MOSHA AMTAKA NDESAMBURO AMLIPE TSH. MOJA NA SENTI 25



Image result for DAVIS MOSHA    

Moshi.
 Mfanyabiashara Davis Mosha amempa siku saba Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Kilimanjaro, Phillemon Ndesamburo, kumlipa fidia ya Sh1.25 (Shilingi moja na senti ishirini na tano) kwa madai ya kumdhalilisha.
Awali, katika barua yake, Mosha alimtaka Ndesamburo kumlipa fidia ya Sh100.25, baadaye ilirekebishwa na kudai Sh1.25.
Hata hivyo, Ndesamburo ambaye amekuwa Mbunge wa Moshi Mjini kuanzia mwaka 2000 hadi 2015, alisema hajapokea barua hiyo. “Niseme nini sasa wakati hiyo barua sijaipata?” alihoji Ndesamburo.
Mosha ambaye aligombea ubunge wa jimbo hilo (CCM) katika uchaguzi uliofanyika Oktoba 25, mwaka jana na kubwagwa na Jaffar Michael wa Chadema, anadai fidia hiyo kwa kile anachodai ni matamshi ya kashfa yaliyotolewa dhidi yake na Ndesamburo.
Alidai kabla na wakati wa kampeni za Uchaguzi Mkuu mwaka jana, Ndesamburo alisema Mosha anafanya biashara ya dawa za kulevya wakati akijua ni uongo.
Katika barua hiyo iliyotumwa kutoka Kampuni ya Madega & Co. Advocates, Mosha anadai Ndesamburo alitoa matamshi hayo kwenye kikao alichofanya katika hoteli ya Keys.
“Katika kikao kingine ulinukuliwa ukisema Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imempa Mosha Sh2.5 bilioni kwa ajili ya kampeni.
“Moja kati ya ushahidi madhubuti ambao mteja wetu atautumia mahakamani ni mkanda wa sauti ya maneno ya kashfa mbele ya mashuhuda wengi,” alidai.
Kwa mujibu wa barua hiyo yenye kumbukumbu MCA/LT/24/2016 iliyotiwa saini na Wakili Madega Omari, Ndesamburo alidai Mosha alipewa Sh2.5 bilioni za kampeni na Serikali.
Inadaiwa kuwa matamshi hayo, yalisababisha Mosha kupata maumivu na kushindwa nafasi ya ubunge Jimbo la Moshi Mjini alilokuwa akigombea kwa tiketi ya CCM.
Pia, Mosha anamtaka Ndesamburo kuomba radhi kupitia vituo vya Redio One, Clouds FM, TBC Taifa, RFA na nyingine ambazo zinasikika zaidi katika jimbo hilo.
Mfanyabiashara huyo anayemiliki vitega uchumi kadhaa nchini, amemtahadharisha Ndesamburo kuwa kama hatatimiza masharti hayo, watafungua kesi mahakamani. Alidai anashirikiana na mbunge wa sasa kwa ajili ya kuleta maendeleo katika jimbo hilo.     
SOURCE, MWANANCHI
MOSHA AMTAKA NDESAMBURO AMLIPE TSH. MOJA NA SENTI 25 MOSHA AMTAKA NDESAMBURO AMLIPE TSH. MOJA NA SENTI 25 Reviewed by WANGOFIRA on 07:45:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.