Shule Kongwe 88 Kufanyiwa Ukarabati
SERIKALI
ya Awamu ya Tano imetenga Sh bilioni 33 kwa ajili ya mpango maalumu wa
ukarabati mkubwa na uboreshaji wa miundombinu mbalimbali, yakiwemo
majengo ya madarasa, mabweni na nyumba za walimu katika shule kongwe za
sekondari za serikali nchini.
Waziri
wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako,
alisema hayo wakati wa uzinduzi rasmi wa mpango huo katika Shule ya
Sekondari ya Mzumbe iliyopo Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro.
Profesa
Ndalichako alisema mpango huo wa miaka miwili utahusisha shule kongwe
88 za serikali kwa kufanyiwa ukarabati mkubwa wa miundombinu, majengo ya
madarasa, nyumba za walimu, mabweni, majengo ya chakula na uboreshaji
wa maabara na vitendea kazi vyake.
Waziri
huyo alikuwa pia mgeni rasmi kwenye maadhimisho ya Siku ya Elimu
Tanzania iliyofanyika juzi kwenye Ukumbi wa Shule ya Sekondari Mzumbe na
kuhudhuriwa na wadau wa sekta ya elimu wakiwemo wakuu wa shule za
sekondari za serikali na maofisa elimu wa mikoa kutoka mikoa yote ya
Tanzania Bara.
Alisema
utekelezaji wa mpango huo unatarajia kuanza wakati wotote baada ya
kupitishwa kwa Bajeti ya Serikali na kuanza kutumika na utaanza kwa
awamu ya kwanza ambako shule kongwe 33 zitahusika.
“Tumekadiriwa
kuwa kila shule itagharimu shilingi bilioni moja na kwa maana hiyo
shule 33 zimeingizwa awamu ya kwanza. Fedha hiyo inaweza ikapungua
kulingana na mazingira ya kitadhimini ya uchakavu wa majengo,” alisema Profesa Ndalichako.
Alisema
uboreshaji wa elimu ni pamoja na ubora wa majengo na miundombinu
mingine katika shule hizo, na lengo la kuzirejesha katika uhalisia wake
wa zamani wa kuwa na mandhari nzuri za kuvutia wanafunzi, walimu na
wazazi.
“Shule
hizi tumeziweka katika mpango maalumu wa miaka miwili kukarabatiwa
majengo yake, miundombinu ya kufundishia, vifaa vya kila somo, vitabu
vya kufundishia na kujifunzia, vifaa vya kutosha vya maabara na
kuboresha makazi ya walimu,” alifafanua Profesa Ndalichako.
Naye
Mkurugenzi wa Usimamizi wa Elimu Ofisi ya Rais Tamisemi, Juma Kaponda,
alimpongeza Waziri Ndalichako kwa kusimamia uboreshaji wa shule kongwe
za sekondari na kuomba wadau mbalimbali waliosoma shule kongwe hizo na
wanazo nyadhifa kubwa serikalini na sekta binafsi kuona wanao wajibu wa
kuchangia maboresho hayo.
Shule Kongwe 88 Kufanyiwa Ukarabati
Reviewed by WANGOFIRA
on
23:02:00
Rating:
No comments: