LOWASA ASEMA CCM WEZI WA KURA

Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad na
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad na mgombea urais wa muungano wa Ukawa, Edward Lowassa wakiwapungia mkono wananchi waliofurika makao makuu ya CUF, Buguruni jijini Dar es Salaam jana. Picha na Anthony Siame 
Dar es Salaam. Mgombea wa urais kupitia Chadema, Edward Lowassa ameituhumu CCM kuwa ni hodari wa kuiba kura hivyo akawataka wananchi wajitokeze kwa wingi kupiga kura ili hata sehemu ya kura hizo ikiibiwa, Ukawa ishinde kwa kishindo.
Lowassa ambaye ni waziri mkuu wa zamani aliuambia umati wa wafuasi wa Ukawa uliojitokeza jana kumpokea katika ofisi za makao makuu ya CUF yaliyopo Buguruni kuwa ili kufanikisha ushindi wa kuwawezesha kuingia ikulu hawana budi kushikamana, kushawishiana kupiga kura kwa wingi na kuzilinda Oktoba 25.
Kauli hiyo ya Lowassa ambaye amelelewa kisiasa na CCM tangu alipojiunga akiwa mdogo mwaka 1977, inaendeleza tuhuma ambazo hutolewa na vyama vya upinzani kuwa chama hicho huchakachua matokeo wakati wa uchaguzi.
Hata hivyo, Lowassa hakuwa na vielelezo wala kuthibitisha kuhusu tuhuma hizo dhidi ya chama chake cha zamani.
“Tukiwa na umoja, tukiwa na mshikamano tutawaondoa Jumapili asubuhi sana. Tutahitaji mshikamano, tatahitaji ushawishi wa kupiga kura tupate angalau asilimia 90 ili wakiiba asilimia 10 tuwasamehe,” alisema Lowassa katika hotuba yake iliyokuwa inakatishwa na kushangiliwa na na salamu ya CUF ya “Hakiii” na kujibiwa “kwa wote.”
“Hodari sana wa kuiba CCM kura. Sasa tupate kura nyingi za kutosha hata wakiiba kura hausikii na kuna usemi wa Chadema unaosema ‘piga kura, linda kura’ na sisi CUF ni hodari sana wa mambo hayo.”
Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alipotafutwa kwa simu kuhusu madai hayo, alijibu kwa ujumbe wa maneno kuwa asingeweza kuzungumza bali atumiwe ujumbe, na alipotumiwa ujumbe huo hakujibu.
Lubuva: Aeleze wanaibaje
Akizungumzia madai hayo, Mwenyekiti wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC)  Jaji mstaafu, Damian Lubuva alisema Lowassa angeeleza jinsi wanavyoiba kura.
“Ili kutoa majibu ya uhakika naomba tufanye utafiti wa kutosha juu ya tuhuma hizo, lazima tujue ni njia zipi watu wanaiba, vinginevyo nitaeleza kitu ambacho sina ufahamu nacho. Yeye (Lowassa) kama mtu aliyekuwa serikalini lazima ana ufahamu walikuwa wanaiba vipi, angeeleza.”
Tume huwa inaendesha uchaguzi kwa mujibu wa taratibu na sheria na iwapo kuna mtu anasema kura zinaibwa ajitokeze aeleze kinagaubaga ili ofisi yake ifanye utafiti wa kina.
“Naomba nieleweshwe kura huwa zinaibiwa vipi? Hii imekuwa ni hisia, wengine wanasema tutaibiwa kura zetu wakati upande mwingine unasema hawa wataleta fujo kwa visingizio vya kuibiwa kura,” alisema Jaji Lubuva.
Lowassa ambaye alihamia Chadema siku 11 zilizopita na baadaye kuteuliwa kugombea urais kwa mwamvuli wa Ukawa kupitia Chadema, alisema safari ya Ikulu itafanikishwa kwa kupiga kura na siyo maandamano, hivyo Watanzania watunze shahada za kupigia kura. Hata hivyo, hakuendelea kueleza undani kuthibitisha ni namna gani CCM huiba kura.
