MFUMO WA ELIMU YETU NDIYO CHANZO CHA WAHIMU KUTOKIDHI VIGEZO VYA SOKO LA AJIRA


Na, BARAKA NGOFIRA
0763580901, 0716216249
Tanzania ni moja ya nchi ambayo asilimia kubwa ya vijana wanaohitamu masomo yao kutoka vyuo mbalimbali vya elimu ya juu, na vile vya elimu ya kati ni wengi ukilinganisha na nafasi za kupata ajira katika fani walizozisomea. Na wengi kutunukiwa vyeti vya stashada na wengine shahada za juu, lakini pamoja na yote hao mianya ya wao kupata ajira imekuwa ni migumu ikilinganishwa na miaka kumi au kumi na mitano iliyopita.

Pamoja na jitihada mbalimbali zilizofanywa na zinazoendelea kufanywa na wadau wa elimu kwa kushiriana na serikali pamoja na mashirika binafsi lakini ndivyo tatizo linazidi kuwa kubwa. Najiuliza maswali mengi ambayo yanayonifanya niumwe kichwa kila siku hasa pale ninapofikiria juu ya vijana wenzangu waliohitimu na waliotunikiwa vyeti, stashada, na wale wa shahada mwaka huu na wengine kunifanya nidondoshe machozi.

Wengi wakiwa wanafurahi kuvaa majoho na kofia siku ya mahafali yao na kusahau kesho yao itakuwaje baada ya kuvua majoho na kuachana na mitihani ya darasani, huku mtaa na msoto wa ajira ukiwaita na kuwangojea kwa hamu kubwa baada tu ya kuachana na maisha ya vyuoni.
 Na pengine huwa natoa machozi kwa kuona tangazo la kazi likihitaji mtu mmoja, lakini maombi zaidi ya elfu mbili yakitumwa ili mmoja wao achaguliwe. Na chakusikitisha sana huenda hata hao 2000 na zaidi asipatikane hata mmoja anayehitajika. Hapo ndipo najawa na maswali yafanyayo kichwa changu kiendelee kuniuma.

Sijasahau zile nafasi chache za kazi zilizotangazwa na uhamiaji zizofanya watu wakafanye mtihani wa kazi uwanja wa taifa, na kuudhihilishia ulimwengu kuwa vijana wengi wa kitanzania hawana ajira. Pia nahisi ni tukio ambalo liliandikwa kwenye vitabu vya kumbukumbu maarufu kama encyopedia kwani ilikuwa inauma na kusikitisha sana kuona vijana wengi zaidi ya elfu kumi wanagombania nafasi zisizozidi 100 za ajira.

Inaniuma sana hasa kwa hawa waliohitimu mwaka huu na wao wanaenda kuongeza idadi tena ya wale waliosota mtaani kwa miaka zaidi ya kumi, huku bahasha zao za kaki zilizochakaa na CV zao kuchafuka na wengine viatu vikiwa vimewaisha soli kwa sababu tu ya kutafuta kazi katika ofisi mbalimbali za kiuserikali na zile za binafsi.

Kinachonishangaza pia ni kuona wengine wanapata kazi tena kwenye makampuni makubwa ya kitaifa na kimataifa huku wakiwa bado shule. Hapa napo najiuliza maswali mengine tena mengi tu kuhusu wao, kuwa wanatumia njia gani kupata kazi hizo au kwa nin I wao wanaosoma wapate kazi mapema huku wengine wakihangaika kutafuta kazi kwa zaidi ya miaka mitano na wengine kukata tama na kuweka vyeti chini na kutafuta njia ya pili au kujiingiza kwenye vitendo viovu na uporaji wa kutumia silaha, na wengine kuamua kujiingiza kwenye uuzaji wa madwa ya kulevya na ujangiri wa wanyamapori wetu pasipo hata kujali athari zake.

Siishii hapo tu huwa naenda mbali zaidi kwenda kuwauliza baadhi ya wakurugenzi ambao utangaza nafasi za kazi na vijana wengi wa kitanzania kujitokeza na kazi wakakosa kwa kutotimiza vigezo. Huwa wananipa majibu ambayo kwa namna moja ama nyingine nakubaliana nayo lakini mengine inanibidi  nikubaliane nao kwa shingo upande.

