Mahakama ya Mafisadi rasmi leo
MAHAKAMA Maalumu ya kushughulikia Makosa ya Rushwa na Ufisadi, inaanza rasmi leo Julai mosi.
Pamoja na kuanza kwa mahakama hiyo, serikali imeanza mchakato
kuifanyia marekebisho Sheria Namba 11 ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa
nchini ya Mwaka 2007 ili kuongeza ukubwa wa adhabu zinazotolewa sasa.
Mahakama hiyo iliyoahidiwa na Rais John Magufuli wakati wa kampeni za
Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 na imo katika Ilani ya Uchaguzi wa Chama
Cha Mapinduzi, itaimarisha zaidi taasisi za uwajibikaji zinazohusika na
mapambano dhidi ya rushwa.
Ahadi hiyo ambayo inatimizwa ndani ya kipindi cha miezi isiyozidi
saba tangu Serikali ya Awamu ya Tano iingie madarakani ni sehemu ya
mapambano ya kujenga misingi ya uchumi kwa kudhibiti rushwa na mianya
yake na kuleta uwajibikaji.
Akiahirisha Bunge jana mjini hapa, Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa
alisema utekelezaji wa ahadi hiyo unakwenda sambamba na kuonesha dhamira
ya serikali ya kushughulikia makosa ya rushwa na kuweka misingi imara
ya uwajibikaji katika sekta zote.
“Mahakama itawafanya watu waliozoea rushwa na ufisadi kujiuliza mara
mbili kabla ya kufanya uhalifu huo yaani kuwa deterrent,” alisema Waziri
Mkuu na kuongeza kuwa kuwapo kwake kutahamasisha wafanyabiashara
kufanya shughuli zao bila shaka huku umuhimu kwao, ikiwa ni kulipa kodi.
Akielezea umuhimu wa mahakama hiyo, alisema kwamba itasaidia
kuendeleza nia ya serikali ya watu kulipa kodi kwa maendeleo ya taifa.
Akielezea umuhimu wa kodi, alisema kuna mahitaji makubwa ya fedha za
utekelezaji wa miradi ya maendeleo na uendeshaji wa shughuli za serikali
na hivyo serikali itaendelea ukusanyaji wa mapato ya ndani na kudhibiti
mianya ya ukwepaji kodi.
Aidha, alisema serikali itaanzisha Kikosi Maalumu cha kufuatilia kwa
karibu matumizi ya mashine za kielektroniki (EFDs) za kutoa risiti kila
mfanyabiashara anapouza bidhaa au huduma na kuhakikisha kuwa Mamlaka ya
Mapato Tanzania (TRA) na Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA)
wanashirikiana na Wakala wa Serikali wa Serikali Mtandao kutekeleza
mfumo wa kuwa na dirisha moja na pia kudhibiti kikamilifu mizigo
inayoingia na kutoka bandari kavu.
Udhibiti wa matumizi
Akizungumzia matumizi, Waziri Mkuu alisema serikali itaendelea na
kudhibiti matumizi yasiyokuwa ya lazima na kufuatilia bajeti na matumizi
ya fedha za umma.
Na ili kufanikisha hilo, itafanya mapitio ya majukumu ya wizara na
taasisi za umma ili kuwianisha majukumu ya vyombo vya serikali na hivyo
kupunguza gharama za uendeshaji.
Aidha, uhakiki wa wafanyakazi utaendelea na watendaji wakitakiwa
wanadhibiti matumizi ya fedha za umma kwa kuzingatia ukomo wa bajeti ya
fungu husika lililoidhinishwa na Bunge.
Aidha, Waziri Mkuu aliagiza halmashauri zote nchini kuanzia leo
kuhakikisha kwamba zinatumia mifumo ya kielektroniki katika kukusanya
mapato, kulipa, kuweka na kutekeleza kikamilifu mikakati madhubuti ya
kuboresha makusanyo iwe yanafanywa na halmashauri au kupitia wakala
wake.
Waziri Mkuu alisema wabunge wamepitisha Bajeti ya Serikali
inayotegemea sana ukusanyaji wa mapato ya ndani ili kupunguza utegemezi
kutoka nje na kuhimiza uwajibikaji katika kuongeza juhudi za kukusanya
na kupanua wigo wa kutoza kodi ili mapato yaongezeke.
Aidha, alisema ipo haja ya wananchi kudai risiti kwa huduma
mbalimbali wanazonunua na kushirikiana na serikali kubaini wakwepa kodi
na kuziba mianya ya upotevu wa mapato ya serikali.
Aliwataka watumishi wa umma kuendelea kufanya kazi kwa maadili katika
maeneo yao wakijenga utamaduni wa kuzingatia sheria, kanuni na taratibu
katika utumishi wa umma ili kuongeza ufanisi na tija.
Mpango wa Maendeleo
Akizungumzia maeneo manne ya Mpango wa Maendeleo, Waziri Mkuu alisema
kwa sasa Serikali ya Awamu ya Tano imeweka msingi kupitia Mpango wa
Pili wa Maendeleo ya Taifa wa kukuza na kujenga uchumi wa viwanda kwa
kuweka mazingira yatakayochochea maendeleo ya viwanda.
Aidha, imejiweka katika hali ya kufungamanisha maendeleo ya uchumi na
maendeleo ya watu kwa kuhakikisha kwamba elimu inayotolewa ni bora na
inayojenga msingi wa rasilimali watu wanaohitajika kuipeleka nchi katika
uchumi wa kati.
Alisema ili kufanikisha hayo serikali itaimarisha mifumo ya kisheria
kuwa rafiki na kuvutia wawekezaji wa ndani na nje huku ikiimarisha
miundombinu ili iweze kutumika kirahisi na kupunguza gharama zake.
Ili kufanikisha ufanisi na tija, Waziri Mkuu alisema serikali
itaimarisha usimamizi, ufuatiliaji na tathmini ya mpango wenyewe wa
maendeleo mara kwa mara.
Ili kufanikiwa ametaka tabia ya vijana kushinda katika pombe na
kucheza pool table kuachwa na kuwataka viongozi waliochaguliwa sasa
wilayani na mikoani kuhakikisha kwamba maeneo ya starehe hayafunguliwi
wakati wa muda wa kazi ili vijana washiriki katika uzalishaji mali.
Akizungumzia mkakati wa ujenzi wa uchumi wa viwanda, Waziri Mkuu
alisema serikali itategemea zaidi sekta binafsi kama injini ya ukuzaji
uchumi na maendeleo na kwamba serikali haitajiingiza moja kwa moja
katika kujenga viwanda na kufanya biashara.
Miradi ya umeme
Akizungumzia uimarishaji wa uchumi kwa kuwa na uhakika wa nichati
hadi vijijini, alisema serikali imetenga fedha kwa ajili ya kuyapatia
maeneo yaliyo nje ya gridi ya taifa nishati bora ikiwa ni pamoja na
maeneo ya visiwani.
Alisema Serikali ya Uingereza na Sweden zinachangia katika
kuhakikisha kwamba mifumo hiyo ya kupeleka umeme maeneo yaliyo nje ya
gridi inafanikiwa. Alisema serikali imetenga zaidi ya Sh trilioni moja
kutoka ndani na benki ya dunia kwa ajili ya kuendeleza nishati vijijini.
Mahakama ya Mafisadi rasmi leo
Reviewed by WANGOFIRA
on
20:32:00
Rating:
No comments: