WANAFUNZI UDSM NA UDOM WAMMWAGIA SIFA KEDEKEDE PROF. NDALICHAKO KWA KUTUMBUA MAJIPU HESLB

NA, BARAKA NGOFIRA
0763580901, 0716216249
Image result for profesa Ndalichako
Waziri wa Elimu,Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi Profesa Joyce Ndalichako akizungumza na waandishi wa Habari (hawapo pichani)
Ni furaha isiyo na kifani mioyoni mwa wanafunzi wa vyuo vikuu nchini, pale waliposikia taarifa kuhusu kusimamishwa kazi kwa wakurugenzi wanne wa bodi ya mikopo (HESLB). Kutokana na kile ambacho wao wanaeleza wazi kuwa walikuwa wamechoshwa na utendaji wa bodi hiyo iliyokuwa inafanya kazi kwa mazoea na ubadhilifu wa fedha za vijana wa kitanzania kwa muda mrefu.
Lakini pia kwa wale ambao awanufaiki na bodi huku sifa za kupata mkopo wakiwa nazo, nao walisikika sauti zao zikipazwa kwa sauti kuu, zikisema afadhali maana tumeteswa kwa muda mrefu, wazazi wenu wanakatwa kodi kila kuchapo. Watoto wa wakulima wanakosa mkopo huku watoto wa vigogo wakipewa hela hata pasipo kuomba na kuwaringishia pesa ambazo kwa namna moja ama nyingine hazikuwa za kwao.
Siku ya jumanne majira ya saa asubuhi zilienea taarifa juu ya waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na mafunzo ya ufundi Profesa Joyce Ndalichako kuwa amewasimamisha kazi watendaji 4 wa bodi ya mikopo ya Elimu ya juu (HESLB) akiwemo mkurugenzi mtendaji wa bodi hiyo Bwana George Nyatenga na wenzake watatu kwa utendaji wao usioridhisha pamoja na kuwa wazembe. Jambo linaloibua matatizo makubwa na kuathiri maisha ya wanafunzi wa vyuo vikuu kogoma na baadhi yao kuandamana kudai pesa zao.
Pamoja na kusimakishwa kwa kwa wakurugenzi wengine watatu ambao ni Yusufu Kisare (Fedha na utawala), Juma Chagonja (urejeshaji mkopo) pamoja na Onesmo Laizer (upangaji na utoaji mikopo). Ambapo wote hawa wanahusika kufanya ubadhirifu wa zaidi ya Bilioni 3.2, ambazo zililipwa kwa watu waliokufa, waliositisha masomi, waliomaliza masomo na wengine kulipwa zaidi ya mara mbili. Lakini jambo la kushangaza ni kuwa ni zaidi ya wanafunzi 19,348 kupewa mkopo pasipo kupitishwa na kamati ya mikopo, huku wanafunzi 54,299 kupewa mikopo pasipo kuomba na kusababisha watoto wengi wenye vigezo na waliolipa zaidi ya Tsh 50,000 katika harakati za kuomba na kutuma maombi kunyimwa mikopo. Huku wengine wakigawana pesa kwa kujuana na kubagua vijana wa walala hoi ambaao hawajui kesho yao itakuwaje.
Lakini pia kwa upande wangu kama mwanahabari na mwanafunzi pia namshukru sana waziri Profesa Ndalichako kwa uamuzi wake, kwani kila mara suala la utendaji mbovu wa Bodi ya Mikopo umekuwa ukilalamikiwa sana na watu wengi. Hasa wanafunzi na wazazi kwani wanatumia pesa nyingi kuomba huku wengine wakithubutu kuomba zaidi ya mara 4 pasipo kupata mkopo huku sifa zote wakiwa nazo.
Lakini pia wanafunzi wa vyuo vikuu wengi wamekuwa wakieleza wazi  jinsi taasisi hii inafanya kazi kwa mazoea na kusahau kuwa sasa ni muda wa kazi tu, pia wamekuwa wakieleza wazi jinsi mikopo hii inavyotolewa pasipo kuzingatia vigezo na kufanya baadhi ya vijana wa kitanzania tena hali ya chini kutoendelea na masomo ya elimu ya juu, kwa saababu ya kukosa mkopo huku sifa na vigezo wakiwa navyo. Na kushangaa wengine waliosoma shule wanazoziita wao eti ni za “SAINT” wamepata mkopo tena kwa asilimia mia moja lakini wao waliosoma shule za kayumba wananyimwa.
Pamoja na jitihada zote ulizozionyesha lakini bado kuna haja ya kufumuliwa yote na kuundwa upya, ili kuweza kuleta ufanisi wa kazi ambao utasababisha  vijana wengi wa kitanzania kufaidi matunda ya nchi yao japo kwa kuwezeshwa kusoma elimu ya juu.
Elihazina Kangalu ni mwanafunzi wa shahada ya kwanza ya ualimu katika chuo kikuu cha Dodoma (UDOM) anasema “kwangu mimi ni sahihi kwa sababu kwa sasa utendaji wao umekuwa ukidorora sana na wanafunzi wengi wamekuwa wakilalamikia utendaji wa bodi hii”
Lakini pia Celvin Nkya mwanafunzi wa shahada ya kwanza ya ualimu chuo kikuu cha Dodoma yeye anasema “ni jambo zuri kwa sababu kati ya bodi hii imekuwa miongoni mwa taasisi ambayo watu wake wamekuwa wakifanya kwa mazoea na kujisahau kuwa wanawatumikia watanzania ambao ni wasomi na viongozi wa kesho.
Nae Rebeka Kishegena ambaye mhitimu wa shahada ya kwanza ya masuala ya kijamii (Sociology) katika chuo kikuu cha Dar es salaam (UDSM) yeye anasema waondolewe tu kwa sababu wamekuwa wakiwahujumu wanafunzi pesa zao na kuwacheleweshea pesa zao huku wakijua kuwa kuna bajeti ambapo wamesababisha wanaafunzi wengi kupata pesa za mkopo na kuishia kulipa madeni”.
Kwa upande wake Marium Thabiti mwanafunzi wa Shahada ya kwanza ya  mawasiliano kwa Umma kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam yeye anasema “ ni sawa kama uchunguzi umefanyika na wamebainika wana makosa ni lazima wawajibishwe. Kwa sababu kila kazi ina kanini na taratibu zake na ni lazima wala si ombi kuzifuata” na kuongezea kuwa “kwa kuwa wamekiuka ni lazima wawajibishwe ili iwe funzo kwa wengine walio katika ofisi za umma”.
“Kwa kweli hilo suala lina pande mbili kwa maoni yangu, inapaswa nijiulize uhalali wa kusimamishwa na pili matunda ya kuteuliwa kwa viongozi wapya. Nikianza na uhalali wa kusimamishwa nafikiri kila mwanafunzi anafahamu kuwa ni halali kutokana na taarifa walizosema kuwa kila mwanafunzi amepewa mkopo jambo ambalo halina ukweli wowote. Na ucheleweshwaji wa fedha za mikopo kwa wastahiki jambo ambalo limekuwa sugu katika miaka yangu miwili niliyopo hapa chuoni” alisema Pious Sylvester mwanafunzi wa shahada ya kwanza ya Sheria kutoka Chuo kikuu chaa Dar es salaam.
Lakini pia Neema Mbundamila mwanafunzi wa shahada ya kwanza ya Mawasiliano kwa Umma kutoka chuo kikuu cha Dar es salaam UDSM yeye anasema “Ni jambo la kusikitisha sana kuona pamoja na juhudi za Rais Dokta Magufuli kuhakikisha anatafuta fedha ili ziwanufaishe wanafunzi wa Elimu ya Juu na wengine wanahitaji mkopo lakini bado kuna baadhi ya wakurugenzi wanakwamisha juhudi hizo”.
Na kuongeza kuwa ikiwa wakurugenzi wa Bodi ya mikopo waliosimamishwa kazi watakutwa na hatia basi sheria kali zichukuliwe juu yao ikiwa ni pamoja na kufilisiwa mali na fedha zao na kupelekwa kwa walengwa.  Pia anamuomba Profesa Ndalichako kuangalia upya waombaji wa mkopo ambao wanaendelea na masomo yao kwa mwaka wa pili, tatu na nne lakini hawakupata mkopo, japo waliahidiwa na Rais Magufuli kipindi cha Kampeni zake.
Na kusisitiza kuwa “waathirika ni wengi na athari zinazidi kuongezeka hivyo ni muhimu kwa serikali kuwapitia mkopo kwani hakuna ajuaye kesho ya yule anayemfadhili kuwa itakuwaje endapo uchumi ukiyumba au kufariki lakini pia anaongeza kwa kusema wakati watoto na wanafunzi wa watanzania maskini na wa wakulima wanakosa mkopo kwa kunyimwa kimakusudi kabisa kwa kisingizio cha fani wanazosomea, jambo linalopelekea wengi kupoteza haki yao ya msingi ya kitaba ya kupata elimu na mahitaji mengine kwa sababu tu ya upuuzi na uzembe wa wakurugenzi wa wasiowaadilifu” na kumuomba waziri profesa Ndalichako kuwawajibisha vilivyo.
Kwa upande wa shirikisho la wanafunzi wa Elimu ya juu ( TAHALISO) kupitia Mwenyekiti wa mawaziri wa mikopo ya elimu Juu Ndugu Shitindi Venance, ambaye pia ni msemaji wa shirikisho hilo anasema kuwa wamepokea kwa furaha kubwa kusimamishwa kwa wakurugenzi hao wa bodi ya mikopo.
“Sisi kama shirikisho la wanafunzi wa Elimu ya Juu (TAHILISO) tumepokea kwa furaha kubwa tena sana na tupende kumpongeza waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi kwa hatua aalizozichukua. Kwa upande wetu TAHILISO tumekuwa tukinyanyaswa na wakurugenzi hawa hasa Mkugenzi mkuu wa bodi ya mikopo aliyesimamishwa ndugu George Nyatenga amekuwa akitutishia sana hasa mimi mwenyewe, kwani tayari keshaniandikia barua mbili kupitia uongozi wa chuo ili nifukuzwe chuo lakini nashukru sijafukuzwa kwani hata uongozi wa chuo unaelewa napigania maslahi ya vijana wa kitanzania na watoto wa maskini na wakulima ambao hawana uwezo wa kujisomesha au kusomeshwa na wazazi au wadhamini wao”
Amefafanua kuwa mpaka sasa zaidi ya wanafunzi 8000 nchi nzima awajalipwa pesa zao za mkopo tangu wameanza masomo yao Novemba mwaka jana. Hivyo kuomba viongozi na makaimu walioteuliwa kulifanyia kazi kwa haraka iwezekanavyo ili kunusuru maisha ya wanafunzi hawa, wanaoishi kwa kukopeshwa na wenzao tena kwa riba kubwa lakini kushindwa kulipa kwa wakati jambo linalojenga uadui na wivu miongoni mwao.
Lakini pia kama msemaji wa Mawaziri wa Mikopo TAHALISO Bwana Shitindi alisema “inabidi bodi hii itambue kuwa inafanya kazi na vijana wasomi tena watu wazima na wala si watoto wa chekechea , hivyo na Mkurugenzi atakayechaguliwa kurithi nafasi ya Nyatenga ajiandae kabisa kujua anakuja kufanya kazi na wasomi wanaojua hali halisi ilivyo, wakiwa na akili timamu kabisa ya kufanya tathimini ya na kuchambua ukweli ni upi na ubaya ni upi kwa hiyo aje kazini akitambua hilo kabisa na kama naye atatambua hilo hakika hatadumu bodi ya mikopo hataondolewa tu”
Na kumalizia kwa kutoa Ushauri kuwa Mkurugenzi ajaye ni vyema na ni lazima akasome utafiti uliofanya na Profesa Maboko na kuchapishwa mwaka 2011, unaotoa miongozo mizuri kuhusu mageuzi ya Bodi ya mikopo. Na kuamini kuwa Mkurugenzi atakayeteuliwa atayamaliza matatizo yote ya mikopo na kufanya wanafunzi wafurahie nchi yao na masomo yao vyuoni waishi salama pasipo kucheleweshewa pesa kutoka bodi ya mikopo ambazo muda mwingi zimegeuka kulipa madeni.

Makala hii imeandaliwa na Baraka Ngofira, mwanafunzi UDSM-SJMC. Anapatikana kwa mawasiliano ya 0763580901, 0716216249 au barua pepe ya barakangofira@gmail.com kwa maoni na ushauri zaidi.


WANAFUNZI UDSM NA UDOM WAMMWAGIA SIFA KEDEKEDE PROF. NDALICHAKO KWA KUTUMBUA MAJIPU HESLB WANAFUNZI UDSM NA UDOM WAMMWAGIA SIFA KEDEKEDE PROF. NDALICHAKO KWA KUTUMBUA MAJIPU HESLB Reviewed by WANGOFIRA on 22:09:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.