HIFADHI YA TAIFA YA MKOMAZI

    HIFADHI YA WANYAMAPORI YA MKOMAZI


Image result for hifadhi ya taifa mkomazi
NA, Baraka Ngofira 
0763580901, 0716216249
 Image result for hifadhi ya taifa mkomazi

Kipindi fulani nikiwa mdogo nilizoea kusikia wimbo ukiimbwa “mbuga za wanyama Tanzania ya kwanza ni Serengeti, ngorongoro, manyara na mikumi ooooh Tanzania oyeeee” kwangu ni wimbo uliokuwa ukinikaririsha mbuga za wanyama zenye kuvutia zipatikanazo nchini Tanzania.

Niliupenda huu wimbo kwani hata nilipokuwa darasa la nne, nakumbuka moja ya swali liliuliza taja mbuga nne za wanyama zipatikanazo nchini Tanzania. Kwangu sikuwa na haja ya kuangaika ninachokumbuka nikiwa ndani ya chumba cha mtihani, nilisikia wimbo huu ukuibwa akilini mwangu ndipo pasipo kupoteza muda nilijaza mbuga hizo.

Lakini kadri nilivyozidi kusoma madarasa ya juu nikafundishwa mbuga na hifadhi nyingine za wanyama pori zinazopatikana Tanzania. Nilitaka kumbishia mwalimu wangu kuwa nikiwa mdogo nilifundishwa na kuimbiwa wimbo ambao kila siku nilipaswa kuuimba kabla sijaingia darasani. Kuwa “mbuga za wanyama Tanzania ya kwanza ni Serengeti, Ngorongoro, Manyara na Mikumi ooh Tanzania oyeee”.

Sikubishana na mwalimu kwani hata wazazi wangu ni walimu nao walishiriki kunifundisha na kunikaririsha hivyo. Lakini walinambia mwanangu uendeleapo na masomo yako usiwe mbishi kwa walimu wako hata kama wakikufundisha jambo ambalo unalifahamu kwani mwalimu amekutangulia na anafahamu mengi kuliko wewe.

Na pia waliniiambia ukiona kama anakudanganya wewe nenda maktaba au muombe mwalimu wa somo husika akuazime kitabu ukajisomee mwenyewe, kwani pia ni mbinu mojawapo na ndiyo nguzo kuu ya kujifunza mambo usiyoyajua.

Nilipokumbuka kauli hii ya wazazi wangu nilienda maktaba nikaanza kusoma kwa undani kuhusu vivutio vya kitalii vinavyopatikana hapa Tanzania, kwa kweli nikashangaa kuwa karibu kila mkoa wa hapa Tanzania una mbuga au hifadhi ya wanyamapori ambao ni tuzo kubwa kwa taifa letu.

Niliporudi likizo niliwauliza wazazi wangu kuwa hivi Tanzania kuna mbuga ngapi za wanyama? Nao walinambia mwanangu kuna mbuga nyiiiingi lakini kubwa ni kama tano ambazo ni Serengeti, Manyara, Mikumi, Ngorongoro  na Selous iliyopo mkoani morogoro.

Waliponimbia hivyo nikasema kumbe ndiyo maana wimbo walionifundisha ulikuwa unataja mbuga hizo, kwa sababu ya ukubwa na wingi wa vivutio vya kitalii vipatikanavyo katika mbuga hizo? Nijisemea moyoni mwangu nitakapokuwa  nitajitahidi kwa kadri ya uwezo wangu nitembee nijionee kwa macho yangu hao wanyama wa asili wanaopatikana katika mbuga tulizonazo nchini.

Lakini sikuishia hapo nilidhamilia kuwaelimisha watanzania kutembelea na kujifunza ili waweze kuwa mabalozi wazuri wa kuitangaza nchi yetu kimataifa kuhusu vivutio vya kitalii vilivyopo nchini kwetu.

Safari yangu ilianzia Serengeti, Ngorongoro, kisha nikaenda Manyara kujionea wanyama pori hawa ambao ni tuzo kubwa tuliyojaliwa kupewa na mwenyezi Mungu. Lakini pia nilipata fursa ya kusoma katika shule kongwe ya sekondari iliyopo mkoani Kilimanjaro katika wilaya ya Hai, si nyingine ni shule ya wavulana ya Lyamungo sekondari. Nikiwa hapa kila siku mchana na jioni nilifurahia kutazama kilele cha mlima wa Kilimanjaro ambao ni mrefu Afrika na wa pili duniani.

Kwangu nilidhamiria kuupanda nikiwa sijamaliza masomo yangu katika mkoa huo na kurudi kwetu Musoma. Lakini kwa bahati mbaya sikupata fursa hiyo hadhimu, lakini ninachokifurahia nilipokuwa nikipata nafasi mimi na marafiki zangu tulienda kutembea walau Machame mahali lilipo lango kuu la kupandia mlima huu mlefu na wa ajabu.

