Shirika la AGPAHI Lazindua Kambi ya Watoto na Vijana Mkoani Kilimanjaro

Watoto na vijana 50  kutoka mikoa ya Shinyanga na Simiyu wameweka kambi ya siku tano mkoani Kilimanjaro ili kupatiwa maarifa mbalimbali yatakayowawezesha kukua na kuishi katika matumaini chanya,Mwandishi wetu Kadama Malunde,anaripoti zaidi.

Kambi hiyo inayoitwa Kambi ya Ariel ni ya sita kufanyika tangu shirika la  Ariel Glaser Pediatric Aids Healthcare Initiative (AGPAHI)  linalojihusisha na mapambano dhidi ya Virusi vya Ukimwi (VVU) na Ukimwi katika mikoa ya Shinyanga,Simiyu na Geita lilipoanzishwa mwaka 2011.

Kambi hiyo imeanza siku ya Jumatatu,Juni 13,2016 katika hoteli ya Lutheran Uhuru mjini Moshi mkoani Kilimanjaro, ambapo maafisa kutoka AGPAHI ,madaktari bingwa wa watoto,wataalaamu wa masuala ya kisaikolojia,wasimamizi wa watoto kutoka vituo vya afya na baadhi ya waandishi wa habari walihudhuria. 


Akifungua kambi hiyo, Mkurugenzi wa miradi wa shirika la AGPAHI Tanzania, Dr. Amos Nsheha alisema malengo ya kambi hiyo ni kuwakutanisha watoto na vijana  wenye umri kati ya miaka 12 mpaka 19 ili kuwafundisha namna ya kuwa wafuasi wazuri wa dawa na kujifunza kuhusu masuala ya ujana na VVU.