Mmoja wapo wa waajiri wa kampuni kubwa tu ya hapa nchini aliniaambia kuwa maombi mengi ya kazi hutumwa ofisini kwake tena na watu waliopata ufauli mkubwa katika vyuo vya walivyosoma, lakini wanapoajiriwa kiwango cha ufanyaji kazi wake na ufaulu alioupata na kutunukiwa na chuo chake ni vitu viwili tofauti.

Kwani utendaji kazi wake ni hafifu mno ukilinganisha na kiwango chake cha elimu na ufaulu ambao yeye alinambia walimu wake ni kama walimzawadia au kuukadilia, aliniambia vijana wengi wa kitanzania hususan wanaohitimu vyuo vikuu kwa sasa ni aibu hata kusema kazi wazifanyazo ofisini ukilinganishwa na kiwango cha elimu na ufaulu wao.

Akanipa mfano kuwa mwezi novemba aliitwa kwenda kusimamia mahojiano ya kutafuta watu 3 kutoka Afrika mashariki ili wakafanye kazi katika Benki ya Dunia. Lakini pamoja na kupata maombi zaidi ya 700 kutoka Tanzania na yeye mwenyewe kukaa chini na kupoitia ombi moja baada ya jingine, lakini cha kusikitisha alikosekana kijana hata mmoja wa kitanzania ambaye alikitimiza vigezo vya kufanya kazi katika shirika hilo la umoja wa kimataifa.

Nilijiuliza sana shida iko wapi na kwa nini iwe kwa watanzania tu, mbona kwa wenzetu wakenya, wanyarwanda, warundi na waganda wanafanya kazi tena kubwa tu kwenye mashirika binafsi yanayomilikiwa na watanzania wenyewe. Hapo ndo nikapata jibu kubwa kuna shida kwenye mifumo yetu ya elimu aiwaandai vijana wa kitanzania kuingia sokoni mara tu wanapohitimu masomo yao  hasa ya juu.

Ukilinganishwa na miaka ya 1990 kurudi nyuma mfumo wa elimu yetu ulikuwa mzuri na masomo yalilenga kumwandaa kijana wa kitanzania kuajirika na kujiajiri mwenyewe na si kutegemea ajira ya serikali au kutoka kwenye sekta binafsi.

Nilipomuuliza baba yangu kuwa kwa nini kipindi chao walikuwa hawasoti mtaani kama sasa alinambia kipindi chao, walikuwa na mumo ambao ulikuwa unawafanya wao wajiajiri na si kutengemea ajira na ndiyo maana walijituma na wengi wao kugombaniwa wakiwa bado masomoni ,tofauti na leo wasomi wanavyogombania kazi.

Hapo ndipo nilipokumbuka ile falsafa ya elimu ya kujitegemea iliyoanzishwa na Hayati Baba wa Taifa mwalimu JK Nyerere baada ya azimio la Arusha ambapo elimu hii ilimjenga mtanzania aliyekuwa anasoma kwa kipindi hicho aweze kuwa wa uwanja mkubwa wa kujiajiri na sio kuajiriwa hapo ndipo masomo kama ya kilimo, ufugaji, muziki, sanaa na mengine mengi ya ufundi kama stadi za kazi yalianzishwa ili tu kumjenga mtoto wa kitanzania aweze kijiajiri na si kutegemea ajira.

Lakini pia nikakumbuka lile azimio la Musoma la mwaka 1974, ambalo nalo lililenga kumjenga mtoto wa kitanzania kuweza kusoma elimu ya msingi ambayo ingemuwezesha ajue kusoma, kuandika na kuhesabu. Hapo ndipo serikali iliamua kuajiri walimu wengi ambao walijulikana kama walimu wa UPE. Ili tu waweze kufundisha vijana wa kitanzania waondokane na maadui ambao mwalimu aliwataja kuwa Ujinga, Maradhi na Umaskini.