Tulipokuwa tukifika tulipokelewa vizuri na walau kutembezwa mita kama mia mbili hivi kutoka lango kuu hilo, huku tukipewa maelekezo muhimu ya jinsi gain ya kupanda mlima huo na ni vitu gani vya msingi vya kuzingatia kabla ya kupanga safari ya kwenda kupanda mlima huo.

Lakini pia katika safari zangu nikagundua kuwa nchini Tanzania kati ya mikoa iliyobarikiwa mmoja wapo ni mkoa wa Kilimanjaro. Kwani hata hali yake ya hewa ni Baraka tosha kuruhusu matunda ikiwemo ndizi ambazo kwao mara nyingi hutumika kutengenezea pombe maarufu kama mbege, maparachichi au kwa lugha ya kigeni “Ovacado”.

Lakini pia bila kusahau mikahawa ambayo hulimwa kwa wingi karibu wilaya zote za mkoa huu, ukitoa mwanga na same ambapo kwazo hulima kwa wingi katani ambazo kwa sasa zinaonekana kukosa soko na viwanda vyake kufa.

Pia, kuna mbuga za wanyama ambazo si maarufu lakini zikiwa na wanyama wa ajabu ambao kama wakitangazwa na vyombo au idara husika zinaweza kutuletea faida kubwa katika sekta ya utalii. Si nyingine bali ni hifadhi ya wanyapori ya Kilimanjaro maarufu kama KINAPA na nyingine ni MKOMAZI ambayo ndiyo lengo langu la kuandika makala haya.

Hifadhi hii ya Mkomazi ina historia ndefu kama zilivyo hifadhi nyingine lakini pia naweza sema ni hifadhi yenye historia ndefu kuliko hata hifadhi nyingine zenye majina makubwa hapa nchini.

Ni hifadhi iliyoanzishwa mwaka 1951 hata kabla ya nchi yetu kupata uhuru, lakini haikuwa hifadhi kama ilivyo leo bali lilikuwa ni pori la akiba la Ruvu. Ikiwa na ukubwa wa kilomita za mraba 2010.4 na huku nyingine 1224.1 za pori la akiba la Umba ambalo jumla kuu ya kilomita za mraba ni 3245. inapatikana katika wilaya ya Same mkoani Kilimanjaro kilomita 6 kutoka Same mjini, 120 kutoka Moshi mjini , 155 kutoka uwanja wa ndege wa Kilimanjaro maarufu kama KIA na 200 kutoka jijini Arusha.

Imepakana na mkoa wa Tanga pia mbuga ya Tsavo iliyopo nchini Kenya ambapo wanyama wengi hususani tembo, nyati na swala hukimbilia wakati wa kiangazi na kurudi wakati wa masika. Kuhama huku kwa wanyama hawa husaidia kuweka ikolojia sawa . ndani ya hifadhi hiyo.

Ilianzishwa rasmi na kupewa mamlaka kama hifadhi ya wanyama mwaka 2007 ambapo mamlaka zinazohusika zikisaidiana na tanapa na wizara ya utalii zimejitahidi kuifanya hifadhi hii kujulikana miongoni mwa watanzania hata na nchi jirani.

Asili ya mbuga hii ni kabila la wapare ambayo inamaanisha kijiko cha tone lolote la maji yaani MKO ni kijiko na MAZI  ni tone lolote la maji. Hapo kidogo nahisi umeelewa jinsi maneno ya kipare yalivyo mafupi lakini yakibeba maana na ujumbe mkubwa. Iliitwa hivi kutokana na maeneo ipatikanapo mbuga hii kuwa maeneo makame sana ambapo upatikanaji wa maji ni wa shida.

Kutokana na jiografia ya wilaya ya same kuwa na vimilima vingi vilivyo jaa miamba na hivyo kusababisha upatikanaji wa  maji kuwa wa shida lakini mbali na shida hiyo wanyama wanaopatikana hifadhini hapa uishi kwa kutegemea vidimbi vidogo vidogo ambavyo uhifadhi maji wakati wa mvua  na kukauka wakati wa jua kali.

Wakati mzuri wa kutembelea hifadhi hii, ni kuanzia mwezi juni mpaka januari ambapo wanyama wengi huwa wamerudi kutoka mbuga ya Tsavo ambapo uenda kipindi cha kiangazi na kurejea wakati wa masika ambapo maji na chakula kama nyasi huwa ni nyingi hifadhini humo.