Aliyataja malengo mengine kuwa ni kuwafundisha namna ya kukabiliana na msukumo rika,stadi za maisha,namna ya kuzuia maambukizi ya VVU kwa watu wengine,kubadilishana uzoefu na kufanya utalii wa ndani.
“Hii ni kambi ya 6,tumewahi kufanya kambi kama hii mkoani Kilimanjaro,Mwanza na Kagera.Katika kambi hizi 6 tumefanikiwa kuwaita vijana wanaoishi na VVU takribani 300.Vijana wanaohudhuria kambi huchaguliwa kutoka kwenye vilabu vilivyoanzishwa kwenye mikoa tunakofanya shughuli zetu, na mpaka sasa tuna vilabu 50 vya watoto na vijana wenye umri kati ya miaka 6 hadi 19 na kwenye vilabu hivyo tuna watoto na vijana takribani 2500”,alieleza Dr.Nsheha.
“AGPAHI ni asasi ya kitaifa isiyo ya kiserikali iliyosajiliwa mwaka 2011 kwa msaada wa Elizabeth Glaser Pediatric Aids Foundation (EGPAF) kwa lengo la kutokomeza Ukimwi kwa watoto nchini Tanzania,tukiwa na lengo la kuwajali watoto wakue na kuishi kwenye matumaini chanya”,alieleza Dr. Nsheha.
Akielezea historia ya jina la Shirika, Dr. Nsheha alisema,AGPAHI ilipewa kwa heshima jina la Ariel Glaser, msichana aliyefariki kwa Ukimwi mwaka 1988 akiwa na umri wa miaka 8. Ariel aliambukizwa virusi vya Ukimwi na mama yake Elizabeth Glaser (mwanaharakati wa Ukimwi kwa watoto wachanga),aliyepata VVU baada ya kuongezewa damu wakati akijifungua na bila kujua alimwambukiza binti yake Ariel wakati wa kumnyonyesha.
“Miongoni mwa kazi tunazofanya ni kupambana ili kuzuia maambukizi kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto na kutoa tiba kwa wale ambao tayari wanaishi na VVU/Ukimwi pamoja na wazazi na familia kwa ujumla”, alieleza Dr. Nsheha.
“AGPAHI imekuwa ikitekeleza miradi minne katika mikoa hii,ambayo ni kutoa huduma za tiba na matunzo kwa watu wanaoishi na VVU,kutoa huduma ya kuzuia maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto,kutoa huduma ya uchunguzi wa awali na tiba ya saratani ya shingo ya kizazi na kutoa huduma za afya ya uzazi na uzazi wa mpango hasa kwa wagonjwa wanaoishi na VVU”, alieleza Dr. Nsheha.
Alisema hadi kufikia mwezi Desemba mwaka 2015, AGPAHI imefanikiwa kupata watu wanaoishi na VVU takribani 150,000 waliokuwa kwenye huduma ya matunzo ,ambapo kati yao watoto wenye umri chini ya miaka 15 walikuwa takribani 9000, waliokuwa kwenye dawa kati ya watu 150,000 ni wagonjwa  58,000 tangu kuanza kwa mradi wa tiba na matunzo kati yao wanaoendelea kutumia dawa ni takribani 49,000.
“Lengo ni kuwafikia watu 110,000 kwenye matibabu,bado tuna jukumu kubwa la kuwabaini watu walio na maambukizi ya VVU hasa watoto ,kwani ndiyo kipaumbele chetu.Katika jitihada zetu tunajitahidi watoto waliozaliwa na mama wenye VVU ,waweze kuishi maisha yao yote ili kufanikisha ndoto zao za kimaisha na wawe na matumaini chanya”,alisema Dr. Nsheha.
Tangu kuanzishwa kwake,AGPAHI inafanya kazi zake katika mikoa ya Shinyanga,Simiyu na Geita kwa kuunga mkono utoaji huduma kamilifu za VVU/Ukimwi ikishirikiana na halmashauri 14 za wilaya pamoja na hospitali,zahanati na vituo vya afya vya serikali na taasisi mbalimbali zikiwemo za kidini.
AGPAHI inatekeleza majukumu yake kwa hisani ya watu wa Marekani kupitia Centres for Disease Control and Preventation (CDC),shirika la misaada la Marekani(USAID) chini ya mpango wa dharura wa rais wa Marekani dhidi ya Ukimwi (PEPFAR), Mfuko wa idadi ya watu duniani (UNFPA) na mfuko wa kusaidia Watoto wenye VVU Kwa hisani ya watu wa Uingereza (CIFF).
Miongoni mwa malengo ya AGPAHI ni kuboresha afya ya watoto na familia kwa kutokomeza VVU/Ukimwi kwa kujengea uwezo,utetezi,huduma za kinga na tiba kwa kushirikiana na wadau mbalimbali ili kubuni na kutekeleza mikakati muafaka kwa afya bora.
Angalia picha na matukio yaliyojiri katika Kambi ya Watoto na Vijana siku ya kwanza.
Mkurugenzi wa miradi ya shirika la AGPAHI Tanzania, Dr. Amos Nsheha akitoa hotuba ya ufunguzi wa Kambi ya Watoto na Vijana 
Baadhi ya watoto kutoka mikoa ya Shinyanga Simiyu wakifuatilia kilichokuwa kinaendelea katika ukumbi wa mkutano
Meneja Mawasiliano na Huduma za Jamii kutoka AGPAHI, Jane Shuma akitambulisha na kuwakaribisha wageni na washiriki wa kambi.
Watoto na vijana wakiwa ukumbini
Afisa miradi huduma unganishi kwa jamii kutoka AGPAHI, Cecilia Yona akizungumza ukumbini
Afisa miradi huduma unganishi kwa jamii AGPAHI, Richard Kambarangwe akisisitiza jambo 
Daktari Bingwa wa Watoto, Dr.Rose Mende kutoka hospitali ya rufaa ya Mkoa wa Arusha,Mount Meru akitoa maelezo kuhusu huduma za uchunguzi na matibabu kwa watoto na vijana wakiwa kambini
Mmoja wa watoto akionesha kipaji chake cha kuimba
Watoto na vijana wakiimba wimbo wa pamoja ukumbini
Mshauri wa Masuala ya Kisaikolojia,Sherida Madanka kutoka Hospitali ya rufaa ya mkoa wa Shinyanga akitoa mada kuhusu stadi za maisha na mabadiliko ya tabia kutokana na msukumo rika.
Kijana akichangia mada ukumbini
Kijana akiwasilisha kazi kwa niaba ya kikundi
Vijana wakitoa elimu kupitia igizo
Vijana wakifurahia uwepo wao kambini 
Vijana wakicheza pamoja kambini

Vijana wakionesha mshikamano
Picha ya pamoja ya washiriki wa kambi 

Shirika la AGPAHI Lazindua Kambi ya Watoto na Vijana Mkoani Kilimanjaro Shirika la AGPAHI Lazindua Kambi ya Watoto na Vijana Mkoani Kilimanjaro Reviewed by WANGOFIRA on 20:05:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.