Maalim Seif Awahutubia Wamarekani ,Aanika Kila Kitu Kuhusu Sakata la Zanzibar


 
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharrif Hamad amesema vitendo vya unyanyasaji wapinzani vinavyoendelea nchini ni maradhi yanayokikumba chama tawala.

Maalim Seif aliyasema hayo alipokuwa akihutubia mkutano uliondaliwa na Kituo cha Elimu cha Kimkakati cha Kimataifa cha Marekani (CSIS) juzi, uliofanyika Washington DC nchini Marekani.

Akizungumzia kukandamizwa kwa wapinzani nchini, Maalim Seif alitoa mfano wa yeye kuhojiwa na polisi 11 kwa saa tatu na kijana aliyehukumiwa kifungo cha miaka mitatu au kulipa faini ya Sh7 milioni kwa kumkosoa Rais John Magufuli kwenye ukurasa wa facebook.

Kadhalika alitoa mfano wa viongozi wa Chadema kuhojiwa polisi na baadhi kuwekwa rumande kwa saa kadhaa huku kiongozi wa Chama cha ACT-Wazalendo naye akihojiwa kwa kufanya mkutano.

“Tunashuhudia mmomonyoko wa hali ya juu wa demokrasia sasa hivi… na hali hii itazidi miezi michache ijayo,” alisema.

Alisema wapinzani wanakandamizwa zaidi upande wa Zanzibar, na kusema kuwa CUF inataka ufafanuzi wa Muungano na wala si kuufuta.

Kiongozi huyo wa CUF alimlaumu Rais John Magufuli na kusema licha ya kuwa nchi za nje zinamuona anafanya vyema katika kupambana na rushwa, lakini Wazanzibari hawana furaha na uongozi wake.

“Kuna mitazamo tofauti hasa kwa walio nje ya Tanzania kwamba anapambana na rushwa, lakini kama kiongozi wa nchi, ameshindwa kufanya majukumu yake kuhusu Zanzibar,” alisema

Alisema mara zote Rais Magufuli anapoulizwa kuhusu suala la Zanzibar, husema hawezi kuchukua hatua.

“Wazanzibari wanachokitaka ni kuona Rais Magufuli anawajibika kama kiongozi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Maalim Seif ambaye katika mkutano huo, aliambatana na mkurugenzi wa Mambo ya Nje wa CUF, Ismail Jussa Ladhu na katibu wake, Issa Kheri Hussein.

Pamoja na mambo mengine, Maalim Seif alisema chama chake kipo tayari kufanya uchaguzi mwingine, endapo utasimamiwa na taasisi za kimataifa zisizofungamana na upande wowote.

Alisema wakati wakisubiri hilo, wafuasi wa chama hicho wanaendelea kufanya mgomo baridi usio na nia ya vurugu ili kuonyesha kuwa mambo hayawezi kwenda kama kawaida.

Akijibu swali la mmoja wa waliohudhuria mkutano huo kuhusu kutuhumiwa kuuvunja Muungano endapo atakuwa Rais wa Zanzibar, Maalim alisema chama tawala kimekuwa kikivibatiza vyama vya upinzani majina ya uongo ili kuvibomoa.

“Kuna wakati walikiita CUF kuwa ni chama cha Kiislamu, lakini hilo si kweli, tumenyang’anywa ushindi zaidi ya mara tano na wala hatujaleta fujo,” alisema.

Katika mkutano huo uliohudhuriwa pia na Rais Alassane Ouattara wa Ivory Coast, Maalim alielezea jinsi uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka jana ulivyofutwa na kusema kuwa CUF imekuwa ikinyang’anywa ushindi tangu mfumo wa uchaguzi wa vyama vingi uanze mwaka 1995.

“Tumefanya chaguzi tano, 1995, 2000, 2005, 2010 na 2015 katika chaguzi zote hizi, watu wa Zanzibar waliichagua CUF kuongoza Serikali. Lakini CUF imenyimwa kushika madaraka,” alisema Maalim na kuongeza:
 
“Kuna harufu ya hatari, kwa miaka yote hiyo tumejitahidi kuwatuliza wafuasi wetu, tumeangalia namna ya kuzungumza na wenzetu ili waheshimu maamuzi ya watu, lakini hawasikii.”

Alisema uchaguzi wa mwaka jana ulifanyika kwa uhuru na haki na matokeo yalionyesha kuwa CUF kimeshinda, lakini polisi waliizingira Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar (ZEC) na baadaye Mwenyekiti wa tume hiyo, Jecha Salim Jecha akayafuta matokeo hayo.

Alisema hata Umoja wa Ulaya (EU) walitoa ripoti yao wiki mbili zilizopita, iliyoonyesha kuwa ZEC haikuwa na mamlaka ya kufuta matokeo hayo.

“Nilijaribu kuwasiliana na Dk Ali Mohamed Shein , lakini hakutaka kupokea simu yangu, lakini baadaye nilimuandikia barua nikitaka mazungumzo naye, alikubali kwa masharti kuwa wawepo watu wengine.”alisema na kuongeza: “Tukakubaliana tufanye mazungumzo, lakini wawepo viongozi wakubwa, wakati tukiendelea na mazungumzo, Jecha alitangaza kuwa uchaguzi utarudiwa Machi 20.”

Maalim Seif alitaja athari za kufutwa kwa uchaguzi huo kuwa ni pamoja na kuvunja maridhiano ya kisiasa ya Zanzibar na Maamuzi ya Wazanzibari wengi walioamua nchi yao iongozwe kwa Mfumo wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).

Alitaja athari nyingine kuwa ni kuwarudisha nyuma watu wa visiwa vya Unguja na Pemba, kuibuka kwa siasa za chuki, migogoro na kubaguana.

“Hayo ni pamoja na kudhoofika kwa sekta za uchumi, biashara, ukosefu wa ajira na maendeleo kwa jumla, na siyo kwa Zanzibar pekee bali kwa Jamhuri yote ya Muungano wa Tanzania, hasa iwapo Mataifa yataitenga na kulinyima Taifa misaada, hali ambayo haiwezi kuepukika”. alisema

Akieleza msimamo wa waandaaji wa mkutano huo, uliojumuisha marais mbalimbali wastaafu wa Marekani na Ulaya, Mkurugenzi Mkuu wa NDI, Peter Craig aliwataka viongozi wa kisiasa wa nchi nyingine za Afrika kuiga mwenendo wa Maalim Seif.

“Tunaomba watu wengine wenye migogoro ya aina hii waige mfano huu wa Seif Sharif Hamad na sisi tutakuwa pamoja nao mpaka haki itendeke na ipatikane na tukianzia na Zanzibar,” alisema
Maalim Seif Awahutubia Wamarekani ,Aanika Kila Kitu Kuhusu Sakata la Zanzibar Maalim Seif Awahutubia Wamarekani ,Aanika Kila Kitu Kuhusu Sakata la Zanzibar Reviewed by WANGOFIRA on 20:13:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.