WALIOBAKA NA KUSAMBAZA PICHA ZA TUKIO HILO WASOMEWA SHITAKA LAO LEO


Watuhumiwa wa Ubakaji Huko Dakawa,Wilaya ya Mvomero mkoani Morogoro wakipelekwa Kortini Mjini humo kusomewa Mashtaka yao mapema leo.

Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Morogoro imewapandisha kizimbani washtakiwa sita wakikabiliwa na mashtaka matatu tofauti, wakiwemo washtakiwa wawili wanaokabiliwa na mashtaka na kubaka na kumuingilia kinyume na maumbile bila ridhaa yake binti mwenye umri wa miaka 21 mkazi wa Wami Dakawa Wilayani Mvomero.

Katika kesi hiyo iliyovuta hisia ya mamia ya wananchi wa mkoa wa Morogoro, washtakiwa Iddi Adam Mabena (21) mkazi wa Njombe na Zuberi Thabit (30) mkazi wa Mbarali Mbeya wamefikishwa mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi  wa Mahakama ya mkoa wa Morogoro Mary Moyo, wakikabiliwa na shtaka la kubaka na kulawiti, wanalodaiwa kutenda aprili 27 mwaka huu majira ya usiku katika nyumba ya kulala wageni ya Titii iliyopo Wami Dakawa wilayani Mvomero.

Upande wa Serikali katika shtaka hilo lililofanyika faragha kwa mujibu wa sheria, umewakilishwa na waendesha mashtaka Gloria Rwakibalila, Edgar Bantulaki na Calistus Kapinga. Washtakiwa wote wawili wamekana mashtaka na kesi hiyo imepangwa kufikishwa tena Juni Mosi mwaka huu  kwa ajili ya kutajwa.

Upande wa mashtaka umewasilisha kiapo cha pingamizi la dhamana kwa ajili ya usalama wa washtakiwa kwa vile shauri hilo limegusa hisia ya jamii na kwa  vile upelelezi wa shauri hilo bado haujakamilika, hivyo washtakiwa wanaweza kuharibu upelelezi.

Katika shtaka jingine lililofikishwa mbele ya Hakimu Ivan Msaki wa Mahakama hiyo, washtakiwa sita wakiwemo Iddi Mabena, Zuberi Thabiti na wengine wanne Rajab Salehe, Ramadhani Ally Makunja anayetetewa na wakili Ignas Punge, Muhsin Ngai na John Petter maarufu kama Paroko, wakazi wa Wami Dakawa wilayani Mvomero wanadaiwa kusambaza picha chafu na za ngono kwa njia ya mtandao kinyume na sheria ya makosa ya mtandao no 14 ya mwaka 2015.

Washtakiwa wote sita wamekana mashtaka ambapo upande wa mashtaka ukiongozwa na mawakili watatu wa serikali uliomba washtakiwa wanyimwe dhamana kwa usalama wao na kutoharibu upelelezi kwa vile bado haujakamilika, huku ule wa mshtakiwa namba nne ukiomba kuwasilisha kiapo cha kupinga mshtakiwa kunyimwa dhamana, ambapo suala hilo la dhamana katika shauri hilo litafikishwa tena juni mosi kwaajili ya kujadiliwa na washtakiwa wote wamerudishwa rumande.


TAZAMA VIDEO HAPA



WALIOBAKA NA KUSAMBAZA PICHA ZA TUKIO HILO WASOMEWA SHITAKA LAO LEO WALIOBAKA NA KUSAMBAZA PICHA ZA TUKIO HILO WASOMEWA SHITAKA LAO LEO Reviewed by WANGOFIRA on 11:02:00 Rating: 5
Powered by Blogger.