Chakunishangaza mpaka sasa maadui hawa bado hawajaisha kwani pamoja na watanzania wengi kwa sasa kujidai kuwa sisi si wajinga lakini bado hatujaweza kutengeneza kitu ambacho tunaweza kujivunia tuendapo popote pale ulimwenguni. Ebu jiulize wembe tunaletewa na wachina, sabuni, chumvi, viberiti na vinginevyo vingi tunaletewa na wakenya, nguo tunaagiza  nje sasa welevu wetu huko wapi? Au tunajivunia nini, Tanzanite, Dhahabu au Almasi ambazo kila mwaka Afrika Kusini na Kenya wanapewa tuzo na zawadi kubwa na mataifa makubwa duniani kwa uuzaji wa maduni hayo nje. Huku dunia yote inatambua kuwa Tanzanite inapatikana Tanzania tu.

Tusiongelee hayo kwa leo lakini tuangalie sera yetu ya elimu iko wapi? Nawaulizeni nyie wakubwa mlioko huko juu ambao wengine wenu mnatutia aibu kama nchi mnashindwa kuelewa hata historia ya nchi yetu, na kusema vitu ambavyo ni aibu tupu kwa nchi yetu.  Na ndiyo maana hata sishangai kumwona anayejiita msomi wa chuo kikuu ukimuuliza kirefu cha TANU ni nini anajibu madudu ambayo hata hayapo.

Tatizo ni mfumo wetu wa elimu na si vinginevyo, inamjenga kijana wa kitanzania kutegemea kazi za ofisini. pia kutokana na utandawazi pasipo hata kujiuliza mara mbilimbili juu ya utoaji wa elimu ya juu na ya kati kwa Kuruhusu umilikaji wa vyuo vingi ambavyo kiukweli vingi vikiwa havina hata sifa ya kutoa hata elimu ya sekondari na kuongeza aibu kwa taifa,kwa kuwa na wasomi wengi wasioweza hata kutengeneza hata kiberiti au kalamu.

 Huku wakitangaza matangazo yanayovutia wateja wao na kuhakikishiwa ajira za uhakika mara tu wamalizapo elimu katika vyuo hivyo. Na wanafunzi pasipo hata kutazama na kufikri kwa kina tangazo ilo lililojaa ushawishi mkubwa na wao kujirundika na kulipa ada kubwa na mwisho wa siku kumaliza na kazi kukosa na kuongeza idadi ya wale tegemezi wa ajira.

Nimalize kwa kuwaomba wadau wa elimu,walimu, wizara ya elimu na wakufunzi wa elimu  kutengeneza falsafa na motto wa elimu ya kitanzania ili tuendapo popote pale nasi tuseme falsafa ya elimu ya mtanzania ni hii. Na si kubaki kujing’atang’ata pale wageni watuulizapo sera na falsafa ya elimu ya Tanzania ni ipi tupate cha kujibu pasipo hata kufikiri sana.

 Kwa leo naweka kalamu yangu chini kuashiria nimemaliza na kuwaachia wahusika mtafakari ili elimu itakayotolewa iweze kumfanya kijana wa kitanzania kuajirika popote pale kama walivyo wenzetu Wakenya, Warundi,Warwanda na mataifa mengine ya kiafrika na duniani kwa ujumla.

Makala haya yameandikwa na mwanafunzi wa mwaka wa pili anayesomea fani ya Mawasiliano kwa Umma katika Shule Kuu ya Habari na Mawasiliano kwa Umma ya Chuo kikuu cha Dar es salaam. Anapatikana kwa mawasiliano ya 0763580901, 0716216249 au e-mail barakangofira@gmail.com.


MFUMO WA ELIMU YETU NDIYO CHANZO CHA WAHIMU KUTOKIDHI VIGEZO VYA SOKO LA AJIRA MFUMO WA ELIMU YETU NDIYO CHANZO CHA WAHIMU KUTOKIDHI VIGEZO VYA SOKO LA AJIRA Reviewed by WANGOFIRA on 01:52:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.