Serikali kutekeleza miradi mikubwa 4 ya kielelezo

MPANGO wa Maendeleo wa Mwaka wa kwanza wa Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Rais John Magufuli, umekuja na miradi mikubwa minne ya kielelezo, itakayotekelezwa kwa kutumia sehemu kubwa ya Sh trilioni 11.8 zilizotengwa kwa maendeleo, ambazo ni sawa na asilimia 40 ya Bajeti yote ya Serikali kwa mwaka wa fedha 2016/2017.
Reli ya kisasa ya kiwango cha geji.
Kwa kuonesha dhamira ya serikali katika utekelezaji wa miradi hiyo, asilimia 74 ya fedha zilizotengwa kwa ajili ya maendeleo itakuwa makusanyo ya ndani ya serikali na asilimia 26 tu ndio mapato ya nje. Akisoma Taarifa ya Hali ya Uchumi kwa Mwaka 2015 na Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2016/2017 bungeni jana, Waziri wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango (pichani) alitaja miradi hiyo ambayo baadhi Rais Magufuli alishaizungumzia katika baadhi ya hotuba zake.
“Kwa maana ya kipekee, Mpango wa Maendeleo wa Taifa wa Mwaka 2016/17, umeainisha miradi mikubwa ya kielelezo, ambayo itapewa msisitizo katika utekelezaji wake,” alisema Dk Mpango. Mradi wa kwanza wa maendeleo katika kundi hilo la miradi minne mikubwa ya kielelezo ni ujenzi wa reli ya kisasa (standard gauge) ambao Rais Magufuli aliahidi kutenga Sh trilioni moja ya kuanza ujenzi wakati wakitafuta fedha za kuendeleza ujenzi wake.


Reli hiyo itaanzia Dar es Salaam kwenda Kigoma na Tabora mpaka Mwanza na itakuwa na matawi ya kutoka Isaka hadi Kigali/Keza na Msongati hadi Kaliua- Mpanda. Aprili mwaka huu, wakati Balozi wa China nchini, Dk Lu Youqing alipokwenda Ikulu, Rais Magufuli alimweleza kuwa Tanzania imedhamiria kuanza ujenzi wa reli hiyo haraka iwezekanavyo na tayari imetenga fedha hizo katika bajeti yake hii ya kwanza kwa ajili ya kuanza awamu ya kwanza ya ujenzi huo.
“Tuna imani kuwa mradi huu utasaidia kuleta mapinduzi makubwa ya uchumi katika nchi yetu na katika nchi nyingine za Afrika Mashariki na Kati zikiwemo Burundi, Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ndio maana hatutaki kupoteza muda kwa mazungumzo marefu, tunataka kazi ianze na watu waanze kunufaika,” alikaririwa Rais Magufuli katika mazungumzo hayo. Naye Dk Youqing alielezea utayari wa China kushirikiana na Tanzania katika mradi huo ambao zabuni za ujenzi zinatarajiwa kutangazwa hivi karibuni.
Rais Magufuli pia alipozindua ujenzi wa barabara ya juu ya Tazara, alirejea kauli hiyo, lakini akasisitiza kuwa reli hiyo ikifika Ruvu, mizigo yote ya Bandari ya Dar es Salaam itasafirishwa kwa reli mpaka eneo hilo na malori yataanzia Ruvu badala ya kuongeza foleni na kuharibu barabara za Dar es Salaam.
Manufaa mengine reli hiyo itakapokamilika, itapunguza gharama za usafirishaji wa mizigo kutoka katika Bandari ya Dar es Salaam kwa asilimia 30, na kuifanya bandari hiyo kuwa na unafuu mwingine kwa wateja kimataifa, mbali na unafuu unaotokana na eneo la kimkakati.
Mradi wa pili wa kielelezo katika bajeti ya maendeleo ya kwanza ya Serikali ya Awamu ya Tano kwa mujibu wa Dk Mpango ni ununuzi wa ndege tatu mpya za Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL).
Dk Mpango alitaja aina ya ndege hizo kuwa ni Bombardier Q400 mbili, zenye uwezo wa kubeba abiria 67 mpaka 88 kila moja na nyingine aina ya Bombardier CS 300 yenye uwezo wa kubeba abiria 100 mpaka 150.
Dk Mpango alitaja mradi wa tatu wa kipaumbele kuwa ni ununuzi wa meli moja mpya ya usafirishaji wa mizigo na abiria katika Ziwa Victoria, ununuzi utakaofanyika sambamba na ukarabati wa meli tatu za Mv Victoria, Mv Butiama na Mv Liemba ili kuimarisha usafirishaji.
Nia hiyo ya serikali ambayo sasa imewekwa katika utekelezaji wa miradi ya kielelezo iliyotengewa fedha iliwahi kuzungumziwa na Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, Machi mwaka huu aliposema serikali imeanza kukusanya fedha kwa ajili ya kununua meli mpya.
Alisema ahadi ya ununuzi wa meli hiyo iliyotolewa na Rais Magufuli katika kampeni za 2015 iko palepale kwa ajili ya usafirishaji wa abiria na mizigo kwenye Ziwa Victoria. Mradi wa nne wa msisitizo katika mpango wa maendeleo wa mwaka huu ambao utekelezaji wake utaanza ni mradi wa makaa ya mawe Mchuchuma na mradi wa chuma Liganga katika wilaya ya Ludewa mkoani Njombe.
Eneo la Mchuchuma linakadiriwa kuwa na hazina ya tani milioni 540 za makaa ya mawe ambayo ni malighafi muhimu ya uzalishaji umeme nafuu kuliko wa mafuta unaohitajika kwa wingi kwa ajili ya kujenga uchumi wa viwanda.
Aidha, eneo la Liganga linakadiriwa kuwa na hazina ya chuma cha pua tani milioni 45 ambayo ndiyo malighafi mama ya viwanda vikubwa na vya kati duniani. Mbali na hazina hiyo, maeneo hayo pia yapo kimkakati zaidi kwa kuwa yako karibu na hivyo kufanya uyeyushaji wa chuma hicho cha pua kuwa nafuu kuliko mahali pengine duniani, kutokana na ukaribu wa hazina ya makaa ya mawe na chuma hicho.
Serikali kutekeleza miradi mikubwa 4 ya kielelezo Serikali kutekeleza miradi mikubwa 4 ya kielelezo Reviewed by WANGOFIRA on 20:37:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.