Kiongozi huyo aliyeonekana mwenye furaha, aliwataka wanawake nao kujitokeza kwa wingi siku ya upigaji wa kura huku wakiwa wameshapika vyakula majumbani mwao ili nao wapate fursa za kupiga na kulinda kura.
Lowassa alisema ameingia Ukawa ili kuandika historia ya nchi kukuza uchumi na kuondoa umaskini na kutekeleza kauli ya Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere ya “mabadiliko ya kweli yatapatikana nje ya CCM.”
Ukawa kutoyumba
Mbunge huyo wa Monduli anayemaliza muda wake, alisema Ukawa ipo imara haitayumbishwa kirahisi na wafitini, licha ya baadhi ya watu kujipitisha kwa viongozi wa juu na kutaka kuwarubuni ili umoja huo utetereke.
“Wanakuja kupitisha hela na kuhongahonga lakini viongozi wapo imara…hawahongeki hawa! Wanapita na maneno kwenye magazeti ya ufukuzi ufukuzi, nawaambia muwapuuze,” alisema Lowassa bila kuwataja wahusika.
Alisema kuna baadhi ya watu wanaleta propaganda kuwa Ukawa ikiingia madarakani nchi haitatawalika kiasi cha kuwatisha wafanyabiashara kukimbiza fedha zao nje ya nchi, jambo ambalo si la kweli.
“Waongo wakubwa hao…nchi itatawalika kuliko awali, Ukawa ikiingia madarakani nchi itatulia tuli, wasiwadanganye mkimbize hela zenu..tupo imara,” alisema.
Juma Duni afafanua
Mgombea mwenza wa urais wa Ukawa, Juma Duni Haji alisema hajahamia Chadema kutafuta vyeo kwa kuwa ameondoka akiwa Makamu Mwenyekiti wa CUF na waziri katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, na hatua yake hiyo ni kutimiza za kuing’oa CCM madarakani.
“Ni vizuri mkaelewa kwamba tutafanya kosa kubwa tusipofika ikulu mwaka huu, tutahitaji kusubiri miaka 50 zaidi maana jamaa hawa wakija kutulia balaa yao ni mara 100 ya wanayoyafanya. Wanaoleta mabadiliko ni vijana siyo wazee,” alisema Duni Haji.
Alisema Ukawa wanatakiwa kushirikiana kwa dhati na Watanzania kwa ujumla kwa kuwa mwaka huu ni wa mageuzi na kila mmoja ana wajibu wa kufanya kampeni ya kuiondoa CCM ili kutafuta hatima bora ya nchi.
Kauli ya Mbowe
Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema kuna nguvu nyingi zinatumika kuivunja Ukawa lakini umoja huo utabaki kuwa imara na kutimiza malengo yake ya kushika dola mwaka huu kwa nguvu za Mungu.
Alisema vyama vya upinzani vimefanya siasa zao kwa shida kwa miaka 25 huku baadhi ya makada wakifungwa, kufukuzwa kazi, ndoa kuparaganyika, kufungwa au kufunguliwa kesi mahakamani lakini miezi minane iliyopita imekuwa migumu zaidi kutokana na baadhi ya watawala kupatwa na hofu baada ya Ukawa kujiimarisha.
“Safari yetu imebaki kidogo tufike tunakoelekea. Sasa akitokea kiongozi mmoja wetu bila kujali ni wa chama gani akaona kwamba malengo yetu siyo ya muhimu kuliko fursa binafsi, huyo hatufai,” alisema Mbowe na kushangiliwa.
Alisema maandamano ya leo kumsindika Lowassa kuchukua fomu yataanzia CUF na kupitia ofisi za Makao Makuu ya NCCR-Mageuzi Ilala hadi NEC kabla ya kurudi ofisi za Chadema Kinondoni.
