Kitwanga Aandaa Ibada ya Shukrani

Baada ya kimya cha muda mrefu, hatimaye aliyekuwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Charles Kitwanga ameibuka na kukabidhi ofisi na akatoa ratiba ya shughuli zake katika Jimbo lake la Misungwi ikiwamo ibada ya shukrani. 
Kitwanga ambaye uteuzi wake ulitenguliwa May 20 na Rais John Magufuli baada ya kuingia bungeni na kujibu swali akiwa amelewa, alikabidhi ofisi jana kwa Mwigulu Nchemba ambaye amechukua nafasi yake.
Baada ya uteuzi wake kutenguliwa, Kitwanga alitoweka bungeni na baadaye ilielezwa kuwa alikwenda Israel kabla ya hivi karibuni kurejea nchini na kusema kuwa yote yaliyotokea anamwachia Mungu. 
Hivi karibuni, Rais Magufuli alimhamishia Mwigulu katika Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kutoka Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi huku Dk Charles Tizeba akimrithi Mwigulu. 
Akizungumza katika mahojiano baada ya kukabidhi ofisi, Kitwanga alisema kila Mtanzania anaweza kufanya kazi iwapo atapewa nafasi huku akinukuu kaulimbiu ya ‘Hapa Kazi Tu’ na kwamba amefanya makabidhiano hayo kwa wema na upendo wa hali ya juu. 
Alisema amekabidhi ofisi bila kinyongo kwa sababu Tanzania si nchi yake peke yake bali ni ya wananchi wote. 
Ratiba jimboni 
Akizungumzia ratiba jimboni mwake, Kitwanga alisema Agosti 6, atafanya ibada ya shukrani nyumbani kwake Misungwi kumshukuru Mungu akisema hiyo ni baada ya ziara yake ya wiki sita mfululizo kwa wapigakura wake. 
Ziara hiyo itaanza keshokutwa atakapokutana na kamati ya mipango na fedha kabla ya kufanya kikao na madiwani wote wa jimbo hilo Jumamosi ijayo. 
Alisema Jumatatu ijayo atakabidhi vifaa mbalimbali vikiwamo magodoro na vitanda kwa hospitali ya wilaya na zahanati, vyerahani na kompresa kwa vikundi za ujasiriamali katika hafla itakayofanyika kwenye Stendi ya Mabasi Misungwi: “Hapo nitatoa nafasi ya dakika 10 mpaka 20 kwa waandishi wa habari kuniuliza maswali... lakini nisingependa umbeya... kwangu mimi ni Tanzania kwanza, nawaambia kabisa.” 
Baada ya shughuli hiyo, alisema siku inayofuata atakutana na wenyeviti wa vijiji vyote vya jimbo hilo kupanga namna atakavyofanikisha ziara yake katika maeneo yao, kazi ambayo alisema ataifanya kwa wiki sita mfululizo; “nitafanya ziara siku tano kwa kila wiki mfululizo, zamani nilikuwa nikigawa muda wa kutembelea jimbo na kurudi Dar kufanya kazi sasa nitakuwa huko muda wote. Dar nitakuwa nakuja mara chache tu.” 
Kitwanga Aandaa Ibada ya Shukrani  Kitwanga Aandaa Ibada ya Shukrani Reviewed by WANGOFIRA on 20:30:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.