SAMIA: WASICHANA VYUO VIKUU VINARA WA KUJIUZA
MAKAMU
wa Rais, Samia Suluhu Hassan, amekemea tabia chafu zinazofanywa na
baadhi ya wanafunzi wa kike wa vyuo vikuu nchini wanaodiriki kushiriki
kujiuza miili yao katika mahoteli makubwa na majumba ya starehe na
kuwataka kuacha tabia hiyo.
Makamu
wa Rais alisema hayo katika hafla iliyofanyika kwenye viwanja vya Chuo
Kikuu cha Mzumbe kwenye maazimisho ya siku ya wahitimu wa Chuo Kikuu Mzumbe pamoja
na Uzinduzi wa Kampeni za uchangiaji wa Ujenzi wa Bweni la wanachuo wa
kike.
Alisema
baadhi ya wanafunzi hao walidiriki kujiuza miili yao kwa ajili ya tamaa
ya kupata vitu vya anasa zikiwemo simu zenye gharama kubwa, mavazi na
vitu vingine jambo ambalo linafedhehesha jamii, wazazi na walezi wao.
Makamu
wa Rais alitumia fursa hiyo kuwataka wanafunzi wa kike wanaosoma katika
vyuo vikuu nchini kujikita katika elimu ili waweze kufanikiwa kwenye
maisha yao ya baadaye.
“Vyuo
vimeharibika kwa tamaa, sisi tulisoma hapa Mzumbe na tuliweza kuishi,
lakini wanafunzi wa sasa mnaingiwa na tamaa ya mashindano ya mavazi
utadhani mnagombea Umiss,” alisema Suluhu.
Aliongeza kuwa,
“nimeambiwa hapa Morogoro wapo baadhi ya wanachuo wa kike wanakwenda
kujiuza miili katika hoteli moja kubwa na kwenye majumba ya starehe kwa
tamaa tu, mnataka kuwa na simu ya laki saba na mavazi ya gharama kubwa
itawezekana wapi, mnatukwaza wazazi wenu.”
Aliwaonya
wanavyuo wenye tabia hiyo ya kuuza milii yao kuacha mara moja, huku
akisisitiza kuwa dunia ipo tu hivyo wasifukuzane nayo kwani mambo hayo
watayakuta baada ya kumaliza masomo yao.
Makamu wa Rais alitoa mfano kwa kuwaambia wanafunzi wa Chuo Kikuu Mzumbe,
“ukitaka
kushika nafasi kubwa kama hii ‘yangu’ ni lazima ufuatiliwe historia
yako tangu chini ukiwa shule ya msingi sasa kwa hali hiyo watoto wetu
mtakosa fursa za kuwa viongozi wa juu.”
Alisema mtoto wa kike anakuwa na safari ndefu zaidi yenye misukosuko mingi kuliko mtoto wa kiume anapokuwa akitafuta elimu.
Samia
alisema katika hatua ya elimu ya juu hasa kwa wanawake imegubikwa na
changamoto ambazo kama wanajamii wa Tanzania tunapaswa kuungana na
serikali kuziondoa ili kumuwezesha mtoto wa kike kufika mbali kielimu.
Alizitaja
changamoto hizo kuwa ni pamoja na ukosefu wa mabweni, ufinyu wa fedha
za kukidhi mahitaji na mtazamo hasi wa walimu na wanafunzi wa kiume
dhidi ya wanafunzi wa kike wanapokuwa vyuoni.
SAMIA: WASICHANA VYUO VIKUU VINARA WA KUJIUZA
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:33:00
Rating:
No comments: