LOWASSA ATAJWA KUNUNUA NYUMBA ZA SERIKALI

MBUNGE wa Viti Maalumu (CCM), Ritha Kabati amemtaja aliyekuwa mgombea urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Edward Lowassa kuwa alinunua nyumba ya serikali iliyouzwa mwaka 2002 yenye jengo namba 68.
Kabati alisema hayo wakati akichangia mjadala wa bajeti ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano jana na kueleza kuwa katika hotuba ya Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni walieleza suala la ununuzi wa nyumba za serikali.
Alisema hotuba hiyo ilisema nyumba za serikali 7,921 ziliuzwa tangu mwaka 2002 hadi 2004 na kutaka serikali ya awamu ya tano kurejesha nyumba hizo kutokana na walionunua kukiuka mikataba na malengo ya mauzo.
“Naomba niwaambie ukiwa usiangalie boriti lililo katika jicho la mwenzako wakati kwako lipo, kwani hata mgombea wao wa urais Edward Lowassa alihusika kwa kununua nyumba ya plot namba 68 na Fredrick Sumaye alikuwa Waziri Mkuu na kuhusika kuuza nyumba hizo,” alisema Kabati.
Baada ya kueleza hayo, Kiongozi wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni na Mbunge wa Hai, Freeman Mbowe (Chadema) aliomba kumpa taarifa mbunge huyo kuwa taarifa hiyo ni kwa maslahi ya taifa, hata kama mhusika atakuwa katokea kambi ya upinzani sheria itachukua hatua.
Awali katika michango mbalimbali ya wabunge wa upinzani wamekuwa wakilalamikia kuuzwa nyumba hizo za serikali na kudai kuwa watumishi wapya wengi walioajiriwa, wamekuwa wakikosa maeneo ya kuishi.
Mbunge wa Kawe, Halima Mdee (Chadema) akichangia mjadala huo alilalamikia kuuzwa kwa nyumba hizo pamoja na nyingine za Tazara zipatazo 500 na kuamua kumpatia Waziri wa Ujenzi ,Uchukuzi na Mawasiliano ripoti aliyodai inaonesha nyumba hizo zilivyouzwa.
LOWASSA ATAJWA KUNUNUA NYUMBA ZA SERIKALI LOWASSA ATAJWA KUNUNUA NYUMBA ZA SERIKALI Reviewed by WANGOFIRA on 20:59:00 Rating: 5
Powered by Blogger.