Polisi Akamatwa na Noti Bandia Zenye Thamani ya Sh. 870,000 Alikuwa Anajiandaa Kuzitumbukiza TIGO PESA

 

ASKARI Polisi Ezekiel Dinoso (32) mkazi wa tarafa ya Mgeta, wilayani Mvomero mkoani Morogoro amekutwa na noti bandia za Sh 10,000 zenye thamani ya Sh 870,000, akijiandaa kuzitumbukiza katika akaunti ya mtandao wa Tigo Pesa katika duka mojawapo eneo la Mawenzi, Manispaa ya Morogoro. 

Kamanda wa Polisi mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei, alisema jana kuwa tukio hilo ni la Mei 14, mwaka huu saa 1:00 usiku katika eneo la Mawezi , Manispaa ya Morogoro. 

Mtuhumiwa alikutwa katika duka la Hadija Hamis (35) mkazi wa Chamwino, wakati alipohitaji kuwekewa fedha hizo, mwenye duka alimtilia shaka hivyo kuarifu Polisi. 

Mtuhumiwa alipokamatwa na askari baada ya kutolewa taarifa Kituo cha Polisi, alikutwa akiwa na noti bandia 87 za Sh 10,000. 



Alitaja namba za noti hizo ni BX 7287490 zikiwa noti 22 , BX 728792 zikiwa noti 20, BX 728791 noti 19 na BX7287487 zikiwa noti 15 na kufanya jumla ya thamani ya Sh 870,000 ambazo ni bandia. 

Kamanda Matei alisema mtuhumiwa huyo anaendelea kuhojiwa na baada ya uchunguzi kukamilika atafikishwa mahakamani. 

Katika tukio jingine, Rashidi Shabani (30) na Michael Lukasa (39), wote wakazi wa Ngerengere wanashikiliwa na Polisi kwa kuwakuta na nyama ya nyati kilo 300 na silaha aina ya gobole iliyotumika kumuulia mnyama huyo. 

Kamanda wa Polisi wa Morogoro, Matei, alisema walikamatwa Mei 14, mwaka huu saa 2:00 usiku katika kijiji cha Kinonko, kata ya Gwata, wilaya ya Morogoro. 

Matei alisema, kukamatwa kwa watuhumiwa hao kumetokana na jitihada zinazofanywa na polisi kwa kushirikiana na wananchi katika kukomesha vitendo vya uhalifu.
Polisi Akamatwa na Noti Bandia Zenye Thamani ya Sh. 870,000 Alikuwa Anajiandaa Kuzitumbukiza TIGO PESA Polisi Akamatwa na Noti Bandia Zenye Thamani ya Sh. 870,000 Alikuwa Anajiandaa Kuzitumbukiza TIGO PESA Reviewed by WANGOFIRA on 20:58:00 Rating: 5
Powered by Blogger.