Vivutio vya kitalii vipatikanavyo ndani ya hifadhi hii ni kama vingine vinavyopatikana katika hifadhi nyingine za hapa nchini lakini vipo vingine ambavyo ni tofauti kabisa na hupatikana ndani ya hifadhi hii pekee ambavyo ni vifaru weusi ambao walitolewa nchi Afrika Kusini mwanzoni mwa miaka ya 1990.

Faru hawa ni wa ajabu kutokana na kuwa na rangi tofauti na faru wengine wapatikanao katika mbuga nyingine za hapa nchini. Na hivyo kuwa kivutio kikubwa kwa watalii wengi kwenda kutembelea hifadhini hapa, ili kujionea kwa macho yao jinsi faru hawa walivyo na wanavyoipamba mbuga hii ambayo wengi wa watanzania hawaifahamu.

Pia, kuna ndege aina mbalimbali wakiwemo Tai, na mbuni na wenginewo wengi ambao hupamba na kuing’arisha hifadhi hii. Ndege hawa hususani Tai na mbuni husifika kwa ujasiri wao wa kuweza kupambana na kuwamudu vyema maadui na wanyama wengine hatari wanatakao kufupisha maisha yao.

Ndege hawa ni wa ajabu sana, na hivyo kuwa kivutio kikubwa sana kwa watalii japo huwa ni adhimu sana kuwaona kutokana na wao kupenda kujificha kwenye mapori na vichaka vidogo vidogo. Ni mara chache sana kuonekana kwa watalii wengi, hivyo wewe kama mtanzania unapaswa kwenda kujionea kwa macho yako jinsi gani ndege hawa wa ajabu wafananavyo.

Pia, ndani ya hifadhi hii utawaona mbwa nap aka mwitu ambao wanapendezesha mbuga hii. Mbwa na paka mwitu hawa ni wanyama kama wale tuwafugao majumbani lakini tofauti yao ni kwamba, mbwa nap aka hawa wana rangi nyeusi na nyuso zao zimechong’oka na uwezo wao wa kukimbia na kupambana na maadui ni mkubwa kuliko paka na mbwa mwitu wa kufuga.

Wengine ni wanyama wa kawaida ambao karibu kila hifadhi upatikana kama vile tembo, swala, digidigi, twiga, nyati na wengine wengi, hivyo ni jukumu lako wewe kama mtanzania kupenda chako na kuthamini maliasili zetu tulizonazo hapa nchini. Jiulize ni wageni wangapi wamekuja kutazama wanyama hawa tena kwa gharama kubwa lakini sisi wazawa walio wengi hawaoni haja ya kutembelea hifadhi hizi. Ebu tuchangamkie fursa wakati ndiyo huu.

Mbali na wanyama hawa kuna milima ya upare na usambala ambayo imekuwa kivutio kikubwa cha kitalii hasa kwa wageni waendao kutembelea hifadhini hapa. Milima hii imekewa maarufu kwa ilivyojengeka, miamba yake na udongo wake ambapo maporomoko ya milima hii ndiyo uwaacha watalii hoi kwani, ilivyojengeka ni vigumu kuadithia ili mtu aelewe kwa urahisi. Lakini kwa wengi waliowahi kufika na kujionea mlima hii wanaweza kuelezea ni jinsi gani milima hii ya ajabu.

Mbali na vivutio hivyo hifadhi hii bado unakabiliwa na changamoto kubwa ya kukosa hoteli na nyumba za malazi za kutosha kwa wageni na watalii hawa na hivyo kutumia muda mwingi na mrefu kwenda kujipumzisha mjini Same. Tofauti na ilivyo hifadhi ya taifa ya Serengeti na Ngorongoro.

Hivi ushawahi kujiuliza ni kwa nini wageni hawa au wazungu wengi hutoka ulaya, Marekani na sehemu nyingine duniani kuja Tanzania kuona wanyama? Huku wewe umekaa na kuwashangaa tu, utadhani wanapoteza muda wao.

Hivyo basi chonde chonde mtanzania mwenzangu panga kutembelea mbuga na vivutio vyetu vya kitalii vipatikanavyo hapa nchini kwetu, ili ujionee mwenyewe na ufurahie utanzania wako.


Makala haya yameandikwa na mwanafunzi wa mwaka wa pili wa shahada ya kwanza ya Mawasiliano kwa Umma ya Shule Kuu ya Uhandishi wa Habari na Mawasiliano kwa umma ya Chuo Kikuu cha Dar es salaam (UDSM-SJMC) anapatikana kwa mawasiliano ya email ya barakangofira@gmail.com au simu namba 0763580901 au 0716216249
HIFADHI YA TAIFA YA MKOMAZI HIFADHI YA TAIFA YA MKOMAZI Reviewed by WANGOFIRA on 06:34:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.