Mwenyekiti wa NLD, Dk Emmanuel Makaidi aliwataka wafuasi wa Ukawa kujitokeza kwa wingi kumsindikiza mgombea wa urais kupitia umoja huo na ikiwezekana kila mfuasi apeleke watu 10.
Mbatia amvaa JK
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia alisema Ukawa itaendelea kuhubiri amani siku zote ili CCM na vyombo vya dola visipate sababu ya kuwatuhumu na kwamba Uchaguzi Mkuu utafanyika kwa amani.
Alisema Rais Jakaya Kikwete alihubiri chuki dhidi ya wapinzani kwa kuwaita maadui siku alipozungumza na wafuasi wa CCM baada ya kumpokea mgombea wa urais kupitia chama hicho, Dk John Magufuli alipotoka kuchukua fomu za kuwania.
 “Sikuamini kama Rais Kikwete angesema maneno yale eti anawaambia wana-CCM wana mikakati ya kila aina ya kushinda na kwamba ‘msiogope kujihadhari na nguvu za adui’. Yaani sisi wapinzani ni adui? Ukianza kuwaita wenzio adui wakati wewe ni amiri jeshi mkuu, nchi hii unaipeleka wapi?” alihoji Mbatia.
Malim Seif apongeza
Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, aliwashukuru wafuasi wa Ukawa waliojitokeza kumpokea Lowassa wakati wa ziara ya kutembelea ofisi zao na kwamba moyo huo uendelee hadi Oktoba 25 siku ya kupiga kura.
“Hakuna silaha kubwa kuliko umoja, ushirikiano na mshikimano. Tukishirikiana tukawa wa kweli wa nafsi zetu bila shaka Lowassa anasubiri kuapishwa tu na sisi Zanzibar tumeshamaliza kazi,” alisema Maalim Seif na kushangiliwa na umati wa wafuasi hao.
Hali ilivyokuwa
Mapema kabla ya Lowassa hajawasili Buguruni wafuasi wa CUF walianza kujikusanya taratibu saa 4 asubuhi kwa kuzunguka na ngoma barabara za Uhuru na za mitaa kuingia ofisi za chama hicho.
Baadaye umati huo uliongezeka kiasi cha kufunga barabara ya Uhuru kwa muda wakati Lowassa anaingia saa 6:20 mchana na kupokelewa na Maalim Seif, Makaidi, Mbatia na viongozi waandamizi wa Ukawa.
Idadi hiyo ya watu iliwapa kibarua maofisa usalama wa Ukawa walioonekana wakihaha kutengeneza njia ili viongozi hao wapite.
Baada ya viongozi hao kuwahutubia wafuasi hao, waliingia katika ukumbi wa Mkutano wa Baraza Kuu la Uongozi saa 7:15 mchana na kufanya mazungumza ya takriban saa moja na baadaye viongozi kutoka nje ya CUF kuondoka.
Nafasi ya Lipumba
Kikao cha Baraza Kuu kilijadili nafasi ya mwenyekiti iliyoachwa na Profesa Lipumba na suala hilo liliachiwa Mkutano Mkuu wa chama ambao utaitishwa baada ya miezi sita kwa kuwa ndio wenye uwezo wa kufanya uchaguzi huo kwa mujibu wa katiba ya CUF.
Akitoa taarifa ya kikao hicho, Maalim Seif alisema Baraza Kuu limeunda kamati maalum ya watu watatu itakayofanya kazi na katibu mkuu kwa miezi sita kabla ya Mkutano Mkuu kukaa na kumchagua mwenyekiti na makamu wake, nafasi ambazo ziko wazi.
Waliochaguliwa kwenye kamati hiyo ni Twaha Taslima ambaye ni mwenyekiti na wajumbe wawili ambao ni Aboubakary Khamis Bakary (Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar) na Sererina Mwijage (mbunge mstaafu wa viti maalumu.
LOWASA ASEMA CCM WEZI WA KURA LOWASA ASEMA CCM WEZI WA KURA Reviewed by WANGOFIRA on 03:07:00 Rating: 5

No comments:

Powered by Blogger.