatumika kama lugha ya mawasiliano na biashara katika nchi za DRC, Namibia, Afrika Kusini, Zimbabwe, Malawi, Msumbiji, Comoro, Zambia, Madagaska, Oman na nchi zote za Afrika Mashariki.

Anasema juhudi za serikali haziishi katika kukuza lugha tu bali pia kuitangaza Tanzania kimataifa na kukuza biashara. “Ni juhudi zinazoijengea lugha ya Kiswahili heshima inayostahili. Aidha kwa hapa Tanzania Kiswahili kimekuwa lugha ya taifa,” anasema Mligo. Anasema, kiongozi wa k i t a i f a anapokuwa ndani au nje ya nchi hana budi kulitangaza taifa lake na kujivunia. Kwa mujibu wa Mligo, viongozi wakizungumza Kiswahili inadhihirisha uhuru walionao na kutangaza wazi sera ya kujitegemea kwa nchi yetu.

Kiswahili ni lugha ya kibantu na ni lugha ya Kiafrika. Kwa kuijenga na kuiendeleza serikali pia inajenga umoja na mshikamano wa Waafrika kwa kutumia lugha ya Kiafrika. “Jambo hili linaungwa mkono na azma waliyokuwa nayo waasisi wa mataifa ya Kiafrika, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere, Kwame Nkrumah, Kenneth Kaunda na wale walioko sasa hivi kama vile Robert Mugabe katika kuijenga Afrika Moja,” anasema.

Anaiomba serikali iendelee na utekelezaji wa suala hilo kwa kusimamia na kutoa maagizo na kuhakikisha yanatekelezwa. Anasema serikali inatakiwa kutoa waraka maalumu wa kurasimisha matumizi rasmi ya Kiswahili katika taasisi zote za umma kutumia Kiswahili katika mawasiliano yote na kuacha matumizi ya Kiingereza. Mligo anasema, katika maazimio hayo, watumishi wote wanaokwenda kuwakilisha serikali ya Tanzania nchi za nje wakipewa ruhusa lazima wapewe pia waraka rasmi wa kutumia na kukitangaza Kiswahili huko waendako.

Wachezaji mpira, wasanii na wanamichezo wanaporuhusiwa kwenda nje ya nchi kuiwakilisha Tanzania, wapewe bendera na waraka wa kutumia Kiswahili kuitangaza nchi yetu. “Mheshimiwa Waziri Mkuu tamko lako bungeni limekuja katika wakati muafaka ambao tunazungumzia umoja wa nchi za Afrika na dunia. “Ni imani yetu kwamba lugha ya Kiswahili ikizungumzwa ipasavyo itakuwa ni kiungo kikubwa sana cha watu duniani. Na hii itasaidia sana kuinua uchumi wa Watanzania na Afrika kwa ujumla,” anasema Mligo.

Anasema, wana imani na utendaji wa serikali hivyo katika maboresho yanayofanywa kwenye utumishi wa umma, matumizi ya Kiswahili yawe ni sehemu ya mikakati itakayotekelezwa. Profesa kutoka Taasisi ya Taaluma za Kiswahili katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Aldin Mutembei anasema chuo hicho kilianza kufundisha Kiswahili mwaka 1930. Anasema mwaka 2009/10 kilianza kufundisha shahada ya kwanza ya Kiswahili na kuendelea na shahada ya pili.

“Sisi tulianza mapema kabla ya wenzetu lakini tulichelewa kuanza kutoa shahada,” anasema Mutembei. Anasema, walimu wengi kutoka UDSM wamepelekwa nje ya nchi kufundisha lugha ya Kiswahili. Kuna taarifa kwamba, kuanzia Julai mwaka huu, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kitaanza kutumia lugha ya Kiswahili kuwasiliana katika vikao vyote isipokuwa kufundishia darasani.

Machi mwaka huu, Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Anastazia Wambura amewataka watendaji wa Baraza la Kiswahili la Taifa (Bakita), kujitangaza na kushiriki katika matukio ya kitaifa na kimataifa kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kiswahili ili kiweze kufahamika na kutumika na mataifa mengine. Katibu Mtendaji wa Bakita, Dk Selemani Sewange anasema baraza hilo limekuwa likishiriki katika Bunge la Afrika na Umoja wa Afrika hivyo kutangaza lugha ya Kiswahili.

Serikali imekusudia kupeleka wataalamu wa Kiswahili katika nchi mbalimbali ili kuwezesha viongozi kutoka Tanzania wanapokwenda katika mikutano ya kimataifa, watumie Kiswahili na wataalamu hao watoe tafsiri kwenda kwenye lugha nyingine za kimataifa. Tanzania imepeleka walimu wa Kiswahili nchini Burundi, Rwanda, Uingereza na Ufaransa ambako wanafundisha lugha hiyo. Kati ya lugha kubwa za kimataifa, Kiswahili kama si lugha ya sita ni ya nane.

Imeandaliwa na Lucy Ngowi.
Kiswahili kinazidi kupasua anga Kiswahili kinazidi kupasua anga Reviewed by WANGOFIRA on 20:47:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.